Mesut Ozil ajiengua timu ya taifa ya Ujerumani

Kiungo mshambuliaji wa Arsenal Mesut Ozil amesema hataki tena kuiwakilisha Ujerumani katika michuano ya kimataifa.

Katika taarifa ndefu iliyotolewa na Ozil mwenye miaka 29, imesema kufanyiwa vitendo visivyo vya kiungwana na chama cha soka cha Ujerumani DFB, kumemfanya asitake tena kuivaa jezi yao.

Ameongeza kuwa amekuwa akilaumiwa sana kwa Ujerumani kufanya vibaya katika michuano ya kombe la dunia.

Mwezi May, Ozil alilalamikiwa vikali na mashabiki pamoja na chama cha soka cha Ujerumani kwa kupiga picha na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan alipokua mjini London.

Ozil alihudhuria katika hafla hiyo akiwa na kiungo mwenzake anayechezea Manchester City Ilkay Gundogan.

Ozil na Gundogan wote wana asili na uraia wa Uturuki.

Ozil amesema yeye na Gundogan walizungumzia masuala ya soka walipokutana na Rais Erdogan.

Picha hizo zilitolewa na chama tawala nchini Uturuki AK kuelekea kampeni za Urais ambazo Erdogan alishinda.

Wanasiasa wengi nchini Ujerumani walihoji kitendo hicho wakati ambao taifa hilo lenye nguvu zaidi ya kiuchumi barani Ulaya likiilaumu Uturuki kwa kukiuka haki za binaadam na kutofuata misingi ya demokrasia.

Ozil amesema ”lisingekua jambo la busara kushindwa kupiga picha na Rais wa nchi ya asili yangu, hata babu zangu wa kale na kale wasingependezwa”.

Ameongeza kuwa yeye na familia yake wamekua wakipokea simu za vitisho, barua pepe za matusi na hata jumbe za kukatisha tamaa katika mitandao ya kijamii.

Akiwa na kikosi cha Ujerumani amecheza mara 92, akifunga magoli 23 na kuchangia mengine 33, huku akishinda kombe la dunia mwaka 2014.