Kizimbani kwa kutishia kumuua Miranda Kerr

Steven Swanson (52) amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Barnstable, California, akituhumiwa kufanya tishio la kumuua mwanamitindo maarufu wa Australia, Miranda Kerr.

Mtuhumiwa huyo ambaye ni mkazi wa Sandwich, Massachusetts, alikamatwa baada ya polisi kupata taarifa kutoka Jimbo la Los Angeles Idara ya ‘Sheriff’ kwamba Swanson angekwenda kumuua Kerr nyumbani kwake mwezi ujao.

 

Inaelezwa kuwa mtuhumiwa huyo alisema alikuwa wakala wa shirikisho na kwamba angeweza kusafiri kwenda Los Angeles akiwa na bunduki mbili.

 

Polisi walipowasili na kufanya upekuzi nyumbani kwa Swanson, walikuta picha za Kerr kwenye jokofu, kabati na shubaka la vitabu. Hata hivyo, polisi hawakuweza kupata bunduki mbili aina Caliber 45, ambazo iliripotiwa kuwa ndizo Swanson angezitumia kumpiga risasi msanii huyo.

 

Polisi walichopata ni bunduki aina ya Pellet yenye mwonekano wa “bastola halisi” na wakaondoka nayo pamoja na mtuhumiwa huyo.

Katika kesi hiyo iliyotajwa kwenye Mahakama ya Wilaya ya Barnstable Juni 19, mwaka huu, Swanson alikana kufanya tishio la kumuua Kerr kwa risasi.

 

Daktari ambaye hakutajwa jina mahakamani hapo, alitoa ushahidi kuwa Swanson alikuwa anasumbuliwa na maradhi yanayofahamika kama Bipolar disorder na Schizophrenia, na kwamba aliacha kutumia dawa Machi, mwaka huu.

 

Kwa mujibu wa Gazeti la Cape Cod Times, Swanson kwa sasa anafanyiwa tathmini ya magonjwa ya akili (psychiatric) na amedhaminiwa kwa dola 8,000. Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa tena Julai 19, mwaka huu.