JPM AWALILIA MAPACHA WALIOUNGANA “WALIKUWA NA NDOTO KUBWA”

Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli ametuma salamu za rambirambi kwa familia, Masista wa Maria Consolata na wote walioguswa na kifo cha mabinti mapacha walioungana Maria na Consolata Mwakikuti waliofariki dunia jana jioni katika hospitali ya Mkoa wa Iringa.

 
Mhe. Rais Magufuli aliwatembelea Maria na Consolata walipokuwa wakipata matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Jijini Dar es salaam tarehe 06 Januari, 2018. Pamoja na kuwapa pole, Maria na Consolata waliongoza sala ya kuliombea Taifa na Viongozi wake.
Mhe. Rais Magufuli anasema anatambua kuwa Maria na Consolata walikuwa na ndoto kubwa ya kuja kulitumikia Taifa baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha Masista wa Consolata Ruaha (RUCO) walikokuwa wakiendelea na masomo yao, lakini haikuwa hivyo.
Amewaombea Mwenyezi Mungu aziweke roho zao mahali pema peponi, Amina.