Marekani imejitoa katika baraza la haki za binaadamu la Umoja wa Mataifa na kulitaja kuwa na ‘unafiki wa kisiasa na lenye upendeleo’.

“Taasisi hiyo ya “unafiki na upendeleo inakejeli haki za binaadamu”, amesema mjumbe wa Marekani katika Umoja huo Nikki Haley.

Bi Haley mwaka jana alilishutumu baraza hilo kwa kuwa na “upendeleo mkali dhidi ya Israel” na kusema Marekani inatafakari uwanachama wake.

Baraza hilo lililoundwa mnamo 2006, lililo na makao yake Geneva limeshutumiwa kwa kuruhusu mataifa yenye rekodi yakutiliwa shaka ya haki za binaadamu kuwa wanachama.

Lakini wanaharakati wanasema hatua hiyo ya Marekani huenda ikaathiri jitihada za kuangalia na kushughulikia ukiukaji wa haki za binaadamu kote duniani.

Bi Haley alitangaza nia ya Marekani kujitoa katika baraza hilo katika mkutano wa pamoja wa waandishi habari kiwa na waziri wa mambo ya nje Mike Pompeo, aliyelitaja baraza hilo kuwa “mteteaji duni wa haki za binaadamu”.

Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa António Guterres, katika taarifa iliyotolewa kupitia msemaji wake, amejibu kwa kusema ange ‘pendelea zaidi’ kwa Marekani kusalia katika baraza hilo.

Kamishna wa haki za binaadamu katika Umoja wa mataifa Zeid Ra’ad Al Hussein, ameitaja hatua hiyo ya ‘kusikitisha’ na habari ya kushangaza mno”. Israel, kwa upande wake imepongeza hatua hiyo.

By Jamhuri