Kiongozi wa kikundi cha wapiganaji wa Boko Haram Abubakar Shekau, ameonekana kwenye video mpya karibu saa ishirini na nne baada ya Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari kwa mara ingine kutamka hadharani kuwa kikundi hicho kimesambaratishwa.
Huu ni mkanda wa video wa kwanza kutolewa na Shekau baada ya kimya cha miezi kadhaa iliyopita, naye ni mongoni mwa viongozi wanaosakwa kwa hamu na ghamu na kupewa sifa ya kuwa miongoni mwa magaidi wanaosakwa na Marekani pamoja na mamlaka ya Nigeria.
Abubakar Shekau anaonekana kwenye mkanda huo wa video akiwa ameketi peke yake akiwa amevalia kanzu,kofia yenye rangi inayofanana na bunduki aina ya AK-47 ambayo anaonekana kuwa na mahaba nayo.Lakini anaonekana kushindwa kuzungumza kwa sauti yenye mamlaka ikilinganishwa na matamko yake ya awali .
Akisoma kutoka katika karatasi kwa lugha ya kiarabu na ki Hausa, Shekau, anakiri kundi lake kuhusika katika matukio ya hivi karibuni nchini Nigeria katika maeneo ya kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo ikiwemo lile lililotukia siku ya siku kuu ya Christimas katika kijiji cha Molai nje ya jiji la Maiduguri, mji mkuu wa Jimbo la Borno.
Shekau alijinasibu kwa kusema kuwa askari wa kundi la wanamgambo la Boko Haram wana afya maridhawa na kwamba vikosi vya ulinzi nchini Nigeria haviwezi kufanya lolote dhidi ya wanamgambo wake.
Sehemu ya dakika thelathini na moja ya mkanda huo zimeoneshwa mbwembwe za wapiganaji wa kundi hilo ikiwemo magari ya silaha, malori na pikipiki huku wakinapiga risasi hewani kwa kile kinachoonekana kizuizi cha njiani katika kambi ya kijeshi iliyotelekezwa .
Wakati huo huo Shekau alionekana akitoa tamko juu ya kukerwa kwake dhahiri juu ya kutambuliwa hivi karibuni mji wa Yerusalemu kama mji mkuu wa Israeli tamko lililotolewa na Rais wa Marekani Donald Trump, Abubakar Shekau, ameijosoa nchi ya Saudi Arabia kwa kushirikiana na wale aliowaita makafiri na kuwalaumu Wapalestini kwa uharibifu wao.
Mpaka sasa serikali ya Nigeria haijatoa tamko lolote juu ya mkanda huo wa video na ujumbe uliomo ndani yake. Hata hivyo jeshi la Nigeria linakiri kuwafukuza waasi kutoka katika ngome zao kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo, hata hivyo wanamgambo wa kikundi cha wapinaji cha Boko Haram bado wanaendeleza mashambulizi ya kujitoa muhanga , mashambulizi ya risasi za moto zaidi wakilenga vifaa vya kijeshi na vijiji.

By Jamhuri