?? d??ta?µa µe t? ?p??? t??eta? ?p? ?a?est?? e????a?s?? t? ?p??at?st?µa t?? FBME Bank Ltd st?? ??p??, e??d?se a??? ??e? t? ß??d? ? ?e?t???? ???pe?a t?? ??p???, t? ?p??? ?a? t????e se ?s??.
S?et??? a?a?????s? a?af??e? ?t? s??p?? t?? d?at??µat?? e??a? ? p???s? t?? e??as??? t?? ?p??atast?µat?? µe st??? t?? p??stas?a t?? ?ata?et??. St? f?t???af?a ta ??afe?a t?? ?p??atast?µat?? t?? FBME Bank Ltd st?? ?e???s?a, 22 ??????? 2014.
Kufungwa kwa benki ya FBME, hapa nchini, kumetokana na tuhuma za benki hiyo kutakatisha fedha na kupitisha fedha za kufadhili ugaidi ambazo zimekuwa zikipitishiwa kwenye matawi yake ya Nicosia, Cyprus na Makao Makuu ya benki hiyo, Dar es Salaam, JAMHURI limebaini.
Julai, 2014 Benki Kuu ya Cyprus, pamoja na Benki Kuu ya Tanzania, waliingilia kati na kuanza kuchunguza, uchunguzi huo ndiyo uliosababisha kufungwa kwa shughuli zote za kibiashara, huku malipo yote yakisimamiwa na mfilisi aliyeteuliwa.


Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Julai, 2014 na Mkurugenzi wa FinCEN, Jennifer Shasky Calvery, benki ya FBME imekuwa na sera dhaifu ya utakatishaji fedha, hali ambayo imekuwa kivutio kikubwa kwa wafanyabiashara wanaojihusisha na ukatatishaji.
“Benki ya FBME, imekuwa inatumiwa na wateja wake kuwezesha utakatishaji fedha, kufadhili ugaidi, uhalifu wa kimataifa, wizi. Wamekuwa wanakiuka vikwazo walivyowekewa pamoja,” inasomeka sehemu ya taarifa ya FinCEN.


Kutokana na taarifa ya FinCEN, taasisi nyingi za fedha zikaanza kusitisha ushirikiano wake na Benki ya FBME, hali iliyosababisha kutoweza kuhamisha fedha kutoka FBME kwenda benki nyingine.
“Kutokana na uamuzi huo uliofikiwa na Benki kuu za Tanzania (BoT) na Cyprus, ukwasi wa benki hiyo ulishuka kwa kasi ya kutisha, huku wenye fedha wakishindana kuondoa fedha zao ili wabaki salama. Wakati hayo yakitokea, gharama za uendeshaji wa benki hiyo zikabaki palepale,” inasomeka sehemu ya ripoti ya FinCEN.


Vyanzo vilivyozungumza na JAMHURI kwa sharti la kutotajwa gazetini, vinasema, FBME, benki iliyoanzia Mashariki ya Kati na baadaye kuhamishia makao yake makuu Dar es Salaam, haikuwa bahati mbaya.
“Haikuwa bahati mbaya kwa benki hiyo kuhamishia makao yake makuu Dar es Salaam, hapa pamekaa kimkakati, hivyo fedha za kufadhili ugaidi zilikuwa zinaweza kuwafikia walengwa kwa haraka. Benki Kuu ya Tanzania imefanya jambo jema sana,” kimesema chanzo chetu.
Wiki iliyopita, BoT ilitangaza kusimamisha   shughuli zote za FBME Bank Ltd, kufuta leseni yake ya kufanya shughuli za kibenki na kuiweka chini ya ufilisi, huku BoT ikiiteua Bodi ya Bima ya Amana kama mfilisi kuanzia tangu Mei 8, mwaka huu.
Wakati hali hiyo ikiendelea, BoT imewataka wenye amana, wadai na wadaiwa wawe wavumilivu wakati mfilisi akiandaa utaratibu wa kushughulikia stahiki zao.


Benki ya FBME imepata kigugumizi na kutoa ufafanuzi dhidi ya tuhuma zinazoikabili, ikiwa ni pamoja na kufadhili ugaidi.
JAMHURI limefika Makao Makuu ya Benki hiyo jijini Dar es Salaam,  kutaka kupata ufafanuzi wa masuala kadhaa ikiwamo hatua hiyo ya BoT kuifilisi benki hiyo.
Afisa mmoja wa benki hiyo aliyejitambulisha kuwa ni mmoja wa maafisa usalama wa benki hiyo, tawi la Arusha, huku akikataa kutaja jina lake, ameliambia JAMHURI kwa sasa wanaendelea kutekeleza maelekezo ya mfilisi.
“Kwani tangazo la Benki Kuu hujaliona? Unataka mimi nikueleze nini? Sababu za benki kufutwa zimetajwa na Benki Kuu. Kama unahitaji taarifa zaidi kawaulize Benki Kuu, sisi hatuna mamlaka ya kulizungumzia hili kwa sababu benki haipo tena.
“Hapa ninavyozungumza na wewe nimetoka Arusha kwa ajili ya jambo hili. Humu ndani kuna maofisa wa Benki Kuu na wa FBME wakilijadili suala hili kwa kina. Wanaanza asubuhi hadi jioni bila kupumzika labda wakati wa kula. Hatuna majibu zaidi ya hayo, kawaulize BoT,” amesema afisa huyo.
Afisa huyo ameshindwa kukamusha wala kukubali iwapo benki hiyo ilikuwa ni mfadhili mkuu wa shughuli za ugaidi Afrika Mashariki na kwingineko.


Benki hiyo ni zao la Federal Bank of Lebanon, iliyoasisiwa mwaka 1953, kabla ya kuwa FBME, mwaka 1982 na kuanzia biashara yake huko Cyprus. Benki hiyo imekuwa ikitoa huduma katika nchi za Cyprus, Tanzania na Urusi.
Nchini Cyprus iliwahi kuwa na matawi mawili ambayo ni Nicosia na Limassol, nchini Tanzania ilikuwa na matawi manne ya Dar es Salaam (Makao Makuu Duniani), Mwanza, Zanzibar na Arusha, ambapo nchini Urusi kulikuwa na ofisi moja mjini Moscow ya kuiwakilisha benki hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopo katika tovuti ya benki hiyo, hadi kufikia robo ya tatu ya mwaka 2013 ilikuwa na mtaji wa dola za Marekani bilioni 2.716 sawa na Sh trilioni 4.4.
Mwaka 1982, Benki ya FBME ilianza shughuli za huduma za kibenki Nicosia, Cyprus kama kampuni tanzu ya Benki ya Shirikisho ya Lebanon SAL.


Mwaka 1986, Benki hiyo ilivifanya visiwa vya Cayman kuwa makao makuu yake ambapo benki ya Cyprus ilibadilishwa na kuwa tawi la benki hiyo.  Mwaka 1993, benki hiyo ilifungua tawi jijini Moscow, Urusi.   
Mwaka 2003 kama sehemu ya mipango yake ya kimkakati, benki hiyo ilijiondoa katika visiwa vya Cayman na kuanzisha makao makuu yake, Dar es Salaam, Tanzania. Wakati huohuo benki iliyokuwapo Cyprus ikafanywa kuwa tawi la FBME Tanzania.
Mkurugenzi wa Bodi ya Bima ya Amana, Emmanuel Boaz, ameliambia JAMHURI kwamba bodi yake inaendelea na kufanya uhakiki wa mali zinazomilikiwa na benki hiyo.
“Kwa sasa tupo katika hatua ya makabidhiano ambayo inahusisha FBME kutupa waraka maalumu wa makabidhiano ya mali zake zote, sisi tuko na wataalamu wetu ambao wameambatana na wale wa FBME katika kupata ripoti sahihi ya mali za benki hii,” amesema Boaz.
Julai 2014, Benki Kuu ya Tanzania iliiweka chini ya usimamizi maalumu (statutory management) benki ya FBME.


Hatua hii ya Benki Kuu ilitokana na notisi iliyotolewa Julai, 2014 na taasisi ya Marekani inayopambana na uhalifu wa Kifedha “the US Financial Crimes Enforcement Network” kwa kifupi FinCEN.
FinCEN iliituhumu FBME kuwa ni taasisi inayojihusisha na biashara ya utakatishaji wa fedha, jambo lililosababisha Benki Kuu ya Cyprus kuliweka tawi la FBME lililopo Limassol chini ya uangalizi maalumu.
Katika notisi hiyo, FinCEN ilitoa kusudio la kuifungia FBME kutotumia mfumo wa kibenki wa Marekani (US financial system).


Julai, 2015, FinCEN ilitoa uamuzi wa kuifungia FBME kutumia mfumo wa kibenki wa Marekani. Kitendo hicho kikasababisha FBME kufungua kesi katika mahakama ya ‘US District Court for the District of Columbia’ ikiiomba mahakama hiyo kutengua uamuzi wa FinCEN.
Aprili, mwaka huu, mahakama hiyo ilitoa uamuzi ambao unairuhusu FinCEN kuendelea na utekelezaji wa uamuzi wake wa mwisho wa kuifungia benki ya FBME kutumia mfumo wa kibenki wa Marekani.
Uamuzi wa mahakama hiyo umeongeza athari kwa kiwango kikubwa katika uendeshaji wa benki ya FBME kwa kuwa isingeweza tena kufanya miamala ya kibenki ya kimataifa na kupata huduma za mifumo ya kibenki na hivyo ingeshindwa kutoa huduma muhimu kwa wateja wake kwa mujibu wa leseni waliyopewa.
Kwa kuzingatia athari zinazotokana na uamuzi wa mwisho wa FinCEN, kwa mamlaka iliyopewa chini ya kifungu cha 58(2)a, 11(3)(i), 61(1) na 41(a) vya Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 (the Banking and Financial Institutions Act, 2006), Benki Kuu ya Tanzania ilifikia uamuzi wa kusimamisha shughuli zote za FBME.


Tayari Benki Kuu imewaandikia taarifa maalumu waliokuwa wateja wa benki hiyo, ambao ni wale wenye amana, wadai na wadaiwa kuwa wawe wavumilivu wakati mfilisi akiandaa utaratibu wa kushughulikia stahiki zao.

By Jamhuri