Mamlaka nchini Ugiriki imeeleza kuwa, imekamata meli iliyokuwa na bendera ya Tanzania iliyokuwa safarini kuelekea ncuni libwa ikiwa imebeba vifaa vinavyotumika kutengenezea vilipuzi.
Meli hiyo iligundulika wakati ikiwa jirani na Kisiwa cha Crete siku ya Jumamosi. Mamlaka hiyo imekuta makontena 29 yakiwa na vifaa mbalimbali kama ammonium nitrate, non-electric detonators na matenki 11 matupu ya petroli.
Afisa mmoja wa mamlaka hiyo amesema kwamba, vifaa hivyo vilikuwa vinapelekwa nchini Libya na vingeweza kutumika kwa kazi za aina mbalimbali ikiwemo kutengenezea mabomu kwa ajili ya uhalifu.
Muungano wa Ulaya na Umoja wa Mataifa wamezuia uuzwaji Libya kuuziwa silaha tangu mwaka 2011.
Kutokana na nyaraka zilizokuwa katika boti hiyo, mzigo huo ulipakiwa katika Bandari ya Uturuki ya Mersin na Iskenderum na ilitarajiwa pia kufika Djibouti na Oman.
Walinzi wa pwani ya Ugiriki wamesema kuwa, uchunguzi wa awali unaonyesha kwamba, nahodha wa meli hiyo ameamriwa na mmiliki wa meli kwenda Libya katika mji wa Mistrata kwa ajili ya kupakua mzigo huo. Katika ukaguzi uliofanyika, walinzi hao hawakupata ramani yoyote ambayo inaonyesha safari yao ya Djibout na Oman.
Watu wanane waliokuwa katika meli hiyo walikamatwa na walitarajiwa kufikishwa mahakamani leo.

By Jamhuri