MAANDIKO YA MWALIMU NYERERE
Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (4)
Huu ni mtiririko wa maandishi yaliyomo kwenye kitabu cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania kilichoandikwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, mwaka 1994. Sehemu iliyopita, Mwalimu alisema, “Kwa kweli hata kesho Nchi za Afrika ya Mashariki zikiamua kuungana, na Tanzania ikawa ni mshiriki, naamini kuwa ni rahisi zaidi kushirikisha Tanzania yenye Serikali Mbili – ya Zanzibar na ya Tanganyika – kuliko Tanzania yenye Serikali Mbili, ya Tanzania na ya Zanzibar. Wapendao Utanganyika watakuwa wazalendo zaidi, badala ya kuwa wasaliti, wakiazimia Afrika ya Mashariki iliyoungana kuwa Nchi Moja, kuliko Tanzania iliyotengana ikawa nchi mbili.” Endelea…..
Siku ya pili yake tarehe 15:8:1993, Wabunge wenye hoja yao, na wengine zaidi, waliomba tena kuja Msasani ‘Tunywe chai’. Na baada ya mazungumzo nao ilikuwa ni dhahiri kabisa kwangu, kwamba hata kama hawakuondoa hoja yao, (wala mimi sikuwaomba waiondoe), wataitumia kutoa dukuduku zao tu; hawataitumia kung’ang’ania kudai Serikali ya Tanganyika.