Mashehe watano waliotoweka katika mazingira ya kutatanisha kuanzia Febuari 9 mwaka huu huko Zanzibar wameachiwa na kurejea katika familia zao usiku wa kuamkia Machi 4, 2018.

Mashehe hao walitoweka ikiwa hakuna aliyekuwa akifahamu walipokwenda, huku wana familia wakiitaka serikali kufanya uchunguzi ili kuweza kubaini walipo ndugu zao.

Mmoja wa Mashehe hao, Amir Khamis akifanya mahojiano na Azam Tv alisema kuwa hajui eneo walilopelekwa, lakini waliohojiwa na baada ya kuonekana hawana hatia waliachiwa bila kudhuriwa.

“Mimi na wenzangu wanne tulipelekwa kusikojulikana na baada ya kuhojiwa wametuachia tukiwa salama. Wale waliotukamata hawakuwa na nia mbaya…walikuwa wakitekeleza kazi yao ya usalama…na ndio maana baada tu ya kugundua kwamba sihusiki na y ale waliyokuwa wakinihoji waliniachia huru na nimerudi nyumbani…niko na familia yangu,” alisema Khamis.

Mmoja wa wanafamilia wa Shehe Khamis alisema kuwa alikuwa na hofu kwamba huenda ndugu yao hayupo hai, hivyo wamefurahi na kufarijika sana kumuona tena.

“Tulikuwa na hofu kwamba yawezekana ametupwa baharini au vinginevyo, lakini tunamshukuru sana Mungu kwa kumrejesha akiwa salama,” alisema Mke wa Shehe Khamis, Mwanaunguja Hadhar baada ya mumewe kurejea nyumbani.

By Jamhuri