Eric Omondi

Mchekeshaji maarufu Afrika Mashariki kutoka Kenya Eric Omondi amejipata taabani kutokana na video yake iliyosambaa mtandaoni ambapo anaonekana akicheza na watoto mtoni, wote wakiwa utupu.

Video hiyo ambayo inadaiwa kupigiwa katika mto mmoja eneo la Lodwar katika jimbo la Turkana, kaskazini magharibi mwa Kenya.

Video hiyo imeibua hisia kali mtandaoni, baadhi wakimshutumu vikali na wengine wakimuunga mkono.

Bw Omondi ameandika ujumbe wa kuomba radhi katika ukurasa wake wa Instagram.

“Nimekuwa mchekeshaji maisha yangu yote…Mara nyingi nimekosea…Leo imekuwa moja ya siku hizo. Nimewakera wengi. Sikukusudia kumkera au kumuudhi mtu yeyote kwa njia yoyote ile …. Naomba radhi kwa hilo.”

Afisa mkuu mtendaji wa Mmalaka ya Kusimamia Viwango vya Filamu na Video (KFCB) Bw Ezekiel Mutua ni miongoni mwa waliomshutumu sana mchekeshaji huyo.

Bw Mutua alisema atahakikisha Bw Omondi amechukuliwa hatua.

“Kutumiwa vibaya kwa watoto ni kosa kubwa. Hivi ndivyo hawa watu wanavyojiita watu mashuhuri wanavyoishia kuwadhalilisha watoto…. Hiyo video yake akiwa utupu na watoto ni ya kuudhi!”

“Video hii inakiuka tu sio mwongozo wa KFCB katika moyo wa Sura 222, bali pia inakiuka Sheria ya Watoto. Wazazi wa watoto hawa wanafaa kumshtaki Eric Omondi kwa kuwadhalilisha na kuwafedhehesha watoto wao.”

Siku za karibuni, Eric amekuwa akiigiza upya maarufu za muziki na filamu kwa njia ya utani na ucheshi video mbalimbali.

Mwaka uliopita, mchekeshaji huyo aliigiza video ya ucheshi ya ‘Gods are not crazy, we are’ ambapo alitania filamu maarufu barani Afrika ‘Gods must be crazy’ . Kwenye filamu hiyo, alikuwa amevalia nguo fupi iliyoficha tu uchi wake.

Eric Omondi

Miongoni mwa nyingine, ameandaa video za marudio ya wimbo ‘Salome’ wake Diamond Platinumz na Rayvanny ambao aliuita ‘Sang’ombe’ na filamu fupi ya ‘Sarafina’ aliyoiita ‘Saratina’.

Amekuwa akiigiza pia ‘jinsi ya kuwa’ watu maarufu wakiwemo Rais wa Tanzania John Magufuli, mwanamuziki Mkenya Akothee na mwanamuziki Mtanzania Diamond Platinumz.

By Jamhuri