Mgogoro wa Israel na Palestina -1

Mzozo kati ya Israel na Palestina ni wa muda mrefu. Ni mzozo ambao umesababisha Wapalestina kuwa walemavu na wengi kupoteza  maisha. Ni mzozo ambao vilevile raia wa Israel na wanajeshi wamepoteza maisha. 

Ni mgogoro ambao mataifa ya Magharibi yameshindwa kusuluhisha huku nchi za Mashariki ya Kati zikiwa kimya, isipokuwa Misri ambayo hivi karibuni ilijaribu kuutatua bila mafanikio.

Mbali na Msiri, Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Marekani, John Kerry, na viongozi wengine wamejaribu kusuluhisha mzozo huo bila jawabu. Kutokana na hali hiyo, dunia iko kimya huku mauaji ya raia wasio na hatia  yakiendelea Palestina.

Mapema Julia 8, mwaka huu, Israel  ilianza kuishambulia Palestina baada ya Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kuitangazia dunia kuwa  Hamas inapaswa kulaumiwa kwa kuhusika katika mauaji ya vijana wake watatu.

Dhamira ya makala hii ndefu ni kufanya upembuzi yakinifu juu ya msingi wa mgogoro huu ambao umekuwa ukirindima miaka nenda rudi. Hata hivyo, nitoe angalizo kabla ya kuzama katika mjadala huu mpana na   kwamba nitajikita  katika uhalisia wa mambo na misingi ya kisheria kuliko mitazamo ya kisiasa.

Henry Cattan, ni mwanasheria  wa kimataifa anayeheshimika ambaye ametoa mchango stahiki katika  kuuchambua  mgogoro  wa Israel na Palestina, kwa lengo la kujua chanzo na misingi ya kisheria inayojenga ama kubomoa  mustakabali wa tabaka hizi mbili hasimu.

Ni mwanasheria mwenye shahada ya uzamili katika sheria (LLM) – London Midle Temple Barister at Law na mwanachama wa zamani wa Chama cha Wanasheria cha Palestina na Mkufunzi katika Shule ya Sheria ya Jerusalem.

Kabla ya kuchunguza madai ya kizayoni dhidi ya hatimiliki ya Palestina, ni muhimu kuzingatia kwa ufupi  ni kwa vipi mahusiano ya Wayahudi na Wapalestina yamekuwa na, kuweka taswira ya ukweli  ya historia ya nchi.

Wayahudi hawakuwa wakazi wa awali wa Palestina. Ushahidi wa kuaminika unaonesha kuwapo kwa ustaarabu Palestina ukienda nyuma zaidi angalau miaka 1,000 Jeriko mji wa kale uliokuwa umenakshiwa umekuwa ukithaminiwa kisayansi 7,000 BC. 

Wakazi wa awali wa Palestina walikuwa Wa Kanaani.  Waliishi katika miji kama jamii na walikuwa na ustaarabu uliotukuka. Wanaaminika kuwa walikuwa wameishi  katika nchi kuanzia mwaka 3000 BC , hii ni  kusema miaka  1,800 kabla ya uvamizi wa Waisraeli. Wakanaani waliipa jina la awali nchi – Biblia inarejea jina lile kama ‘Nchi ya Kanaani’ nchi ya Wa Kanaani (Kutoka 3:17)  “Kwa hiyo, nimekusudia kuwapandisha tokea  mateso ya Misri, niwapeleke katika nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, Wayebusi katika nchi inayotiririka maziwa na asali.

“Watayasikia maneno yako, nawe utakwenda pamoja na wazee wa Israel kwa mfalme wa Misri na kumwambia hivi: BWANA MUNGU wa Waebrania amekutana nasi. Basi tupe ruhusa  twende mwendo siku tatu jangwani, tupate kumtolea huko sadaka BWANA MUNGU wetu”.

(Hesabu 34:1) Kisha BWANA akanena na Musa, na  kumwambia waagize wana wa  Israel, uwaambie mtakapoingia nchi ya  Kanaani (hii ndiyo nchi  itakayowaangukia kuwa urithi, maana, hiyo nchi ya Kanaani kama mipaka yake ilivyo), ndipo upande wenu wa Kusini utakuwa tangu Bara ya Sini kupita kando ya Edomu, na mpaka wenu wa Kusini utakuwa tangu mwisho wa  Bahari ya Chumvi kuelekea Mashariki.

Kisha mpaka wenu utageuka kwenda upande  wa Kusini wa kukwelea kwake Akrabimu, kisha kupitia kwenda Sini, na kutokea kwake kutakuwa kuelekea upande wa Kusini wa Kadesh- Branea, kisha utaendelea mpaka Hasar- Adari – na kufikia Azmoni.

(Hesabu 35:1) Kisha BWANA  akanena na Musa katika nchi tambarare za Moabu, karibu na mto Yordani, hapo Yeriko, akamwambia uwaagize wana wa Israel wawape Walawi miji wapate mahali pa kukaa, katika milki yao, pamoja na malisho yaliyoizunguka hiyo miji kote kote mtawapa Walawi… Hiyo miji watakuwa nayo kwa wanyama wao na mifugo na kwa mali zao, na kwa wanyama wao wote, walikuwa ni wa Kanaani waliovumbua Jerusalemu.

Je, unafahamu kuwa Wafilisti (Wapalestina) walipigana vita miaka 200 na Waisraeli walitawaliwa kwa karne 24 kabla ya kurejea Jerusalem kwa nguvu? Usikose toleo lijalo katika makala hii itakayofafanua mgogoro wa Israel na Palestina ulivyoanza na nini suluhisho. Mhariri.

 

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa Anapatikana kwa:-

 (+255)784  142  137

(+255) 713 333141

Au  barua  pepe

[email protected]

[email protected]