Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, Januari 25 alifanya ziara fupi Loliondo wilayani Ngorongoro, Arusha.

Malengo ya ziara hiyo yalikuwa kukagua vyanzo vya maji vilivyoharibiwa na maelefu ya mifugo kutoka ndani na nje ya nchi katika eneo la Loliondo; na pia kukagua kazi ya uwekaji ‘beacos’ katika mipaka ya Pori Tengefu Loliondo (LGCA), Hifadhi ya Taifa Serengeti (SENAPA) na Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro (NCAA).

Profesa Maghembe na mwenyeji wake, Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Mfaume Tika, walizuru vyanzo viwili vya mito. Vyanzo hivyo ni Olomanaa katika Kijiji cha Piyaya, na Oltigomi kilichoko kijijini Ololosokwan.

Kote huko, alishuhudia maelfu kwa maelfu ya ng’ombe, mbuzi na kondoo ambayo ni mali ya Watanzania na Wakenya.

Katika chanzo cha Olomanaa, Profesa Maghembe, aliweza kuoneshwa watu wanaodaiwa kuwa ni raia wa Kenya, ambao wanajulikana kwa uvaaji wao (huvaa vibwaya), alama za nchi yao (mikanda na urembo mwingine) na kutoweza kuzungumza lugha ya Kiswahili.

“Ninyi Wakenya nawaamuru mrudi kwenu Kenya. Watanzania pekee hawana mifugo ya kushindwa kutoshelezwa na malisho na maji. Haya tunayoyaona ya ukame na upungufu wa maji yanasababishwa na wingi wa mifugo kutoka Kenya. Mkuu wa Wilaya watu wako hawa hakikisha wanarudi kwao kwa sababu hata sheria za kimataifa haziruhusu watu kuingia nchi nyingine na kufanya mambo wanavyotaka. Please, go back to your country,” alisema Profesa Maghembe.

Baada ya kutoka hapo, Profesa Maghembe na msafara wake walienda hadi Oltigomi ambako ndiko kwenye mpaka wa LGCA na SENAPA. Hapo alishuhudia maelfu ya ng’ombe wakisogezwa mpakani ili usiku waingizwe hifadhini Serengeti. Akaagiza ng’ombe hao wazuiwe hata ikibidi kwa kuongeza nguvu ya askari wayamapori.

Yafuatayo ni mazungumzo -neno kwa neno ya Waziri Maghembe na DC Tika wakiwa Oltigomi.

 

Waziri Maghembe 

Serengeti, hii ndio hifadhi bora kuliko zote hapa barani Afrika na kwa kweli kwa maana ya kuona wanyama makundi makubwa katika dunia- ndio nzuri kupita zote duniani. Kwa hiyo ni rasilimali kubwa sana ya nchi yetu. Kwa maana hiyo lazima tufanye kila juhudi za kuiokoa- kwa gharama yoyote lazima tuiokoe Hifadhi ya Serengeti.

Hifadhi hii inahatarishwa na vitu vingi hapa sasa. Cha kwanza, kukauka maji ya mito na vijito na hii inatokana na shughuli za binadamu hasa kuchunga ng’ombe, kondoo, mbuzi na wanyama wengine ambao tunafuga. Hii ndio moja ya hatari kubwa sana inayohatarisha uhai wa Serengeti.

Vyanzo hivi vya maji ambavyo tumevipita hapa leo mmeona ninyi wenyewe. Pale njiani (Mto Olomanaa, kijijini Piyaya) ni moja ya chemchem za maji zinazoingia kwenye mto mkubwa, mmeona ng’ombe zote zimehamishiwa pale na ni nyingi sana. Hakuna namna yoyote ambayo wanyama wanaweza kukanyaga pale kwa mwaka mmoja, kwa mwaka kesho na mwaka keshokutwa halafu bado mto upo-haiwezekani. Hapa (Mto Oltigomi kijijini Ololosokwan-unamwaga maji Mto Grumeti) mmeona kumeshakauka, na huu ndio mto mkubwa Serengeti ukiacha mto Mara. Kwa sababu hiyo, lazima tufanye juhudi tuweze kuokoa huu mto ili wanyama kule Serengeti na wenyewe waweze kuokoka. Kwa hiyo ni muhimu niseme kwamba kama Serikali tumefurahi sana juu ya mazungumzo yanayoendelea kwa ajili ya kuweka matumizi bora ya ardhi kwa ajili ya eneo hili la Pori Tengefu Loliondo. Nadhani mazungumzo yanaendelea vizuri na mwelekeo wake mzuri.

Wako watu ambao wanafaidika kukiwa na mgogoro hapa. Wako wengi sana. Wanatamani huu mgogoro usiishe, lakini wakati umefika sasa Serikali lazima iweke msimamo na ifanye maamuzi makubwa. La kwanza, tangu mwaka 1990; miaka yote hii mpaka sasa kumekuwa na tathimini mbalimbali zinafanywa kwenye eneo hili na mojawao ni kugawanya eneo hili la Pori Tengefu Liliondo kwenye maeneo mawili-eneo moja liwe kwa matumizi ya wananchi na eneo lingine lilinde rasilimali ya Serengeti. Na kwa sababu hiyo, hili eneo la kilometa za mraba 1,500 ni lazima litengwe, yaani hakuna suala la mjadala hapa maana lazima tufike mahali tujue Serengeti haiwezi kupona bila hiyo. Lakini wananchi pia wanahitaji maji kwa hiyo tutakachoanza kufanya tutatafuta wataalamu wataanza kutafuta maji kwenye maeneo ambayo wananchi wanakaa ili tuweze kuona namna gani tunaweza kupatia maji mifugo ile ya wananchi wa Tanzania wanaoishi katika maeneo haya.

Eneo hili la kilometa za mraba 1,500 hilo lazima litengwe kama eneo la hifadhi. Na mimi ninavyoona kama hali itazidi kuwa mbaya kiasi hiki, itabidi tulihifadhi kabisa – liwe sehemu ya Serengeti. Liwe kabisa sehemu ya mbuga, lakini ili kuhakikisha kwamba tunatoa maji tuwapelekee wananchi, tunaweza kuwapa wananchi huduma tutaanza kwanza chini ya Sheria Namba 5 ya mwaka 2009 kulitenga liwe eneo la uhifadhi na lile eneo lingine wananchi wapewe na wasimamiwe na wilaya namna ya matumizi ya kilometa zile za mraba 2,500.

Haya maeneo ni maeneo makubwa, hatuwezi kuyapima kwa idadi ya hawa wanyama (mifugo) waliopo kwa sababu zaidi ya nusu ya wanyama  (mifugo) waliopo si wa Tanzania wala si wa wananchi wa Tanzania. Hatuwezi kuanza kuhesabu ugali, tunapika ugali nyumbani na tunahesabu na ugali wa jirani, hata kidogo! Kwa hiyo tunawaomba kwenye Serikali hapa wilayani mtusaidie kufanya uchunguzi wa haraka na ‘effective’ tujue ng’ombe za Kenya ni zipi na za Watanzania ni zipi; Wakenya ni kina nani na Watanzania ni kina nani-ng’ombe zetu zote zianze kuwekwa alama. Wananchi wetu wapewe vitambulisho vya uraia wa Tanzania ili sasa tujitenganishe na majirani zetu maana hata watu wetu walioko Kenya wiki mbili zilizopita walifukuzwa. Kwanini sisi tunawa-entertaine Wakenya hapa? Haiwezekani.

Kwa upande wa Tanapa (Shirika la Hifadhi za Taifa) kazi hii ya kuweka alama kwenye mipaka mmalize. Mkishamaliza muanze kuweka mipaka kwenye eneo hilo la kilometa za mraba 1,500 wakati huo wale wataalamu wanaoliangalia watakuwa wamemaliza. Muanze kazi ya kuweka alama (beacon) kwenye hilo eneo na wale watu wana maboma humo ndani waanze kuangalia maeneo mengine ya kuweka maboma yao kwa sababu baada ya tarehe 30 Machi (mwaka huu) lazima tuwe tumelitangaza eneo hilo kama eneo la hifadhi na wakati tutakuwa tumeangalia na kujua ni maeneo gani tunaweza kuwasaidia wananchi wapate maji kwa ajili ya mifugo. Tutaendelea na yale mazungumzo na yatamalizika vizuri. Hawa wanyama (ng’ombe) wote mnaowaona hapa wanaandaliwa leo usiku waende Serengeti, na kila siku ni hivyo. Kwa utaratibu huu Serengeti haitapona. Tutaongeza askari, lakini pia tubadilishe utaratibu wa kushughulika na jambo hili. Sheria Namba 5 inataka mtu anayepeleka vitu visivyotakiwa ndani ya hifadhi akamatwe na vitu hivyo, ashitakiwe. Anzeni kufuata sheria. Kuanzia leo mtu anayeingia humu ndani (hifadhini) kesho tunataka kusikia wamepelekwa Wasso na ng’ombe zao- kushitakiwa; na hizo ng’ombe muanze kuzitaifisha. Ndiyo njia ya kuzuia watu wasiingie kwenye hifadhi. Msianze kuwapiga faini Sh 50,000 kwa kila ng’ombe-wataanza kuonyesha ubingwa wa pesa zao. Taifisha hizo ng’ombe zote, taifisha hizo mbuzi zote – watajua si busara kuingiza mifugo kwenye hifadhi. Asanteni sana.

 

Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro

Nilipopata taarifa Mheshimiwa Waziri anakuja, nilisema ‘karibu’ maana wakati mwingine ni jambo jema kuja ‘site’. Ukikaa Dodoma, ukikaa Dar es Salaam ukawa unasema- zote ni kauli, lakini wakati mwingine zinaweza kupishana na zilizoko ‘site’. Jambo kubwa ambalo ametoka kulisema sasa ambalo na mimi naunga mkono kwa asilimia 100 kwa sababu nilianza mchakato huu ni kwamba yapo mazungumzo yanayoendelea sasa katika kujaribu kuleta maridhiano bila kuathiri sheria zilizopo. Na hili ni jambo la kawaida, linafanyika. Sheria ni za Tanzania na wanaozungumza ni Watanzania kwa hiyo nadhani kwamba kama maslahi mapana tumeshatoka kuzungumza kwamba lazima tuangalie hifadhi zetu hizi-siyo hii tu (Serengeti). Tumetoka kule kwenye ‘beacon’ inayopakana na Ngorongoro. Ile ni hifadhi yetu pia na zipo nyingine kadha wa kadha. Lazima tuhakikishe kwamba zinalindwa na ecosystem yote hii ya Serengeti, lakini lazima pia tuone kwamba hatima ya wananchi wetu ambao wamekuwa katika maeneo haya ambayo kwa sehemu kubwa baadaye mimi nafikiri ndio wawe wahifadhi namba moja. Lazima tuangalie na wenyewe itakuwaje. Yale matatizo yao ya msingi-suala la maji, suala la malisho na kadhalika lazima yatazamwe vizuri. Lakini pia amehitimisha masuala ya wawekezaji wetu ambao wapo hapa ambao wanalipa na ndio wanao-promote utalii wenyewe tunaozungumza. Sasa na wenyewe lazima tuangalie. Kwa hiyo kuna u-tatu ambao kama Serikali na wananchi lazima wakae pamoja wajadili. Hiyo ndio kauli yangu kwamba lazima maslahi yote matatu yalindwe kwa pamoja.

Niseme tu kwamba mazungumzo haya yanaendeshwa na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa (Mrisho Gambo) na ninavyofahamu mimi ni kuwa mchakato bado unaendelea. Pengine nitumie nafasi hii kukanusha kauli zilizozagaa kwamba watu wanasema hatujafikia mwafaka…hatujaenda kufika hatua ambayo tunasema tumefikia mwafaka. Mimi ninachofahamu ni kuwa tunaenda na kama alivyosema Mheshimiwa Waziri tunaenda vizuri. Na ni kitu cha kawaida mnakwenda, mnasimama mnaangalia mlikotoka; mnapanga tena mnakwenda mbele, lakini mwishowe ninavyofahamu ni kwamba hayawezi kuwa alfu lela ulela – mazungumzo ambayo hayana mwanzo na hayana mwisho! Yatafika siku yatakuwa na mwisho, na mwisho huo uwe mzuri ninaoamini kama Mkuu wa Wilaya hii utakuwa umezingatia maslahi ya pande zote tatu- maslahi mapana ya hifadhi zetu hizi. Na hapa lazima ieleweke si maslahi tu ya Serikali, ni maslahi mapana ya hifadhi kwa sababu hizi hifadhi ni za kwetu. Lakini pia itaangalia na wananchi wenyewe ambao ndio wenye hizo hifadhi, lakini pia wageni kwa maana ya wawekezaji wanaokuja kutu –promote na kutupatia mapato kwa hiyo naamini yatakuwa mazuri kwa sababu hadi Mkuu wa Mkoa anayaahirisha Jumamosi iliyopita (Januari 21) tulikuwa hatujatofautiana. Kila mtu aliridhika kuwa hapa tulipofika tunakwenda vizuri na ninaamini Mungu atatufikisha huko.

 

Waziri Maghembe

Lazima tupunguze athari, ndicho ninachosema hapa. Lazima tuchukue hatua, tupunguze athari na tuwaeleze wananchi wasipeleke ng’ombe huko (hifadhini Serengeti) na ndio maana nimesema kuanzia sasa lazima wabadilishe utaratibu wa kushughulikia jambo hili badala ya kuwatoza faini ya kuingiza ng’ombe- ni kama kulipa kodi ya kwenda kuchunga huko ndani. Wapelekeni mahakamani wahukumiwe kwa sheria ya wanyamapori.

 

Mkuu wa Wilaya

Nafikiri amefafanua vizuri. Toka mwanzo hili liko very clear, lieleweke kuwa kupeleka vitu visivyoruhusiwa na hapa tuzungumze kwa ujumla wake-mifugo ndani ya hifadhi ni kosa. Bahati nzuri Mwenyekiti (wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro), amezungumza sasa. Si kwamba tunaendelea na mazungumzo sasa- hayajafika mwisho, basi unapandisha (mifugo) kupeleka hifadhini, hapana. Ukipeleka huko unakutana na mkono wa sheria na huwa hatufanyi chochote tunaiacha sheria ichukue mkondo wake. Kwa hiyo hili lazima niliseme ndio maana nimesema tusitishike wala tusijipe holiday kwamba tunaendelea na mazungumzo kwa hiyo tuharibu, hapana. Meseji hiyo hatuwezi kuikubali hata kidogo.

 

Madiwani

Baada ya kauli ya Profesa Maghembe, Januari 26 madiwani kadhaa walikutana na Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro ofisini kwake na kufanya mazungumzo.

Matokeo ya mazungumzo hayo ni taarifa ya inayodaiwa kuwa ni ya Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, isiyokuwa na majina wala tarehe iliyotolewa kupinga msimamo wa waziri huyo kuhusu kutengwa kwa kilometa za mraba 1,500.

Taarifa hiyo ya ‘Baraza’  ilitoa mapendekezo manne:

Mosi, Wizara ya Maliasili na Utalii kuachana na mpango wa kukata au kumega eneo la ardhi ya vijiji vya  Loliondo

Pili, Kuruhusu majadiliano ya kutafuta suluhu ya kudumu inayotokana na wadau wote uendelee kwa kuzingatia maslahi ya wananchi, uhifadhi na uwekezaji.

Tatu, Maelekezo ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa yaendelee kuwa dira ya mjadala wa wadau wa kutafuta suluhu ya mgogoro, na

Nne, Serikali na wadau wa mgogoro huu wazingatie sheria za ardhi na nyingine katika kufikia mwafaka wa kudumu wa mgogoro huu.

 

Kinachoendelea Loliondo

Sintofahamu ilijitokeza Ijumaa na Jumamosi za tarehe 20 na 21 Januari ambako Kamati mpya jumuishi iliundwa ili kuunganisha mada mbalimbali zilizoripotiwa ili kupata ripoti moja ya maridhiano.

Kamati hiyo iliwashirikisha wawakilishi mmoja mmoja wa Tume ya Taifa ya Mpango na Matumizi Bora ya Ardhi, Wanyamapori, TANAPA, NCAA, TAWIRI, OBC, Thomson, Andbeyond, GIZ & Frankfrurt na kuunganika na Kamati ya Jamii, Mkoa na Wilaya.

NGOs, Kamati ya Jamii, Wazee wa Mila, Wawakilishi wa Akinamama, Vijana na Wazee Mashuhuri, Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji na wananchi wengine walioingia ukumbini mwa Domel ambao wengi wao ni wenyeviti wa vitongoji.

Waliingia ukumbini bila ruhusa wakidai kwamba hawakushirikishwa kutoa maoni na mapendekezo yao juu ya ripoti iliyounganishwa. Baada ya kikao kumalizika na kufungwa rasmi na RC Gambo  walitoka nje ya ukumbi wakiwa wamejawa hasira, wakasusa kula chakula na walikwenda Oloip Bar & Guest House kwa Matthew Timan na kufanya kikao chao.

 

Wakapitisha maazimio yafuatayo:

(i) Wao kama NGOs, Kamati ya Jamii, Wazee wa Mila, wawakilishi wa akinamama, vijana na wazee mashuhuri, madiwani na wenyeviti wa vijiji wa kata saba wamejiondoa kwenye mchakato mzima wa maridhiano ya Pori Tengefu katika kikao cha wadau cha RC Gambo na DC Mfaume Taka.

(ii) Wataanzisha kamati yao na itakayofuata utaratibu wao wa kuitisha vikao kwenye vijiji vyote vya kata saba, mihutasari ya uamuzi watapeleka ngazi ya kata saba ipate baraka kisha watapeleka katika Baraza la Madiwani ipate baraka pia; na mwishowe wapeleke kwa Waziri Mkuu hadi kwa Rais.

(iii) Msimamo wao ni kudai hifadhi ya Jamii (WMA) ianzishwe ndani ya ardhi za vijiji vya kata saba ambavyo vilikwishasajiriwa na kupewa vyeti vya vijiji na wanadai Serikali lazima irudishe vyeti hivyo na kuvibariki kwa ajili ya kuanzisha WMA.

(iv) Msimamo wao ni kupinga kwa nguvu zote na kukataa katakata LGCA mpya ya kilometa 1,500

(iv) Wapiga debe wakuu wa WMA ni Damian Bell wa NGO ya Honey Guide, Dk. Karaine Kuneei wa Frankfrurt Zoological Society-Loliondo; NGOs za PWC, UCRT, NGONET, PINGOS FORUM, TPCF, PALISEP, TNRF, Ndorobo Safaris, Northern Tanzania Rangelands Initiative na maswaiba wao kama Mbunge wa Ngorongoro na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, William Nasha; Mwenyekiti wa Halmashauri Siloma; Mwenyekiri wa CCM Wilaya ya Ngorongoro, Ibrahimu Sakai; Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Michael Lekule Laizer, na baadhi ya madiwani, wazee wa mila, wenyeviti na wanaharakati. Kinachofanywa sasa ni ukusanyaji fedha kutoka sehemu mbalimbali kwa ajili ya kufanikisha mpango wa kuanzishwa kwa WMA.

Vikao vinaandaliwa kote kote – jijini Arusha na Loliondo ili kuipitisha WMA na kuondoa Pori Tengefu. Bila Serikali kuchukua ‘maamuzi’ magumu, mgogoro wa Loliondo hautakoma. Mbaya zaidi, viongozi kadhaa wa Serikali wako upande wa NGOs.Mtendaji wa Kijiji cha Luchili, Kata ya Nyanzenda, Halmashauri ya Buchosa Sengerema, mkoani Mwanza anatuhumiwa kumtorosha Mchungaji wa Kanisa la Agape, lililopo katika kijiji hicho, Geofrey Kamuhanda, anayetuhumiwa kumbaka na kumlawiti binti wa miaka 13.

Vyanzo vya habari vimeiambia JAMHURI kuwa tukio la kubakwa kwa mtoto huyo na Mchungaji Kamuhanda, lilitokea Januari 10 mwaka huu kijijini hapo.

Siku moja baada ya tukio, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Luchili, Mathias Njulilo, alimkamata Mchungaji huyo ila ofisi yake ikamwachia katika mazingira ya kutatanisha.

“Baada ya tukio hilo, ofisi ya Mtendaji iliagiza Mchungaji huyo kukamatwa mara moja kwa hatua zaidi ikiwamo kupelekwa polisi, lakini saa chache baada ya kufikishwa ofisini hapo, Mchungaji huyo aliachiwa katika mazingira yenye utata na yaliyoacha maswali mengi kwetu,” anasema mtoa taarifa.

Taarifa zinaonesha baadhi ya wachungaji wa madhehebu ya Kikristo katika kijiji hicho walimchangia nauli Mchungaji huyo akaondoka, huku wananchi wakiutupia lawama uongozi wa kijiji kwa kukumbatia uozo na kuiomba Serikali kuwachukulia hatua kali za kisheria.

Dada wa binti aliyefanyiwa ukatili huo (jina tunalihifadhi) anasema kuwa mdogo wake alifika kwake maeneo ya Kashai, Bukoba Mjini akiwa amebakwa na kuumizwa vibaya kutokana na ukatili huo.

Anasema Mchungaji alimchukua mdogo wake kwa ajili ya kwenda kumsomesha na hakujua kama alikuwa na lengo jingine la kumfanyia unyama huo na ambao umemwachia kilema cha kudumu kilichotokana na kumbaka.

“Naiomba Serikali hii ya awamu ya tano kwa vile imeapa kukomesha vitendo hivi, basi ianze na waliohusika kumtorosha, kwani hawa ndiyo wanaofahamu alipo Mchungaji huyu aliyevaa ngozi ya kondoo wakati ni mbwa mwitu mkali. Wala hatukuwahi kuwaza kwamba ndugu yetu angekuja kukumbana na tukio hili kwenye maisha yake,” anasema dada huku akibubujikwa na machozi.

Akisimulia tukio hilo, binti aliyebakwa (jina linahifadhiwa) anasema Mchungaji alimwomba kwa wazazi wake wanaoishi katika Kijiji cha Izibwa, Wilaya ya Bukoba Vijijini kwa lengo la kwenda naye wilayani Sengerema, mkoani Mwanza amsomeshe.

Anasema baada ya siku nne akiwa nyumbani kwa Mchungaji huyo, alimuuliza kuhusu shule na kujibiwa kuwa atampeleka shule asijali.

Anasema usiku wa siku hiyo saa chache tangu alipotaka majibu ya lini angepelekwa shule, Mchungaji Kamuhanda alimfuata chumbani akiwa amelala na kumkaba koo kisha kumfanyia unyama huo kwa kumbaka na kumlawiti huku

By Jamhuri