Trump Atishia Kujiondoa Kwenye Mazngumzo na Kim Jong-un

Rais Donald Trump aonya kujiondoa katika mazungumzo na Kim Jong Un

Rais wa Marekani Donald Trump anasema kuwa iwapo mazungumzo yake na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong un hayazai matunda ‘atainuka na kuondoka katika mazungumzo hayo’.

Katika mkutano wa pamoja na vyombo vya habari, yeye na waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe walisema kuwa shinikizo dhidi ya Korea Kaskazini ni sharti iendelee kwa kukataa kusitisha utengezaji wa silaha za nyuklia.

Bwana Abe yuko katika mgahawa wa rais Trump wa Mar-a-Lago resort mjini Florida kwa ,mazungumzo.

Mapema , bwana Trump alithibitisha kwamba mkurugenzi wa CIA Mike Pompeo alifanya ziara ya kisiri hadi Korea Kaskazini ili kukutana na Kim Jong Un.

Alisema kuwa bwana Pompeo aliweka uhusiano mzuri na bwana Kim ambaye bwana Trump alimuita ‘mtu mdogo’ na kwamba mkutano wao ulifanyika vizuri.

Ziara hiyo iliadhimisha mawasiliano ya juu kati ya Marekani na Korea Kaskazini tangu 2000.

Mkutano huo kati ya Trump na bwana Kim unatarajiwa kufanyika kufikia mwezi Juni. Maelezo ikiwemo eneo litakaloandaa mkutano huo bado yanaendelea kufanyiwa kazi.

Ni nini kilichosemwa kuhusu mkutano huo?

Rais Trump alisema katika mkutano wa pamoja kwamba iwapo anadhani kwamba mkutano huo hautafanikiwa basi hatoshiriki na kwamba iwapo mkutano huo umefanyika na haoni matunda yake basi atasimama na kuondoka.

”Kampeni yetu ya shinikizo itaendelea hadi pale Korea Kaskazini itakapositisha utengezaji wa silaha za Kinyuklia”, aliongezea.

“Kama nilivyosema awali nyota ya Korea Kaskazini itang’aa wakati taifa hilo litakaposimamisha mpango wake wa kinyuklia .Itakuwa siku kuu kwao na itakuwa siku kuu ulimwenguni.”

Ni Nini chengine kilichozungumziwa?

Kuhusu biashara, viongozi hao wawili walikubaliana kuanza mazungumzo kuhusubiashara huru na isiopendelea upande wowote.

Bwana Trump alisema kuwa Marekani itaendelea kupinga hatua ya kujiunga na biashara ya ushirikiano ya Trans Pacific Partnership hadi pale Japan na washirika wengine watakapoweka makubaliano ambayo Marekani haiwezi kukataa.

Marekani hatahivyo haikuiondoa Japan katika kuitoza kodi ya vyuma na alminium kama alivyowafanyia washirika wengine wa Marekani.

Akizungumzia kuhusu Korea Kaskazini Bwana Abe alisema kwamba amemtaka rais Trump kusaidia kuwachiliwa huru kwa raia wa Japan waliotekwa nyara na Korea Kaskazini miaka ya 1970 na 1980.

Korea Kaskazini imekiri kuwateka nyara raia 13 wa Japan ili kuwatumia kuwafunza wapelelezi wake kuhusu forodha ya Japan. Japan inaamini takwimu hizo ziko juu.

Swala hilo limeathiri pakubwa uhusiano kati ya mataifa hayo mawili kwa miongo kadhaa. Raia watatu wa Marekani pia wanazuiliwa nchini Korea Kaskazini.

Bwana Trump anasema kuwa Marekani itatumia kila njia ili kuhakikisha kuwa raia wa taifa hilo waliotekwa nyara na Japan wanarudishwa nyumbani.

SOURCE: BBC SWAHILI