TPA: Maonesho ya kilimo Nanenane ni muhimu kwa taasisi

Na Mwandishi Wetu,Jamhurimedia,Mbeya

Maonesho ya Kilimo ya Nanenane 2022 yanayofanyika kitaifa kwenye viwanja vya John Mwakangale Jijini Mbeyayametoa fursa kwa Taasisi mbalimbali kukutana na wananchi hususani wakazi wa Mkoa wa Mbeya na mikoa ya jirani ya iliyopo Nyanda za Juu Kusini kupata elimu na uelewa wa shughuli mbalimbali zinazofanywa na taasisi hizo.

Moja ya Taasisi zilizoshiriki Maonesho hayo ni Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ambapo wamepata fursa ya kukutana na wananchi wengi waliokuwa wakifurika kwenye Banda la Taasisi hiyo kupata kuuliza maswali mbalimbali yaliyolenga kupata ufahamu zaidi juu ya kazi za bandari

Nicodemas Mushi ni Kaimu Mkurugezi wa Idara ya Masoko na Uhusiano Mamlaka ya Bandari Tanzania TPA anasema kushiriki katika maonesho hayo kunatoa wakati mwingine wa kukutana na watanzania, wadau na wateja wa bandari kutoka nyanda za juu Kusini, vilevile kutoka nchi jirani ambao wanafika katika mkoa wa Mbeya wakiwa katika shughuli zao za kibiashara.

Mushi ameyasema hayo alipokuwa katika maohojiano maalum na waandishi wa habari Agosti 7,2022 katika Banda lao ambapo amefafnua kuwa Mamlaka hiyo ina jukumu kubwa la kusimamia bandari zote hapa nchini.

“Maonesho kama haya ni eneo la wazi ambapo tunawalteta watu pamoja pasipo na taratibu ngumu za kuonana, tunazungumza nao kwa njia rafiki, tunawaelimisha na kupokea maoni na ushauri wao ,na kujibu maswali yao mbalimbali magumu na mepesi ikiwemo kutengeneza miradi ya biashara” amesema Mushi

“TPA ndio Mamlaka pekee hapa nchini yenye jukumu la kusimamia bandari zote zilizoko katika mwambao wa bahari ya hindi kama vile Bandari kuu ya Dar es salaam, Bandari ya Mtwara na Bandari ya Tanga. Pia Bandari zote za maziwa kama vile Ziwa Tanganyika, Victoria na Ziwa Nyasa hizi zote zinasimamiwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania TPA” amefafanua.

Aidha amezungumzia upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na kusema kuwa mambo yanakwenda vizuri kupitia mradi wa DMDP ambapo awamu ya kwanza imekamilika na kwamba sasa Bandari hiyo iko kwenye viwango bora vinavyotambulika kimataifa kuanzia gati namba 0 la kupokelea magari mpaka gati namba 7 na kwamba biashara inakwenda vizuri.

“Kwa upande wa wateja wetu ambao ni TICS wanaofanya kazi ya kuhudumia makontena nako kazi inaenda vizuri sana upanuzi wa bandari umekamilika kwa kiwango kikubwa na utoaji wa huduma za bandari unaenda vizuri,” ameongeza Mushi.

Amesema kuwa pia maboresho makubwa yamefanyika kwa upande wa vitendea kazi ambapo kwa sasa zipo mashine na mitambo mbalimbali ya kisasa ya kuhudumia meli na kwamba kwa ujumla na kwamba Bandari hiyo imekidhi viwango na huduma imeimarika

Katika hatua nyingie Mushi amezungumziasuala zima la ulinzi na usalama wa Bandari ikiwemo mizigo na vitendea kazi ni wa hali ya juu hali ambayo sasa inaifanya Bandari ya Dar es Salaam kuvuka vile viwango vya awali na kuwa viwango vya juu kabisa na kupelekea makampuni makubwa kuchagua kuitumia Bandari hiyo ukilinganisha na zamani ambapo kulikuwa na kugombea wateja na Bandari za jirani.

Amebainisha kuwa Tanzania imebahatika kwa kuwa na jografia nzuri inayopelekea nchi zote za jirani ambazo hazina miundombinu ya Bandari kutegemea Bandari ya Dar es Salaam kwa kufikisha mzigo katika nchi zao.

Amezitaja nchi zinazotumia bandari ya Dar es Salaam kusafirisha na kupokea mzigo yao kuwa ni Zambia, Malawi, Congo DRC, Burundi, Rwanda, Zimbabwe na baadhi ya visiwa kama Comoro Re- Union, Mauritius na maeneo kulingana na unafuu wa gharama za kusafirisha mizigo.