Mkurugenzi wa Miradi wa TASAF, Amadeus Kamagenge(aliyesisima) akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Wadau wa Maendeleo na Serikali ulioanza leo mjini Dar es salaam . 

Kiongozi wa Shughuli za TASAF katika Benki ya Dunia Mohamed Muderis (aliyesimama) akitoa maelezo kwenye Mkutano wa Wadau wa Maendeleo,Serikali na TASAF unaojadili maendeleo ya Mpango wa Kunusuru  Kaya Maskini.


Baadhi ya Wadau wa Maendeleo,Maafisa wa TASAFna Serikali wakiwa kwenye Mkutano wa kujadili Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini.
Baadhi ya Wadau wa Maendeleo,Maafisa wa TASAFna Serikali wakiwa kwenye Mkutano wa kujadili Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini. 
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii -TASAF- na wadau wa Maendeleo wameanza mkutano jijini Dar es salaam kupitia pamoja na mambo mengine utekelezaji wa Shughuli za Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ——PSSN- unaotekelezwa na serikali kupitia TASAF.
Pamoja na Mkutano huo ulioanza leo kwenye ukumbi wa Mikutano wa TASAF jijini Dar es salaam , wadau hao wa Maendeleo,maafisa wa serikali na wenyeji TASAF watatembelea mkoa wa Kagera,Shinyanga,Manyara,Unguja,Pemba na Tanga ambako watakutana na viongozi wa serikali na walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya maskini kujionea namna Mpango huo unavyoendelea kuchangia uboreshwaji wa Kaya za Walengwa.
Utaratibu wa serikali kupitia TASAF kukutana na Wadau wa Maendeleo hufanyika kila baada ya miezi sita kwa lengo la kutathimini utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ulioanza kutekelezwa mwaka 2012 Tanzania Bara, Unguja na Pemba.
Hadi sasa takribani Kaya za Wanufaika Milioni Moja na Laki Moja zimeandikishwa kwenye Mpango ambapo licha ya kupata ruzuku inayotolewa kila mwezi kwa kipindi cha miezi miwili, walengwa hao wamekuwa wakishiriki kwenye shughuli za kujiongezea kipato kupitia utaratibu wa Ajira ya Muda, Mpango wa kuweka akiba na kukopeshana kupitia vikundi kama njia mojawapo ya kujiimarisha kiuchumi.
Aidha Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ambao unatekelezwa kupitia Kaya Maskini ambazo zilibainishwa na wananchi wenyewe kwenye maeneo yao kwa sasa unatekelezwa katika asilimia 70 ya vijiji nchini kote wakati jitihada za kutafuta fedha ili kukamilisha asilimia 30 ya vijiji viliyosalia zinaendelea.
Taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini iliyowasilishwa kwenye mkutano huo zinaonyesha kuwapo kwa mafanikio makubwa kwa walengwa ambao wengi wao wameanza kujiwekea rasilimali ambapo mifano ya uboresha makazi,kupata uwezo wa kuhudumia kaya zao,elimu na afya zimebainishwa kupatikana kwa kaya za walengwa .
Zifuatazo ni picha za wadau wa Maendeleo na maafisa wa serikali na TASAF wakiwa kwenye Mkutano wao ulioanza leo jijini Dar es salaam.

By Jamhuri