RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameanika madudu mengine ya Wizara ya Madini akisema kuwa baadhi ya wateule wake katika wizara hiyo wamekuwa wazembe katika kutekeleza maagizo na kutimiza majukumu yao kama watendaji wa serikali.

Magufuli ameyasema hayo leo Jumatatu wakati akimwapisha Mhe. Dotto Mashaka Biteko kuwa Naibu Waziri wa Madini Ikulu jijini Dar es Salaam. Rais ametolea mfano wa sheria mpya ya madini iliyopitishwa bungeni mwezi Julai mwaka jana, ambapo amesema mpaka sasa wizara hiyo haijapitisha kanuni (regulations) ili sheria hiyo iweze kufanya kazi jambo ambalo amesema ni uzembe usiovumilika huku akimwagiza Waziri wa Sheria, Prof. Palamagamba Kabudi kukamilisha kanuni hizo na kuzisaini kufikia Ijumaa ya wiki hii.

“Nakushukuru Mhe spika kwa kutoa ushauri kwa serikali na sisi tumekuwa tukiufuata sana. Wizara ya madini ina changamoto sana na hata sasa ina changamoto na haifanyi kazi vizuri. Spika utakumbuka mwezi wa saba mlifanya marekebisho ya sheria ya madini. Na ilipokuja kwa kwangu siku hiyo hiyo nilisaini na kuipitisha, lakini tangu Julai mpaka sasa regulations (kanuni) hazijasainiwa lakini sheria imepitishwa na bunge, hivyo sisi Watanzania watumishi hatupo serious.

“Nasikitika kusema baadhi ya ninaowateua hawajajua nataka nini. Ndiyo maana nikamteua aliyekuwa kwenye kamati ya madini, labda atatoa changamoto kwa wenzake maana huenda yeye anaelewa zaidi. Na mnada wa Tanzanite hautafanyika tena mpaka regulations zitakaposainiwa. Sasa mpo manaibu wawili na waziri wa sheria yupo hapa nataka regulations hizi zisainiwe kabla ya Ijumaa, tumeibiwa mno, sasa nimesema imetosha,” alisema Rais Magufuli kwa uchungu.

TAZAMA VIDEO MAGUFULI AKIZUNGUMZA