Huyu ndio Ronaldo Bana Apiga Hat Trick

Mtanange uliokuwa unasubiriwa kwa hamu Afrika na pande zingine duniani baina ya Spain na Ureno umemalizika kwa timu zote kuambulia alama moja baada ya dakika 90 kumalizika kwa sare ya 3-3.

Mechi hiyo imepigwa kwenye Uwanja wa Fisht uliopo Sochi huko Russia na kuweza kushuhudia nyavu za Spain zikitikiswa mapema na Ronaldo kwa njia ya penati mnamo dakika ya 4 ya mchezo.

Spain walikuja juu na kusawazisha katika dakika ya 24 kupitia nyota wa Atletico de Madrid, Diego Costa na ikiwa imesalia dakika moja kuelekea mapumziko, Ronaldo akafunga tena bao la pili na kufanya ubao usomeke 2-1.

Mpaka dakika 45 za kwanza zinamalizika Ronaldo alikuwa ameipeleka timu yake mbele kwa mabao hayo mawili kwa moja

Kipindi cha kilianza kwa kasi huku Spain wakisaka bao la kusawazisha ambapo kwenye dakika ya 55, Costa tena alitia kambani na kufanya matokeo ya mchezo huo kuwa 2-2.

Ilichukua dakika tatu tu Nacho kuweza kuiandikia tena Spain bao la tatu huku kwa kutikisa nyavu za Ureno katika dakika ya 58.

Mnamo dakika ya 88 tena zikiwa zimesalia dakika mbili dakika 90 kumalizika, Ronaldo alifunga bao la tatu kwa Ureno na kufanya matokeo yamalizike kwa mabao 3-3.

Mabao matatu aliyofunga Ronaldo yanamfanya kuwa mchezaji pekee wa kwanza kuweka rekodi kwenye michuano ya Kombe la Dunia mwaka huu kufunga hat trick.