RC Wangabo Atoa Mwezi Mmoja Kuwa na Mkakati wa Kuzuia Uvuvi Haramu Kuokoa Viwanda vya samaki Mwambao wa Ziwa Tanganyika

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akisalimiana na Mkurugenzi wa Mikebuka Fisheries Tanzania Ltd Azim Premji muda mfupi baada ya kuwasili katika kiwanda hicho.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa tatu kutoka kulia) akipewa maelezo na Mkurugenzi wa Mikebuka Fisheries Tanzania Ltd Azim Premji (wa pili kutoka kulia) katika kiwanda cha Mikebuka Fesheries Tanzania Ltd.
Kiwanda cha Akwa Fisheries Tanzania Ltd. kilichosimamisha uzalishaji.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (Katikati) akitoa maelekezo kwa Meneja wa Tanesco Mkoa wa Rukwa Mhandisi Herini Mhina (Kulia) na (Kushoto) Mkuu wa Wilaya ya Kalambo Mh. Juleth Binyura.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa tatu kushoto) akipokea maelezo kutoka kwa Mhandisi Mshauri Martin Hossey (wa pili kushoto) kuotoka Kampuni ya Nicholas O’Dwyer inayosimamia ujenzi wa Barabara ya Sumbawanga – Matai – Kasanga yenye urefu wa Km 112 ya thamani ya Bilioni 133 iliyomalizika kwa kiwango cha Km 71.5.

 

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Kalambo pamoja na kamati yake ya Ulinzi na Usalama kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Kalambo kukaa pamoja na kuandaa mkakati wa kuzui uvuvi haramu unaoendelea katika mwambao wa ziwa Tanganyika ili kuokoa viwanda vilivyopo katika mwambao huo.

Amesema kuwa uvuvi haramu unaoendelea katika mwambao huo unahatarisha maendeleo ya viwanda vya samaki vilivyopo na hatimae kudhoofisha ajira za wananchi waliopo karibu na viwanda hivyo na hatimae kurudisha nyuma juhudi za serikali ya awamu ya tano katika kuibua na kuimarisha viwanda vilivyopo.

“Mwisho wa mwezi huu nataka taarifa ya namna mlivyojipanga kupiga marufuku uvuvi haramu ikiwa ni pamoja na kutoa elimu na kuwakamata wale wanaokaidi na kuendesha uvuvi haramu, uvuvi haramu ukiendelea hiki kiwanda hakitakuwepo, kwasababu ya kuua samaki na watoto wake, achene uvuvi haramu, mnamaliza samaki katika ziwaletu hili,” RC Wangabo Alisisitiza

Ameongeza kuwa samaki ndio rasilimali pekee inayowaajiri pamoja na kuendesha kiwanda na kuwataka wananchi kuungana pamoja kuhakikisha wanatunza rasilimali hiyo, na kupiga marufuku aina zote za uvuvi haramu na kuonya kutosikia kiwanda kimefungwa kutokana na kukosa samaki amabao wamekwisha kwasababu ya uvuvi haramu.

Ameyasema hayo alipotembelea viwanda viwili vya samaki vya Mikebuka Fisheris Tanzania Limited pamoja na Akwa Fisheries Tanzania Limited vilivyopo katika kata ya Kasanga ambapo kiwanda pekee kinachojikongoja ni Mikebuka fisheries huku AkwaFisheries kikiwa kimesimamisha uzalishaji.

Awali alipokuwa akisoma taarifa ya Kiwanda cha Mikebuka Fisheries Tanzania Limited Mtendaji wa Kijiji cha Muzi Gasper Kateka amesema kuwa mbali na ukosefu wa samaki ametaja kuwa changamoto nyingine ni Umeme na barabara jambo linalowafanya kutumia gharama kubwa kendesha kiwanda hicho kwa majenereta na kupakia samaki kwenye boti hadi bandari ya kasanga ili kuweza kuwasafirisha kwenda Sumbawanga kukwepa kipande cha barabara cha Km 1.2 kilichojaa mawe.

“Mikebuka Fisheries in maeneo mawili ya kuchakata samaki ikiwa Sumbawanga yenye uwezo wa kilo 8000 kwa siku na kasanga yenye uwezo wa kilo 15000 kwa siku lakini kutokana na uhaba wa samaki uwezo umeshuka na kuchakata kilo 3000 hadi 4000 kwa siku na kuajiri watu 30 na vibarua 55,” Kateka alieleza.

Kwa upande wake Afisa uvuvi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo Godfrey Makoki alitoa ufafanuzi wa makubaliano ya matumizi ya ziwa Tanganyika yaliyofanya na nchi nne (Zambia, Burundi, Tanzania na DR Congo) katika kikao kilichofanyika 18/10/2012 Mjini Bujumbura katika kanuni ya nne ya makubaliano hayo imekataza uvuvi wa dagaa mchana katika ziwa Tanganyika.

“jambo linalotupa shida ni uvuvi wa kuvua dagaa mchana, kitaalamu dagaa huwa wanakuja kutaga mchana hivyo wanakuwa wakubwa kwasababu wana mayai na usiku huwaoni, sasa huwa tunawaambia kuwa huo ni uvuvi haramu hapo inakuwa ni tatizo,” Makoki Alibainisha.

Katika Kutatua tatizo la Umeme na Barabara Mh. Wangabo amemuagiza Meneja wa Tanesco Mkoa wa Rukwa kuhakikisha umeme wa REA awamu ya tatu unawafika haraka katika Kijiji hicho kwani kipo kwenye mkakati na kuwaagiza TARURA na TANROAD kushirikiana na Mkurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha ndani ya miezi mitatu wanairekebisha barabara ya Km 1.2 ili iweze kupitika.

Mwambao wa Ziwa Tanganyika kwa Mkoa wa Rukwa una Viwanda Vinne vya Samaki, Viwili vipo Kata ya Kipili, Wilaya ya Nkasi na Viwili vipo Kata ya Kasanga, Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa.