WAGONJWA 64,093 WATIBIWA KATIKA TAASISI YA MOYO JAKAYA KIKWETE KWA MWAKA 2017

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa mwaka wa 2017 imeona jumla ya wagonjwa 64,093 kati ya hawa wagonjwa wa nje ni 60,796 na waliolazwa 3297. Wagonjwa waliolazwa 3010 waliruhusiwa baada ya hali zao kuwa nzuri na wagonjwa 287 walipoteza maisha hii ikiwa ni sawa na asilimia 8.7.
Wagonjwa 225 walifanyiwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua ambapo wagonjwa 200 waliruhusiwa na wagonjwa 25 walifariki Dunia hii ikiwa ni sawa na asilimia 11 (wastani wa kimataifa ni asilimia 13). Kati ya wagonjwa 225 waliofanyiwa upasuaji wa kufungua kifua wagonjwa 105 walifanyiwa upasuaji na madaktari wetu bingwa wa magonjwa ya moyo watoto wakiwa ni 60 na watu wazima 45.
Upasuaji wa moyo wa bila kufungua kifua (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab ulifanyika kwa wagonjwa 800 kati ya hao 798 wanaendelea vizuri na wagonjwa wawili (2)walifariki hii ikiwa ni chini ya asilimia 1.6. Kati ya wagonjwa 800 waliotibiwa wagonjwa watu wazima 631 walifanyiwa upasuaji na madaktari wetu wa ndani.
Tulikuwa na jumla ya kambi za matibabu 15. Tumefanya matibabu ya pamoja na washirika wetu kutoka mabara ya Asia, Australia, Ulaya na Amerika. Katika kambi zote hizo kambi za watoto ni tano na kambi za watu wazima 10. Jumla ya wagonjwa 120 walifanyiwa upasuaji wa kufungua kifua kati ya hao watoto 80 na watu wazima ni 40. Wagonjwa 169 walifanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua kati ya hao watoto 92 na watu wazima 77.
Kwa wagonjwa wote hao 1025 kufanyiwa upasuaji wa kufungua kifua na bila kufungua kifua hapa nchini Taasisi imeweza kuokoa zaidi ya bilioni 29 (Tshs. 29,725,000,000/=) ambazo Serikali ingezilipa kama wagonjwa hawa wangefanyiwa upasuaji wa moyo nje ya nchi. Gharama za mgonjwa mmoja anayetibiwa nje ya nchi ugonjwa wa moyo ni zaidi ya milioni 29.
Tulifanya upasuaji wa kuunganisha mishipa ya damu (AVF- Arterio Venous Fistula) kwa ajili ya kusafishia damu kwa wagonjwa wenye matatizo ya figo (Hemodialysis) 52.
Wakati huo huo Taasisi ilishiriki katika utoaji wa huduma ya upimaji afya bila malipo na kutoa elimu ya afya bora ya moyo kwa wananchi katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Lindi na Katavi. Katika mikoa hiyo tuliweza kuwaona na kuwapatia huduma wananchi 8000.
Malengo tuliyokuwa nayo kwa mwaka huu wa 2018 ni kuona wagonjwa wengi zaidi ya hawa tuliowaona mwaka 2017 katika kliniki zetu za kila siku na kufanya upasuaji. Taasisi imejipanga kufanya upasuaji wa kufungua kifua kwa wagonjwa 400 na bila kufungua kifua kwa wagonjwa 1000.Tunatarajia kuwa na kambi maalum za upasuaji wa moyo zisizozidi 15.
Aidha tunawaahidi wananchi kwa mwaka 2018 tutaendelea kutoa huduma katika kiwango cha kimataifa, kuendelea kupunguza kupeleka wagonjwa nje ya nchi, kupunguza gharama za tiba katika Taasisi yetu, kuongeza idadi ya huduma, kuboresha usafi zaidi katika Hospitali yetu na kuzidi kushirikiana na Serikali na wananchi.
Changamoto kubwa tunayokabiliana nayo katika kazi zetu za kila siku ni ufinyu wa chumba cha uangalizi maalum (ICU) kwa wagonjwa wanaotoka katika chumba cha upasuaji. Hii inatokea wakati ambao tunafanya upasuaji kwa wagonjwa wengi kwa wakati mmoja hasa kipindi cha kambi za matibabu. Pamoja na ufinyu wa wodi ya watoto. Asilimia 70 ya wagonjwa tunaowafanyia upasuaji wa kufungua kifua ni watoto, tunajumla ya vitanda 123 kati ya hivi vitanda vya watoto ni 24 tu.
Wagonjwa wengi tunaowapokea mioyo yao kutokuwa katika hali nzuri hii ni changamoto nyingine tunayokabiliana nayo katika matibabu ya wagonjwa wetu.
Kwa upande wa wazazi na walezi tunawaomba wasisahau kupima afya za watoto wao pale watakapoona kuna hali ya tofauti katika ukuaji wa mtoto kwani magonjwa mengi ya moyo yanaanzia utotoni. Mtoto akianza kuuguwa magonjwa ya moyo wazazi wengi wanadhani ni matatizo ya kifua baada ya kumfikisha Hospitali na kufanyiwa vipimo ndipo inagundulika mtoto anasumbuliwa na magonjwa ya moyo. Kwa wamama wajawazito wafanye uchunguzi (Fetal Echocardiography) wa kuangalia kama mtoto aliyeko tumboni anamatatizo ya moyo.
Tunawashauri watu wazima kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara hii itawasaidia kujuwa kama wana matatizo ya moyo au la na hivyo kupata tiba kwa wakati.
Katika Bara la Afrika Taasisi yetu iko katika nafasi ya tatu katika utoaji wa huduma bora za magonjwa ya moyo hasa katika upasuaji wa moyo kwa watoto.
 
Imetolewa na:
Kitengo cha Uhusiano
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
 
15/01/2018