STAA wa Misri, Mohamed Salah, atakosa mchezo mmoja tu wa Kombe la Dunia baada ya hapo atakuwa fiti. Salah aliumia bega kwenye mchezo wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid baada ya kuumizwa na Sergio Ramos.

 

Hata hivyo, kulikuwa na hofu kuwa staa huyo atashindwa kucheza fainali hizo lakini sasa imefahamika kuwa atakwenda na kukosa mchezo mmoja tu kwa kuwa kuanzia leo atakuwa nje kwa wiki tatu tu.

Shirikisho la Soka la Misri, limesema kuwa madaktari wanapa-mbana kuhakikisha kuwa mchezaji huyo anakuwa fiti.

 

Salah anaendelea na matibabu nchini Hispania na ataungana na wenzake hivi karibuni kabla ya safari ya kwenda Urusi kwenye fainali hizo ambazo zitaanza Juni 14.

“Mohamed Salah atakuwa nje kwa wiki tatu, kutokana na jeraha ambalo alilipata kwenye fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya nchini Ukraine.

“Atakuwa kwenye Kombe la Dunia, lakini atakosa mchezo dhidi ya Uruguay, ingawa bado juhudi zinaendelea kuhakikisha anakuwa fiti.

 

“Wakati huu anaendelea na matibabu, atakuwa nje ya kambi ya mazoezi na wenzake,” ilisema taarifa kutoka kwenye shirikisho hilo.

Salah ndiye staa wa Misri baada ya kumaliza msimu akiwa na mabao 44, kwenye klabu yake ya Liverpool na kuibuka mfungaji bora wa Ligi Kuu England. Misri wapo kundi A, wakiwa na wenyeji Urusi, Saudi Arabia na Uruguay.

By Jamhuri