Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT), Zitto Kabwe ameangukia pua baada ya kubainika kuwa hoja anayojenga bungeni ni ya “kubumba”, Uchunguzi wa JAMHURI umebaini.
Kwa muda sasa Zitto amekuwa akitoa matamko bungeni na kuandika katika mitandao ya kijamii kuwa ndege ya Boeing 787 – 800 iliyonunuliwa na Serikali ni mbovu, wakati uhalisia ndege hiyo ndiyo kwanza matengenezo yake yameanza.
Ukweli kuhusu ndege mpya aina ya Boeing 787-800 Dreamliner iliyonunuliwa na Serikali, umejulikana.
Kwenye mitandao ya kijamii na hata katika Bunge, Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT), amekuwa akitoa taarifa zenye mwelekeo wa kuaminisha umma kuwa Serikali imenunua Terrible Teen ambazo zina matatizo ya kiufundi na kwa gharama kubwa.
Hata hivyo, uchunguzi wa kina uliofanywa na JAMHURI umebaini kuwa sakata hili limegubikwa zaidi na vita ya kibiashara. Nyaraka za mawasiliano ambazo JAMHURI limezipata zinathibitisha hilo.
Uchunguzi umebaini kuwa si kweli kuwa ndege inayosemwa imenunuliwa kwa dola milioni 224.6 za Marekani (zaidi ya Sh bilioni 450).
JAMHURI limefanikiwa kuona mkataba wa Boeing na Serikali kwenye ununuzi wa ndege hiyo ya Boeing 787-800 Dreamliner na kubaini kuwa imenunuliwa kwa dola milioni 150 za Marekani (zaidi ya Sh bilioni 330).
Hadi makubaliano hayo yanafikiwa kati ya Boeing na Serikali, kulikuwa na majadiliano ya kimkataba yaliyoongozwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali; Wakala wa Ndege za Serikali; Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) na Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA).
Uchuguzi uliofanywa na JAMHURI umethibitisha kwamba kulikuwa na muda wa kutosha wa majadiliano kabla ya kusaini mkataba wa matengenezo ya Dreamliner.
JAMHURI limebaini kuwa Dreamliner iliyonunuliwa na Serikali ya Tanzania na inaweza kuruka kutoka Dar es Salaam hadi Guangzhou China ikiwa imejaza abiria na na mzigo wa tani 13.3 ukilinganisha na Terrible Teens, ambayo ina uwezo wa kubeba tani 5.8 tu.
Hii ina maana ndege iliyonunuliwa na Serikali inabeba mzigo tani 7.5 zaidi ikilinganishwa na hiyo yenye matatizo anayoisema Zitto.
Mmoja wa maafisa wa Boeing, Morris Keelan, ameliambia JAMHURI kuwa ndege inayotengenezwa kwa ajili ya Tanzania, si miongoni mwa Terrible Teen, huku akithibitisha kwamba ndege iko kwenye matengenezo kuanzia ngazi ya awali kabisa (tazama picha ukurasa wa kwanza).
“Kwa ufafanuzi, kulikuwa na ndege chache za Boeing 787-800 zilizokuwa zinatengenezwa kiwandani kwetu, vyombo vya habari viliziita ‘terrible teens’ kwa sababu namba za kutengenezwa kwake zilikuwa kati ya 12-20.
“Ndege hizo zimekwishauzwa na kukabidhiwa kwa wateja wetu, na zimekuwa zikiendelea kufanya vizuri na kuthibitisha ubunifu wetu katika teknolojia na uchumi imara kama zilivyo Boeing 787 Dreamliners,” amesema Keelan.
Akizungumza kuhusu Dreamliner, ndege yenye uwezo wa kubeba abiria 264, Keelan anasema ndege hiyo kwa ajili ya Tanzania bado haijaanza kuunganishwa (assembling), huku akithibitisha kuwa shughuli ya kutengeneza vifaa vya kuunganisha ndege hiyo inaendelea vizuri.
 “Bado hatujaanza kuunganisha ndege ya Tanzania, hatuwezi kuanza leo, ni mpaka mwaka 2018 kama tulivyokubaliana kwa mujibu wa mkataba…sasa tunaendelea kuandaa mahitaji muhimu katika ndege hiyo kama mahitaji tuliyopewa na mteja wetu,” amesema Keelan.
Anasema, hadi Oktoba 31, mwaka jana kampuni ya Boeing ilikuwa imepokea oda 1,208 za ndege aina ya Boeing 787-800 Dreamliner zinazofanana na ile iliyonunuliwa na Tanzania (line number 719).
Keelan ameliambia JAMHURI kuwa kazi ya uchaguzi wa namna ndege ya Tanzania itakavyokuwa (configuration) ilimalizika katikati ya Machi, wakati uchaguzi wa injini bado unaendelea.
“Hivyo, ndege ya Tanzania ndio iko katika hatua za mwanzo kabisa za ununuzi wa vifaa vya kuitengeneza,” amesema.
Taarifa ambazo JAMHURI limezipata zinaonesha kwamba mpaka sasa Serikali inaendelea na uchambuzi wa aina ya injini zitakazotumika katika Boeing 787-800 Dreamliner. Wauzaji wakubwa wa injini hizo duniani ni General Electric (GE), Rolls-Royce na United Technologies (Pratt & Whitney).
Mchakato wa kutengeneza ndege unahusisha utengenezaji wa sehemu mbalimbali (parts) na mifumo ya ndege ambayo hutengenezwa nchi tofauti duniani na baadaye kupelekwa katika kiwanda kimoja kwa ajili ya kuunganishwa.
Mfano, mkia na mabawa ya ndege zilizo nyingi hutengenezwa nchini Malaysia na kuuzwa kwa nchi za Magharibi ikiwa sehemu mfu wa biashara ya ndege wenye kunufaisha nchi nyingi kwa wakati mmoja inapotengenezwa na kuuzwa ndege angalau moja.
Hatua hiyo hufuatiwa na uunganishaji (assembling) wa sehemu hizo ili kupata umbo kamili la ndege, uwekaji mifumo na mitambo mbalimbali inayotumiwa na ndege, kuweka muundo wa ndani wa ndege (interior installation) uliochaguliwa na mnunuzi, na mwisho upakaji rangi.
Baadaye uunganishaji hufanyika katika kiwanda cha Boeing nchini Marekani. Mnunuzi wa ndege anaweza kushiriki ukaguzi wa awamu mbalimbali za uunganishwaji wa ndege ili kujiridhisha kama ubora umefuatwa katika utengenezaji wa ndege yake.
Ndege iliyonunuliwa na Serikali ni Boeing Line number ni 719 na serial number yake ni 64249, tofauti na maelezo yaliyoko katika tovuti inayodai kuwa Tanzania imenunua ndege mojawapo ya ndege za Boeing zijulikanazo kama Terrible Teens Dreamliners zilizokataliwa na mashirika mengine ya ndege duniani.
Maelezo ya ndege inayodaiwa kununuliwa na Tanzania ni tofauti kabisa na maelezo rasmi yaliyotolewa na kampuni ya Boeing, serial number na line number (ambayo huonesha ni ndege ya ngapi kutengenezwa) ilizopewa ndege ya Tanzania ni tofauti  na zilizoko katika tovuti isiyomilikiwa na Boeing.
Ndege moja haiwezi kuwa na line number na serial number mbili tofauti, hata kama ikiwa imefanyiwa ukarabati mkubwa line number na serial number hubaki zile zile.
Akizungumza na JAMHURI, Mkurugenzi Mtendaji wa ATCL, Mhandisi Ladislaus Matindi amesema kuna maneno mengi yanasemwa kuhusu ndege hiyo mpya ambayo ni upotoshaji mtupu.
“Kuna taarifa kuwa ndege ni ya zamani na bei yake ni kubwa, lakini sitaki kuzungumzia mambo ya mkataba hapa, zaidi ya ukweli kwamba ndege yetu bado haijaanza kutengenezwa kwani ni lazima tuhusishwe katika awamu zote za utengenezaji.
“Kwa mujibu wa vigezo tulivyovichagua kama wanunuzi ili kuhakikisha kuwa ndege tuliyonunua na kukubaliana katika mkataba ndio inaletwa Tanzania, ratiba ya utengenezaji wa ndege yetu tunayo. Kwa ufupi hiyo ndege inayosemwa mitandaoni na bei yake haviko katika makubaliano kati yetu na Boeing,” amesema Matindi.
Mei, mwaka huu, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, aliliambia Bunge; “Serikali imeingia Mkataba na Boeing wa kutengeneza ndege mpya yenye line number 719, ndege inayozungumzwa hapa [inayosemwa na Zitto] Kama tumechukua ilikuwa iende Rwanda ina line number 19. Yetu sisi ni line number 719; ni tofauti.”
Akizungumza na JAMHURI,  Kabwe ambaye amekuwa mstari wa mbele katika ‘kuhoji’ gharama za ndege hizo na ubora wake kwa mujibu wa fedha zilizotolewa, amesema hoja yake kubwa ni kwamba kama Serikali imenunua Terrible Teens, basi bei yake ilipaswa kupungua kama ilivyokuwa kwa Shirika la Ndege la Ethiopia.
“Boeing wanasema bei (list price ni USD 224.6 milioni). Serikali muda wote imekuwa ikiliambia Taifa kwamba wamenunua ndege hiyo kwa bei inayotajwa na Boeing.
“Hata hivyo Waziri amesema ndani ya Bunge kuwa pamoja na  kuwekewa bei hiyo kwenye tovuti mazungumzo marefu yalifanyika na ndio tulipewa punguzo kubwa.
“Swali linaloibuliwa sasa ni, kama tunanunua ndege mpya kabisa na siyo Terrible Teen, kwanini tumepewa punguzo kubwa sana? Sasa tumelipa kiasi gani baada ya hilo punguzo? Mazungumzo marefu yalihusu nini kama tunanunua ndege mpya kabisa?” Amehoji Zitto
Anasema amepitia taarifa ya Serikali bungeni, hususan randama za Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili kuona taarifa ya miamala ya malipo kwa ndege hii. Serikali imelijulisha Bunge kuwa imeshalipa takribani asilimia 44.6 ya bei ya ndege iliyoagizwa.
Anasema kwa mujibu wa randama hizo, Serikali imeshalipa dola milioni 67 za Marekani, (zaidi ya Sh bilioni 134) kwa kampuni ya Boeing ambako dola milioni 10 za Marekani (zaidi ya Sh Bilioni 22) zililipwa Desemba, mwaka jana.
“Kwa niaba ya wananchi wote wa Tanzania nimechukua hatua ya kumwandikia Spika kumwomba kupatiwa mkataba kati ya Serikali na Boeing na ushahidi wa miamala yote ya malipo ya fedha kutoka Hazina ya Tanzania kwenda Boeing au kwingine kokote kunakohusiana na ununuzi wa ndege hii Dreamliner Boeing 787-800,” amesema Zitto.
Uhuru huo wa kuomba kupatiwa nyaraka hizo, unatajwa katika kifungu cha 10 cha Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge, Sheria Na. 3 ya mwaka 1988.
Akizungumza na JAMHURI, Katibu Mkuu anayeshughulika na Sekta ya Uchukuzi, Dk. Leonard Chamriho, amesema kumekuwapo mchakato wa wazi katika kuwapata wazabuni wawili ambao kimsingi ndio watengenezaji wa ndege hizo kubwa.
“Kutokana na ukweli kwamba watengenezaji wa ndege aina hiyo ni wawili tu, tuliamua kutumia ‘restricted tender’ ambayo kimsingi Sheria ya Unuuzi na Ugavi inaturuhusu kufanya. Tulifanya hivyo kutokana na mazingira yenyewe tuliyonayo,” amesema Dk. Chamriho.
Amesema, katika zabuni hiyo zilijitokeza kampuni mbili za utengenezaji wa ndege, ambazo ni Boeing na Air Bus.
Ameliambia JAMHURI kuwa kampuni zote ziliruhusiwa kuwasilisha taarifa za bidhaa zao mbele ya jopo la wataalamu. Dk. Chamriho anasema wote walionesha ugumu wa kupatikana ndege kwa haraka, lakini pamoja na vingine vilivyozingatiwa, ilikuwa gharama pamoja na mahitaji ya ndege hiyo kwa wakati ambao inahitajika.
“Ninakumbuka Air Bus walituambia wataweza kutupatia ndege hiyo kuanzia mwaka 2023, huku wakitupatia chaguo la kukodi ndege kama hiyo. Hatukuhitaji kukodi maana tunayo historia mbaya katika mikataba ya kukodi ndege.
“Boeing wao walisema wanaweza kutupatia slot ndani ya Juni 2018; kutokana na mazingira tukalazimika kuendelea na mazungumzo na Boeing, walitutaka kuweka fedha za dhamana ya kutengeneza ndege hiyo. Tuliwalipa dola milioni 10 za Marekani (zaidi ya Sh bilioni 22).
“Baada ya kulipa malipo hayo, tulipewa muda wa mwezi mmoja kujadiliana kuhusu masharti ya mkataba wetu wa kununua ndege hiyo pamoja na vipimo (specification) kwa mujibu wa mahitaji yetu,” Katibu Mkuu, Dk. Chamriho ameliambia JAMHURI.
Amesema Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Wilson Masilingi ameshiriki katika kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.
“Balozi Masilingi alifanya ziara makao makuu ya Boeing na kukutana na rais wa kampuni hiyo, mazungumzo yao yameleta ahuane kubwa sana katika majadiliano mpaka kufikiwa kwa makubaliano ya mkataba,” amesema.
Kuhusu muda wa majadiliano hadi kufikia makubaliano ya kusaini mkataba, Katibu Mkuu huyo anasema iliwachukua “muda wa kutosha”  kujadiliana na hatimaye kusaini mkataba wa ununuzi wa ndege.
Dk. Chamuriho amesema baada ya kutiliana saini, ulifanyika utaratibu kwa ujumbe wa Boeing kwenda kumwona Rais John Magufuli. “Walikwenda kufanya ‘courtesy call’, hiyo ilikuwa baada ya makubaliano yetu kukamilika”.
Hata hivyo Dk. Chamriho, hakuwa tayari kuliambia JAMHURI, serikali imelipa kiasi gani, huku akisisitiza kwamba, serikali haikulipa kiasi cha fedha kilichowekwa kwenye mtandao wa Boeing.
“Pale kwenye mtandao wao wameweka list price, baada ya majadiliano bei ilipungua, lakini kwa mujibu wa mkataba tulioingia na kampuni hiyo, sitakiwi kusema tumekubaliana kiasi gani, lakini kwa hakika maana sisi tulikuwa na fedha mkononi, gharama ilipungua,” amesema Dk. Chamriho
Taarifa ambazo JAMHURI limezipata na kuthibitishwa na vyanzo vyetu, zinasema Air Bus, baada ya kukosa zabuni walianza kutoa vitisho vikiwamo vya kuishitaki Tanzania kwa Benki ya Dunia na Umoja wa Ulaya (EU), wakidai kuwa kulikuwa na utapanyaji fedha katika ununuzi wa ndege hiyo.
Aidha, Air Bus na wapambe wake walikwenda mbali zaidi hata kumchongea Dk. Chamuriho kwa Rais Magufuli.
Katibu Mkuu alishitakiwa kwa Rais Magufuli, kupitia barua iliyoandikwa na Air Bus kwenda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Katika barua hiyo, walimtuhumu Dk. Chamuriho kutowapatia kandarasi na badala yake kuwapatia Boeing zabuni hiyo ya mabilioni ya shilingi.
Alipoulizwa na JAMHURI kuhusu tuhuma hizo, Dk. Chamriho alisema ni kweli alishtakiwa kwa Rais Magufuli, kutoa upendeleo kwa kampuni ya Boeing.
“Uchunguzi umeshafanyika, nadhani waliochunguza walipata ukweli wa tuhuma hizo dhidi yangu, lakini pamoja na hayo nililazimika kuandika maelezo na naamini ukweli umebainika,” amesema Dk. Chamriho.
Katibu Mkuu huyo anawataja Hadi Akoum, Makamu wa Rais wa Air Bus, anayeshughulikia mauzo katika bara la Afrika na ukanda wa Bahari ya Hindi, pamoja na Jerome Charieras, Mkurugenzi wa Mauzo pamoja na uhusiano wa wateja, ambao walikwenda kulalamika wakihoji Boeing kupewa zabuni hiyo badala ya wao.
Anasema katika mazungumzo yao walionesha kwamba hata Boeing hawataweza kukamilisha kwa wakati, na kwamba nafasi waliyonayo ni sawa na Air Bus yaani mwaka 2023.
Dk. Chamriho amesema wakazidi kumshawishi kwamba Boeing wataiuzia Tanzania ndege zilizokataliwa za ‘Terrible Teens’.
“Waliniambia kutorishwa kwao na mchakato, lakini wakasema lolote linaweza kutokea kwa nchi za Kiafrika…nikawauliza mnamaanisha nini? Kwamba nimepokea rushwa? Wakasema inawezekana, nikawataka waondoke ofisini kwangu, maana kwangu hiyo ilikuwa ni dharau kubwa,” amesema Dk. Chamriho.
Mbali na ajenda hiyo, wakamwambia hapakuwa na ushindani wa wazi, na kwamba Tanzania imekuwa ikipokea misaada kutoka EU na hivyo watakwenda kuishtaki huko na katika Benki ya Dunia.
JAMHURI limewasiliana na Hadi Akoum kwa barua pepe ili kuthibitisha baadhi ya tuhuma zao, mpaka tunakwenda mtamboni hakuwa amejibu.

Masuala muhimu katika mkataba
a) Dhamana: Kuna dhamana ya uwezo wa ndege (aircraft performance), kuna dhamana ya aina ya ndege iliyochaguliwa (aircraft model applicability), kuna dhamana ya mwonekano na vifaa/nakshi vilivyochaguliwa kuwekwa ndani ya ndege.
b)  Bei ya ndege: Bei ya mwisho ya ununuzi wa ndege inatokana na bei iliyotolewa kampuni (listed price), na ukitoa punguzo (concessions).
C) Bei ya kampuni kwa jumla inahusisha bei ya umbo la ndege (airframe), bei ya injini, bei ya vitu vya nyongeza vinavyochaguliwa na mnunuzi (optional features), bei ya mifumo ya burudani ndani ya ndege (inflight entertainment system), na punguzo.
Mengine ni punguzo litokanalo na majadiliano (Basic credit memorandum), punguzo la kimkakati (Strategic relationship memorandum), na punguzo la kumwezesha mteja kukidhi mahitaji ya utumiaji wa ndege (Goods and services memorandum).
Katika mazungumzo yao walikuja na hoja kwamba walikuwa na mkataba na Air Tanzania (ATCL) pamoja na Senangol ya China, ambayo iliingia mkataba na ATCL mwaka 2012, huku wakisisitiza kwamba walishachukua fedha ya kiasi cha Dola za Marekani Milioni 2.5, (Zaidi ya Sh Bilioni 5) kama sehemu ya mkataba wao na washirika hao wawili.
Dk. Chamuriho amesema, aliwajibu kwamba sehemu ya mkataba huo hauna uhusiano na ununuzi wa ndege mpya aina ya Boeing 787-800 Dreamliner, isipokuwa hiyo ilikuwa inanunuliwa na Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA).

 Terrible Teens ni nini?
 Terrible Teen ni ndege za mwanzo Aina ya dreamliner 787 zilizotengenezwa kati ya miaka 6-7 iliyopita. Ndege iliyonunuliwa ina uzito kidogo ukilinganisha na dreamliner za zamani, za sasa 787 zina uzito wa tani 4-6 ukilinganisha na dreamliner za mwanzo
Kutokana na kufanyiwa marekebisho ya mara kwa mara, ndege hizo zilizidi uzito kwa tani 3.2 ikilinganisha na uzito uliotakiwa. Kutokana na kuongezeka uzito ndege hizo zikapunguza hata uwezo wake. Ina uwezo wa kwenda umbali wa Nautical Mile 5,900, hiyo ina maana inaweza kufika Guangzhou China ikiwa imejaza abiria na na mzigo wa tani 5 tu.
Kutokana na hili makampuni yaliotaka order za mwanzo kama All Nippon, Maroc na mengineyo yaligoma kuchukua ndege hizo kutokana na kutengeneza hasara katika safari kama wangeamua kuzitumia.
 Terrible Teen zilizokosa soko, ni pamoja na L10, L12, L13, L14, L15, L16, L17, L18, L19, L22. Terrible Teens line namba 11 inatumiwa na Boeing business jet, namba 12 Ethiopia airways wameonyesha nia kuichukua, terrible teens line namba 4 na namba 5 zinatumiwa na boeing kama ndege za majaribio.
Mwezi April, mwaka huu, Mkurugenzi Mtendaji wa ATCL, Ladislaus Matindi, alinukuliwa akisema shirika lake limefanikiwa kukusanya Sh Bilioni 9 kwa Miezi minne tu kwa kutumia ndege mbili za Bombardier.
Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL) ilianzishwa mwezi Novemba 2002 baada ya Serikali kubinafsisha lililokuwa Shirika la Ndege la Tanzania (Air Tanzania Corporation, ATC).
Ujio wa ndege hizo mbili za ATCL, umeweza kupunguza ukiritimba katika usafiri wa anga kwa safari za ndani. Mwanzo kulikuwa na mashirika mawili tu yaliyokuwa yakitoa huduma hiyo ya usafiri wa anga.

By Jamhuri