Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo na Msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abass.

Serikali imewatoa hofu Watanzania kuhusu tatizo la umeme na utekelezaji wa mradi wa treni ya umeme nchini ambao ujenzi wake unaendelea.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo na Msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abass amesema jitihada zinaendelea kufanyika kuhakikisha umeme wa kutosha unazalishwa nchini.
Akizungumza na wanahabari leo Jumatatu jijini Dar es Salaam kuhusiana na utekelezaji wa ahadi za Serikali, Dk Abass amesema kazi ya kusanifu njia yote itakayopita reli hiyo ya umeme imeshakamilika.
“Suala la umeme sio tatizo Serikali inaendelea kutekeleza miradi zaidi ya  20 kuhakikisha nchi ina umeme wa uhakika,”
Dk Abass amesema Serikali kupitia kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (Rahco) inatarajia kununua vichwa 23 vya treni ya umeme na viwili vya treni ya dizeli kwa ajili ya kuboresha usafiri wa reli.
Sambamba na hilo inatarajia pia kununua mitambo 25 ya ukarabati wa reli na mabehewa 1,590 kati ya hayo 1,530 yakiwa ya mizigo na 60 ni ya abiria.
Dk Abass amesema zabuni za manunuzi hayo zinatarajiwa kufunguliwa ndani ya mwezi huu.
Amesema kati ya mabehewa 60 ya abiria 15 ni daraja la kwanza na 45 daraja la kawaida.
Kuhusu usafiri wa majini Dk Abass amesema tayari Serikali imenunua meli mpya mbili za mizigo katika ziwa Nyasa.
Meli hizo Mv Njombe na  Mv Ruvuma na zina uwezo wa kubeba tani 1,000 kila moja na zimeanza kufanya kazi wiki iliyopita.

By Jamhuri