Watu 10,262 wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi mkoani Mwanza, hawajulikani waliko kwa zaidi ya miezi mitatu sasa baada ya kutohudhuria kliniki ya kutoa dawa hizo.

Hatua hiyo imekuja huku baadhi ya watu wanaoishi na maradhi hayo nchini wakiendelea kutafakari juu ya ama waendelee au wasiendelee kutumia dawa za kuongeza muda wa kuishi (ARV), kutokana na madai ya kuwapo kwa uchakachuaji wa dawa hizo.

Mratibu wa Ukimwi mkoani Mwanza, Dk. Pius Masele, alitoa taarifa hiyo jijini hapa wiki iliyopita wakati akitoa mada kwenye kikao kilichoandaliwa na  Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (SCCS) kwa wadau mbalimbali.

 

Lengo lilikuwa SCCS kuwataarifu wananchi matarajio yake ya kuzindua mradi unaolenga kuuwarejesha wagonjwa waliokwepa kuhudhuria kliniki kwa ajili ya kupatiwa ARV, kwani dosari zilizokuwapo zimesharekebishwa.

 

Dk. Masele alisema  watu  hao 10,262 hawajulikani  waliko  na  kwamba maendeleo ya afya zao hayajulikani, kwa vile hawajafika kliniki kwa zaidi  ya miezi mitatu sasa pasipo taarifa zozote.

 

Alibainisha kuwa idadi  hiyo  ni sehemu  ya  watu   34,422   waliojitokeza  kupimwa   afya  zao tangu  mwaka 2004  kupitia   maeneo  yaliyotengwa  na Serikali,  ambapo ilibainika kuwa  wanatakiwa   kutumia ARV.

 

Katika hatua nyingine, Dk. Masele alisema watu 4,455  wameripotiwa  kufa   mkoani  hapa   kutokana   na  Ukimwi, tangu Serikali  ilipoanzisha   huduma  ya  kutoa   ARV  mwaka  2004.

 

Alifafanua kuwa  watu hao  ama wamefariki  kutokana  na kushindwa  kuzingatia  masharti  ya matumizi  ya  dawa hizo,  au  kuchelewa  kupima   afya zao.  Hata hivyo, alisema  idadi  ya  maambukuzi  mapya ya VVU na vifo vinavyotokana  na Ukimwi  imepungua  ikilinganishwa na miaka iliyopita.

 

Kwa   mujibu  wa Dk.   Masele,  takwimu   hizo   zimekusanywa   hadi   kufikia  Machi  mwaka huu,  na kwamba  zinajumuisha Wilaya  ya Busega mkoani  Simiyu  na Wilaya  ya Geita mkoani Geita.

 

Kwa upande wake, Meneja wa SCCS Kanda ya Ziwa, Richard Mbwambo, alisema tume  hiyo  inatarajiwa  kuzindua  mradi utakaowezesha kurejesha  watu  wote waliokwepa kuendelea na matumizi ya ARV.

 

Pamoja   na  sababu  nyingine,  Mbwambo alisema  lengo  la mradi  huo  ni kupunguza  vifo  miongoni  mwa  watu   wenye  VVU/Ukimwi.

 

Alisema   mradi  huo   utazinduliwa  mwishoni   mwa  mwezi  huu   katika Hospitali  ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure,  ambapo  Mkuu  wa Mkoa  huu, Mhandisi  Evarist  Ndekilo,  anatarajiwa  kuwa  mgeni rasmi.


 

By Jamhuri