Baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry, kusafisha njia Kenya kwa ziara ya siku tatu aliyoifanya mwanzoni mwa mwezi huu, imethibitika kuwa Rais Obama atatua Nairobi kwa ulinzi mkali na kufanya ziara ya saa 8 tu.
 Ziara hii ya kihistoria itafanyaka mwishoni mwa mwezi Julai, lakini mpaka sasa Ikulu ya Marekani ‘White House’ imejizuia kutoa taarifa zaidi ikiwa ni pamoja na kutaja tarehe, lakini taarifa ambazo gazeti la JAMHURI limezipata zinathibitisha kwamba Rais Obama atakaa Kenya kwa saa 8 sawa na dakika 480.


 Ziara ya kiongozi huyo wa taifa kubwa duniani ambaye ana asili ya Kenya kutokana na baba yake, Hussein Obama kuwa ni raia wa Kenya, itakuwa na ulinzi ambao hata mwenyeji wake, Rais Uhuru Kenyatta watakuwa kando.
  “Walinzi wa Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, siku hiyo hawatakuwa na nafasi. Aliyekubaliwa ni mpambe wake tu ‘ADC’ na sektretari wake,” inasema taarifa hiyo kiintelijensia.
  Vikosi vya ulinzi vya Marekani vinakusanya walinzi wa karibu wa Rais wa Marekani ‘Secret Service,’ CIA na FBI pamoja na wakuu wa Ikulu tayari wametua Kenya na kuwa na vikao na wakuu wa usalama nchini humo kupanga ziara ya Obama. Wamepanga kushika dola nzima ya ulinzi ya Kenya na majeshi ya nchi hiyo.


 Meli ya kivita ya Marekani ipo njiani kuingia Bahari ya Hindi kuja karibu ya Kenya kama njia ya kudumisha usalama. Taarifa zinasema Jeshi la Wanamaji ndilo litakaloongoza usalama upande wa bahari katika nchi zote za Afrika Mashariki.
  Jeshi hilo lenye meli za kivita lililopewa jina la Abraham Lincolin limeandaliwa kwa kazi moja tu kujiandaa na shambulizo la kivita baada ya kubeba silaha nzito za B52. Itakuwa imeegeshwa pwani ya Mombasa.
  Kikosi hicho maalum kinatarajiwa kuweka mikakati ya kumlinda Rais Obama iwapo kutakuwa na jaribio lolote la kuhatarisha maisha yake atakapokuwa Kenya.


  Maofisa hao kutoka kitengo cha Recce na Idara ya Jeshi la Kenya wanatarajiwa kufanya doria katika sehemu mbalimbali za jiji la Nairobi na kudhibiti umma wakati wa ziara hiyo.
  Barabara zote kuu za Kenya zitafungwa na kutakuwa na ‘satellite’ kutoka Texas, Marekani na kusimamiwa vema na vifaa vya jeshi vitakavyokuwa kwenye kambi za jeshi nchini Kenya. Hakuna meli ya biashara itakayoruhusiwa kutia nanga Bandari ya Mombasa.
  Rais Obama anatarajiwa kuwasili nchini Kenya akitumia ndege ya Rais wa Marekani ‘Air Force One’ aina ya Boeing 747-200B na kisha kutumia gari yake anayoitumia akiwa nchini Marekani, inayodaiwa kuwa salama zaidi duniani.


 Vikosi hivyo vya CIA, FBI vinatarajiwa ‘kuiteka’ Kenya kila pembe kutokana na kuwa na mikakati ya kuhodhi Ikulu, Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta pamoja na viwanja vingine ikiwa ni pamoja na bandari zote za Lamu na Mombasa.
  Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta utafungwa kwa kutoruhusu ndege za mashirika mengine kutua au kupaa.
  Uwanja huo utakuwa na kazi moja tu kuhudumia ndege ya Air force One ambako wafanyakazi wake watakuwa likizo kwa siku hiyo kwani maeneo yote yanashikwa na Jeshi la Marekani.  


  Mamlaka ya Anga ya Marekani pamoja na Makao Makuu ya Jeshi hilo Pentagon watakuwa wakifanya kazi siku hiyo bila kuhitaji msaada wa vikosi vya ulinzi vya Kenya.
  Ndege hiyo imetengenezwa kuweza kutoa huduma ya umeme iwapo Shirika la Umeme la Kenya litakwama ina uwezo wa kukata umeme moja kwa moja bila kusubiri kukimbilia kwenye mitambo kisha ikapaa hata kama ni gizani bila kuwasha taa, vikosi vya CIA ndivyo vitakavyosimamia kazi hiyo.
 Taarifa zinasema wafanyakazi wote wa Serikali watakuwa likizo ya siku tatu kupisha ziara ya Rais Obama na gari atakalotumia Rais Obama litakuwa na vifaa maalum kuzuia aina yoyote ya milipuko kuilipua.


  Taarifa za kiintelijensia zinasema anga la nchi za Tanzania, Somalia, Eritrea, Uganda, Rwanda na Burundi zitafungwa na kwamba kwa saa hizo nane, simu zote za mkononi nchini Somalia zitazimwa.
  Kerry aliyekuwako Kenya kwa siku tatu kabla ya kuzuru Somalia, alikuwa na ajenda ya usalama hasa baada ya wanamgambo wa al-Shabaab kutoka Somalia kuwa na matukio ya kulipua maeneo mbalimbali ya Kenya, ikizingatiwa kuwa mwezi mmoja uliopita walifanya shambilio katika Chuo Kikuu cha Garissa na kuua watu zaidi ya 150.


 Vikosi maalum kutoka Marekani vya CIA na FBI vimeanza kuwasili nchini Kenya kujiandaa na usalama wa Rais Obama anayetarajiwa kuzuru Kenya mwezi Julai.
 Obama anatarajiwa kufanya mkutano na Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na baadaye wote wawili kuhudhuria Kongamano la Ubunifu wa Kibiashara Ulimwenguni la 2015 litakalofanyikaa jijini Nairobi.
  Kongamano hilo linajumuisha viongozi mbalimbali wa kibiashara, mashirika ya kimataifa na serikali.


 Wataalamu wa masuala ya kiuchumi wa Kenya wametafsiri ziara hiyo kuwa mwanzo mpya wa kufufuka kwa uhusiano uliofifia wa kirafiki na kibiashara baina ya Kenya na Marekani.
  Katika miaka ya hivi karibuni Kenya imeshirikiana zaidi kibiashara na China na Japan na ziara hiyo ya Obama imetafsiriwa na vyombo vya habari vya duniani kama kuboresha uhusiano katika ya nchi hizo mbili.
  Hii itakuwa ziara ya tatu ya Obama kuja Afrika baada ya mwanzo kutembelea Ghana, baadaye Senegal, Afrika Kusini na Tanzania. Hakuzuru Kenya akiishutumu kuwa imekithiri kwa rushwa.


  Hata hivyo, Rais Obama alichelewa kuzuru Kenya kutokana na kesi ya tuhuma ya uhalifu dhidi ya binadamu iliyokuwa ikimkabili Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, na Makamu wake, William Ruto, iliyofunguliwa katika Mahakama ya Uhalifu wa Kivita (ICC) yenye makao makuu mjini the Hague.
  Obama anadaiwa kukubali zira hiyo baada ya kufutwa kesi dhidi ya viongozi hao kwa kukosekana ushahidi. Mwaka jana baada ya kesi ya Uhuru Kenyatta kufutwa, Kenya iliongeza idadi ya uagizaji wa bidhaa kutoka Marekani kwa asilimia 165.3 kuwa dola bilioni 1.5 kutoka dola milioni 594.5
  Taarifa zinasema kwamba ratiba ya Rais Obama imebana kiasi kwamba hatapata muda angalau wa kumuona au kuteta na nyanya yake – mke wa tatu wa babu yake, ambaye anaishi katika kijiji kimoja magharibi mwa Kenya.


 Tangu alipochaguliwa mara ya kwanza mwaka 2008, Rais Obama hakuwahi kutia mguu nchini Kenya alikozaliwa baba yake.
  Obama akiwa Seneta wa Illinois aliwahi alitembelea Kenya mwaka 2006, ambapo alikwenda kumuona hata bibi yake.
  Hussein Obama, baba yake Barack, alisomea Marekani na kurejea Kenya baada ya kuwa amemzaa Barack nje ya ndoa akiwa masomoni.

By Jamhuri