Azma ya Rais John Pombe Magufuli kuelekea nchi ya viwanda huenda isitimie kutokana na genge ya walanguzi kutoka nje ya nchi kuikosesha Serikali mapato zaidi ya bilioni 25, uchunguzi wa JAMHURI umebaini.

JAMHURI imebaini ufisadi wa kutisha unaodidimiza sekata ya ngozi nchini, kutokana na uwepo wa mtandao wa wafanyabiashara walanguzi wa ngozi ghafi kuzisafirisha nje ya nchi kinyume cha sheria.

Katika nyaraka ambazo JAMHURI imeziona, kampuni ya SAK International kutoka Pakistan na washirika wake, imeiingizia Serikali hasara ya mabilioni ya shilingi kutokana na kujihusisha na biashara hiyo.

Juni 9, mwaka jana, raia watatu wa familia moja kutoka Pakistan, Tauseef Mohmood, Asim Mahmood na Mahmood Sadiq walikamatwa na TRA kwa ukwepaji kodi na kuzuia makontena 65 ambapo walikiri kuyatambua makontena 15 kati ya hayo na kutozwa faini ya Sh milioni 400.

Walishikiliwa Kituo cha Polisi cha Kati (Central Police) jijini Dar es Salaam, kisha wakapewa dhamana baada ya TRA kushikilia hati zao za kusafiria na kufunga kiwanda chao cha ngozi cha Arusha hadi uchunguzi wa TRA utakapokamilika.

Timu ya uchunguzi kutoka TRA ilibaini ukwepaji mkubwa wa kodi na kwamba makontena waliyoyakana ni mali ya kampuni hiyo, hivyo iliwatumia hati ya madai (Demand Notice) ya Sh bilioni 2.9 ambazo hawakuzilipa wakakimbia nchi.

Kampuni hiyo inayomilikiwa na raia wa Pakstan, inaelezwa kuwa karibu na mmoja wa wafanyabiashara wakubwa nchini (jina linahifadhiwa), ambaye amekuwa akiikingia kifua pindi wamiliki wake wanapokamatwa na vyombo vya dola.

Julai mwaka jana TRA walilazimika kushikilia hati zao za kusafiria, lakini waliamua kubuni mbinu za kutoroka nchini kwa kutumia hati nyingine baada ya kwenda kuripoti kituo cha polisi kuwa wameibwa begi lililokuwa na nyaraka muhimu ikiwa ni pamoja na hati hizo.

“Unajua tena mgeni akienda polisi ni rahisi kuaminiwa. Walipewa Police Loss Report ambayo waliitumia katika ofisi za ubalozi wa Pakistan na kupewa hati nyingine za kusafiria wakati ukweli ni kwamba hati zao zilizuiwa na TRA,” anasema mtoa taarifa.

Julai 21, mwaka jana, katika juhudi zao kutaka kutoroka nchini, walimtanguliza Mahmood Sadiq Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere kununua tiketi kwa kutumia hati mpya, lakini kwa msaada wa raia wema TRA walifahamishwa mara moja na kwa kushirikiana na Uhamiaji Mahamood alikamatwa ila ndugu zake waliondoka kwa kutumia ndege ya kukodi mpaka jijini Arusha.

Tauseef Mohmood na Asim Mahmood walikamatwa wakiwa mkoani Arusha na kusafirishwa mpaka jijini Dar es Salaam, ambapo kwa mashangao saa saa tano usiku waliachiwa.

Baada ya kukwama kutoroka nchini, walibadilisha mbinu za kusafirisha ngozi ghafi kwa kushirikiana na baadhi ya watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ambao walisajili kampuni iliyotumika kufanya ujanja huo.

Kwa mujibu wa nyaraka ambazo JAMHURI imeziona, Kampuni ya Chinyange Argo Allied Enterprises ya jijini Dar es Salaam, inayomilikiwa na Jonathan Mwita Maswi yenye namba ya usajili 106459 na kupewa namba ya mlipa kodi 124-637-856 Julai mwaka jana ilihusika na usafirishaji wa ngozi ghafi kwa lengo ya kuzitoroshea Mombasa, Kenya kwa kutumia malori mawili yenye usajili namba T771 BMN na T513 BHW.

Hati za usafirishaji wa ngozi hizo zilibainisha kuwa ni mali ya kiwanda cha Himo Tannery kilichopo Moshi lakini kampuni hiyo ilikana kuhusika na mzigo huo.

“Dereva wa kwanza akakosea njia akapeleka mzigo moja kwa moja hadi kiwanda cha Himo Tannery kwa mshangao wa mwenye kiwanda ambaye hakuwa na taarifa za mizigo hiyo na mara moja kuwataarifu TRA ambao waliizuia mizigo hiyo ambayo inashikiliwa na vyombo vya dola,” anasema mmoja wa wafanyakazi wa kiwanda hicho.

Akizungumza na JAMHURI, Jonathan Mwita amesema yeye ndiye mmiliki wa kampuni ya Chinyange na kwamba mpaka sasa kampuni yake imepata hasara kutokana na wafanyabiashara wa ngozi viwandani kutonunua ngozi, na kwamba mzigo unaoelezwa kukamatwa Himo ulipelekwa kuuzwa katika kiwanda hicho.

“Kuuza ngozi ni lazima kutumia akili. Ukijulikana unatoka kwenye kampuni yangu haununuliwi maana kuna genge la wafanyabiashara waliamua kutupiga vita kutokana na kuwaeleza ukweli kwamba wanahujumu biashara hii.

“Katika kikao tulichofanya na Waziri mjini Dodoma, tulisema ukweli, kwani yupo Mzungu anayesimamia kiwanda cha (jina limehifadhiwa) cha Morogoro pamoja na hicho cha Moshi kinachomilikiwa na (jina linahifadhiwa) ni watu hatari,” anasema Mwita.

Hata hivyo, anabainisha kuwa kampuni ya SAK International ndiyo kampuni inayofanya biashara ya ngozi nchini, na imekuwa ikifanya vizuri sokoni, hayo maneno yanayosemwa ni uongo na uzushi wa hali ya juu kuhusu kampuni hiyo.

“Hao SAK unaowasema wapo nchini na wanaendelea na biashara, ndiyo wanunuzi wakubwa wa ngozi. Wengine wamekuwa ni wababaishaji wenye mtandao wa kuangamiza sekta ya ngozi. Najua mpaka Waziri wa Biashara analijua hili maana tulimweleza ukweli,” anasema.

Akizungumzia kukamatwa kwa mzigo wa kampuni hiyo mkoani Kilimanjaro, alikiri mzigo kuwa mali ya kampuni yake na kwamba ulikuwa unapelekwa kiwandani Himo na kwamba ulipofika na kugundulika kuwa umetokea kwa Chinyange ukakataliwa hivyo amepata hasara ya Sh bilion 1.2 kutokana na ngozi hizo kuendelea kuwapo kiwandani bila kununuliwa kwa kipindi kirefu.

“Sijakamatwa na TRA kuhusu huo mzigo. Wangekamata hilo gari kwanini waliache kiwandani wasiondoke nalo? Nenda hata sasa hivi utalikuta pale kiwandani. Ngozi zinazidi kuoza tu, na mimi nimeamua kuziacha zioze kama zile zilizopo kwenye makontena bandarini,” amesema Mwita.

Baadhi ya nyaraka za kusafirishia bidhaa (bill of lading) za kampuni hiyo, ziliandaliwa nchini Pakistan, huku inapopakiwa mzigo (port of loading) ikiwa ni Dar es Salaam. Kampuni inayosafirisha mzigo huo imejitanabahisha kuwa ni mgahawa wa kahawa uliopo eneo la Fire jijini Dar es Salaam. 

Pamoja na sheria kuwataka wasafirishaji wa bidhaa za ngozi kuwa na kiwanda nchini, jambo hilo halikufanywa na kampuni hiyo zaidi ya malipo yake kuandaliwa katika nchi za Falme za Kiarabu na malipo kufanyika Dubai.

JAMHURI imefanya mawasiliano na mtu wa karibu na wafanyabiashara hao, ambaye amesema bado hawajarejea nchini kwa madai ya kuwa likizo ya mwisho wa mwaka baada ya kufanya sherehe kubwa eneo la City Mall walipoaga wenzao wakitamba kuiweka Serikali mfukoni.

Katibu wa Chama cha Wasindikaji wa Ngozi Tanzania (TTA), Joram Wakari, ameiambia JAMHURI kuwa sekta hiyo hukumbwa na changamoto ya ulanguzi kutoka kwa wafanyabiashara wa magendo, ambao hukwepa kodi na kutorosha ngozi ghafi kupitia Bandari ya Dar es Salaam.

Amesema Kampuni ya SAK ni miongoni mwa kampuni zilizoitia hasara Serikali kwa ukwepaji kodi, ambapo imekuwa ikisafirisha makontena ya ngozi bila kulipiwa ushuru unaohitajika.

“Serikali imeweka sheria. Ukisafirisha ngozi ghafi unatakiwa kulipa asilimia 80 ya thamani ya ngozi unayosafirisha, na kama zimesindikwa unalipia asilimia 10. Lakini SAK wamekuwa wakifanya magendo miaka yote, wamesafirisha makontena na makontena ya ngozi ghafi kupitia bandari hadi walipogunduliwa na TRA kisha kutozwa faini. Suala la kampuni hii kufanya magendo siyo siri hata kidogo,” anasema Wakari.

Kuhusu kauli iliyotolewa na Mwita kuwa SAK ndiyo kampuni inayofanya biashara ya ngozi nchini, amesema hizo ni lugha za mitaani na kwamba siku zote Mwita ndiye aliyekuwa mshirika wa karibu na SAK katika kuhujumu biashara hiyo.

“Afuate sheria na taratibu zilizowekwa, aache ujanja ujanja. Huyo alikuwa akishirikiana na watu wa magendo siku zote,” anasema Wakari.

Mkurugenzi wa Kiwanda cha Ngozi cha Morogoro, ACE Leather Tanzania Ltd Tannery, Onorato Garavaglia, amesema kumekuwapo upotoshwaji mkubwa kuhusiana na umiliki wa kiwanda hicho na kukihusisha na Rostam Aziz. Anasema yeye Onorato ndiye mmiliki halali wa kiwanda hicho na si Rostam.

“Nimekuja nchini kuwekeza siyo kufanya siasa, kiwanda ni mali yangu… sema mimi ni mpangaji. Na huyo anayesema hivyo ni mshirika mkubwa wa SAK katika ulanguzi wa ngozi na ukwepaji mkubwa wa kodi nchini. TRA wanajua jinsi Chinyange walivyoshirikiana na SAK katika kuikosesha Serikali mabilioni ya shilingi kwa kutorosha makontena ya ngozi ghafi bila kulipia ushuru, mwambie akwambie vizuri kuhusu ngozi alizokuwa akizitorosha kuelekea Mombasa zilizokamatiwa mkoani Kilimanjaro,” anasema Onorato.

Pia anaeleza kuwa yeye ndiye Mwenyekiti wa TTA nchini, na amekuwa akishirikiana na Serikali katika kupambana na ukwepaji kodi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu, ambao wengine wamekuwa wakishirikiana na baadhi ya watendaji wa Wizara ya Mifugo.

Kwa upande wake, mmiliki wa kiwanda cha Himo Tannery, Sabas Woiso, ameiambia JAMHURI kuwa magari hayo mawili yalikamatwa na askari mkoani Kilimanjaro baada ya kuonekana yakielekea mpakani na kwamba walipokamatwa walidai kuwa mzigo huo ni mali ya Himo Tannery, jambo ambalo si kweli.

“Hiyo ngozi ilitoka Dar ikiwa na nyaraka zinazoonesha kuwa zinakuja kwangu, wakasindikiza magari mpaka kiwandani kwangu. Mimi nikawauliza mbona sifahamu? Na mzigo siyo wangu. Wakatokea vijana wawili wa Kikenya wakaongea nami kuwa wamelazimika kusingizia kuwa ni mzigo wangu, lakini ukweli ni kwamba wameuziwa na Chinyange na kwamba wanaupeleka Kenya. Nilipowauliza kwanini wananisingizia wakasema ni njaa tu,” anasema Sabas.

Amesema alilazimika kuwaeleza polisi ukweli kuhusiana na mzigo huo ambapo magari hayo yalitakiwa kutoondoka kiwandani hapo, lakini gari moja liliondolewa usiku likabaki moja ambalo baada ya siku 10 baadhi ya maafisa wa TRA waliomba ngozi hizo zishushwe kwenye gari kuliepusha kuharibika kutokana na ngozi kuanza kuoza, ambapo baada ya kushushwa gari hilo nalo liliondolewa kinyemela ngozi zikatelekezwa kiwandani hapo.

“Ni juzi tu nimewaomba TRA tuzifukie hizo ngozi maana hali yake si nzuri, na hata maturubai yangu tuliyoyatumia kuzifunika nayo yanaharibika tu. Ila kama ni masuala ya magendo kampuni hii ya Chinyange imekuwa ikijihusisha kwa muda mrefu kwa kufoji nyaraka kuwa mzigo unakuja kiwandani kwangu. Nimeshawafahamisha TRA na wanachama wenzangu katika umoja wetu kwani nimekuwa nikipata taarifa kuwa kuna mzigo unakuja kwangu, lakini siuoni na sina taarifa nao,” anasema Sabas.

Kuhusu umiliki wa kiwanda hicho kuwa mali ya Basil Mramba, anasema si mara ya kwanza kwa Mwita kuyasema hayo ila anahitaji ampatie ushahidi kuhusu madai hayo kwani ni mali yake na ametumia nguvu kubwa kufika hapo alipo.

A

zma ya Rais John Pombe Magufuli kuelekea nchi ya viwanda huenda isitimie kutokana na genge ya walanguzi kutoka nje ya nchi kuikosesha Serikali mapato zaidi ya bilioni 25, uchunguzi wa JAMHURI umebaini.

JAMHURI imebaini ufisadi wa kutisha unaodidimiza sekata ya ngozi nchini, kutokana na uwepo wa mtandao wa wafanyabiashara walanguzi wa ngozi ghafi kuzisafirisha nje ya nchi kinyume cha sheria.

Katika nyaraka ambazo JAMHURI imeziona, kampuni ya SAK International kutoka Pakistan na washirika wake, imeiingizia Serikali hasara ya mabilioni ya shilingi kutokana na kujihusisha na biashara hiyo.

Juni 9, mwaka jana, raia watatu wa familia moja kutoka Pakistan, Tauseef Mohmood, Asim Mahmood na Mahmood Sadiq walikamatwa na TRA kwa ukwepaji kodi na kuzuia makontena 65 ambapo walikiri kuyatambua makontena 15 kati ya hayo na kutozwa faini ya Sh milioni 400.

Walishikiliwa Kituo cha Polisi cha Kati (Central Police) jijini Dar es Salaam, kisha wakapewa dhamana baada ya TRA kushikilia hati zao za kusafiria na kufunga kiwanda chao cha ngozi cha Arusha hadi uchunguzi wa TRA utakapokamilika.

Timu ya uchunguzi kutoka TRA ilibaini ukwepaji mkubwa wa kodi na kwamba makontena waliyoyakana ni mali ya kampuni hiyo, hivyo iliwatumia hati ya madai (Demand Notice) ya Sh bilioni 2.9 ambazo hawakuzilipa wakakimbia nchi.

Kampuni hiyo inayomilikiwa na raia wa Pakstan, inaelezwa kuwa karibu na mmoja wa wafanyabiashara wakubwa nchini (jina linahifadhiwa), ambaye amekuwa akiikingia kifua pindi wamiliki wake wanapokamatwa na vyombo vya dola.

Julai mwaka jana TRA walilazimika kushikilia hati zao za kusafiria, lakini waliamua kubuni mbinu za kutoroka nchini kwa kutumia hati nyingine baada ya kwenda kuripoti kituo cha polisi kuwa wameibwa begi lililokuwa na nyaraka muhimu ikiwa ni pamoja na hati hizo.

“Unajua tena mgeni akienda polisi ni rahisi kuaminiwa. Walipewa Police Loss Report ambayo waliitumia katika ofisi za ubalozi wa Pakistan na kupewa hati nyingine za kusafiria wakati ukweli ni kwamba hati zao zilizuiwa na TRA,” anasema mtoa taarifa.

Julai 21, mwaka jana, katika juhudi zao kutaka kutoroka nchini, walimtanguliza Mahmood Sadiq Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere kununua tiketi kwa kutumia hati mpya, lakini kwa msaada wa raia wema TRA walifahamishwa mara moja na kwa kushirikiana na Uhamiaji Mahamood alikamatwa ila ndugu zake waliondoka kwa kutumia ndege ya kukodi mpaka jijini Arusha.

Tauseef Mohmood na Asim Mahmood walikamatwa wakiwa mkoani Arusha na kusafirishwa mpaka jijini Dar es Salaam, ambapo kwa mashangao saa saa tano usiku waliachiwa.

Baada ya kukwama kutoroka nchini, walibadilisha mbinu za kusafirisha ngozi ghafi kwa kushirikiana na baadhi ya watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ambao walisajili kampuni iliyotumika kufanya ujanja huo.

Kwa mujibu wa nyaraka ambazo JAMHURI imeziona, Kampuni ya Chinyange Argo Allied Enterprises ya jijini Dar es Salaam, inayomilikiwa na Jonathan Mwita Maswi yenye namba ya usajili 106459 na kupewa namba ya mlipa kodi 124-637-856 Julai mwaka jana ilihusika na usafirishaji wa ngozi ghafi kwa lengo ya kuzitoroshea Mombasa, Kenya kwa kutumia malori mawili yenye usajili namba T771 BMN na T513 BHW.

Hati za usafirishaji wa ngozi hizo zilibainisha kuwa ni mali ya kiwanda cha Himo Tannery kilichopo Moshi lakini kampuni hiyo ilikana kuhusika na mzigo huo.

“Dereva wa kwanza akakosea njia akapeleka mzigo moja kwa moja hadi kiwanda cha Himo Tannery kwa mshangao wa mwenye kiwanda ambaye hakuwa na taarifa za mizigo hiyo na mara moja kuwataarifu TRA ambao waliizuia mizigo hiyo ambayo inashikiliwa na vyombo vya dola,” anasema mmoja wa wafanyakazi wa kiwanda hicho.

Akizungumza na JAMHURI, Jonathan Mwita amesema yeye ndiye mmiliki wa kampuni ya Chinyange na kwamba mpaka sasa kampuni yake imepata hasara kutokana na wafanyabiashara wa ngozi viwandani kutonunua ngozi, na kwamba mzigo unaoelezwa kukamatwa Himo ulipelekwa kuuzwa katika kiwanda hicho.

“Kuuza ngozi ni lazima kutumia akili. Ukijulikana unatoka kwenye kampuni yangu haununuliwi maana kuna genge la wafanyabiashara waliamua kutupiga vita kutokana na kuwaeleza ukweli kwamba wanahujumu biashara hii.

“Katika kikao tulichofanya na Waziri mjini Dodoma, tulisema ukweli, kwani yupo Mzungu anayesimamia kiwanda cha (jina limehifadhiwa) cha Morogoro pamoja na hicho cha Moshi kinachomilikiwa na (jina linahifadhiwa) ni watu hatari,” anasema Mwita.

Hata hivyo, anabainisha kuwa kampuni ya SAK International ndiyo kampuni inayofanya biashara ya ngozi nchini, na imekuwa ikifanya vizuri sokoni, hayo maneno yanayosemwa ni uongo na uzushi wa hali ya juu kuhusu kampuni hiyo.

“Hao SAK unaowasema wapo nchini na wanaendelea na biashara, ndiyo wanunuzi wakubwa wa ngozi. Wengine wamekuwa ni wababaishaji wenye mtandao wa kuangamiza sekta ya ngozi. Najua mpaka Waziri wa Biashara analijua hili maana tulimweleza ukweli,” anasema.

Akizungumzia kukamatwa kwa mzigo wa kampuni hiyo mkoani Kilimanjaro, alikiri mzigo kuwa mali ya kampuni yake na kwamba ulikuwa unapelekwa kiwandani Himo na kwamba ulipofika na kugundulika kuwa umetokea kwa Chinyange ukakataliwa hivyo amepata hasara ya Sh bilion 1.2 kutokana na ngozi hizo kuendelea kuwapo kiwandani bila kununuliwa kwa kipindi kirefu.

“Sijakamatwa na TRA kuhusu huo mzigo. Wangekamata hilo gari kwanini waliache kiwandani wasiondoke nalo? Nenda hata sasa hivi utalikuta pale kiwandani. Ngozi zinazidi kuoza tu, na mimi nimeamua kuziacha zioze kama zile zilizopo kwenye makontena bandarini,” amesema Mwita.

Baadhi ya nyaraka za kusafirishia bidhaa (bill of lading) za kampuni hiyo, ziliandaliwa nchini Pakistan, huku inapopakiwa mzigo (port of loading) ikiwa ni Dar es Salaam. Kampuni inayosafirisha mzigo huo imejitanabahisha kuwa ni mgahawa wa kahawa uliopo eneo la Fire jijini Dar es Salaam. 

Pamoja na sheria kuwataka wasafirishaji wa bidhaa za ngozi kuwa na kiwanda nchini, jambo hilo halikufanywa na kampuni hiyo zaidi ya malipo yake kuandaliwa katika nchi za Falme za Kiarabu na malipo kufanyika Dubai.

JAMHURI imefanya mawasiliano na mtu wa karibu na wafanyabiashara hao, ambaye amesema bado hawajarejea nchini kwa madai ya kuwa likizo ya mwisho wa mwaka baada ya kufanya sherehe kubwa eneo la City Mall walipoaga wenzao wakitamba kuiweka Serikali mfukoni.

Katibu wa Chama cha Wasindikaji wa Ngozi Tanzania (TTA), Joram Wakari, ameiambia JAMHURI kuwa sekta hiyo hukumbwa na changamoto ya ulanguzi kutoka kwa wafanyabiashara wa magendo, ambao hukwepa kodi na kutorosha ngozi ghafi kupitia Bandari ya Dar es Salaam.

Amesema Kampuni ya SAK ni miongoni mwa kampuni zilizoitia hasara Serikali kwa ukwepaji kodi, ambapo imekuwa ikisafirisha makontena ya ngozi bila kulipiwa ushuru unaohitajika.

“Serikali imeweka sheria. Ukisafirisha ngozi ghafi unatakiwa kulipa asilimia 80 ya thamani ya ngozi unayosafirisha, na kama zimesindikwa unalipia asilimia 10. Lakini SAK wamekuwa wakifanya magendo miaka yote, wamesafirisha makontena na makontena ya ngozi ghafi kupitia bandari hadi walipogunduliwa na TRA kisha kutozwa faini. Suala la kampuni hii kufanya magendo siyo siri hata kidogo,” anasema Wakari.

Kuhusu kauli iliyotolewa na Mwita kuwa SAK ndiyo kampuni inayofanya biashara ya ngozi nchini, amesema hizo ni lugha za mitaani na kwamba siku zote Mwita ndiye aliyekuwa mshirika wa karibu na SAK katika kuhujumu biashara hiyo.

“Afuate sheria na taratibu zilizowekwa, aache ujanja ujanja. Huyo alikuwa akishirikiana na watu wa magendo siku zote,” anasema Wakari.

Mkurugenzi wa Kiwanda cha Ngozi cha Morogoro, ACE Leather Tanzania Ltd Tannery, Onorato Garavaglia, amesema kumekuwapo upotoshwaji mkubwa kuhusiana na umiliki wa kiwanda hicho na kukihusisha na Rostam Aziz. Anasema yeye Onorato ndiye mmiliki halali wa kiwanda hicho na si Rostam.

“Nimekuja nchini kuwekeza siyo kufanya siasa, kiwanda ni mali yangu… sema mimi ni mpangaji. Na huyo anayesema hivyo ni mshirika mkubwa wa SAK katika ulanguzi wa ngozi na ukwepaji mkubwa wa kodi nchini. TRA wanajua jinsi Chinyange walivyoshirikiana na SAK katika kuikosesha Serikali mabilioni ya shilingi kwa kutorosha makontena ya ngozi ghafi bila kulipia ushuru, mwambie akwambie vizuri kuhusu ngozi alizokuwa akizitorosha kuelekea Mombasa zilizokamatiwa mkoani Kilimanjaro,” anasema Onorato.

Pia anaeleza kuwa yeye ndiye Mwenyekiti wa TTA nchini, na amekuwa akishirikiana na Serikali katika kupambana na ukwepaji kodi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu, ambao wengine wamekuwa wakishirikiana na baadhi ya watendaji wa Wizara ya Mifugo.

Kwa upande wake, mmiliki wa kiwanda cha Himo Tannery, Sabas Woiso, ameiambia JAMHURI kuwa magari hayo mawili yalikamatwa na askari mkoani Kilimanjaro baada ya kuonekana yakielekea mpakani na kwamba walipokamatwa walidai kuwa mzigo huo ni mali ya Himo Tannery, jambo ambalo si kweli.

“Hiyo ngozi ilitoka Dar ikiwa na nyaraka zinazoonesha kuwa zinakuja kwangu, wakasindikiza magari mpaka kiwandani kwangu. Mimi nikawauliza mbona sifahamu? Na mzigo siyo wangu. Wakatokea vijana wawili wa Kikenya wakaongea nami kuwa wamelazimika kusingizia kuwa ni mzigo wangu, lakini ukweli ni kwamba wameuziwa na Chinyange na kwamba wanaupeleka Kenya. Nilipowauliza kwanini wananisingizia wakasema ni njaa tu,” anasema Sabas.

Amesema alilazimika kuwaeleza polisi ukweli kuhusiana na mzigo huo ambapo magari hayo yalitakiwa kutoondoka kiwandani hapo, lakini gari moja liliondolewa usiku likabaki moja ambalo baada ya siku 10 baadhi ya maafisa wa TRA waliomba ngozi hizo zishushwe kwenye gari kuliepusha kuharibika kutokana na ngozi kuanza kuoza, ambapo baada ya kushushwa gari hilo nalo liliondolewa kinyemela ngozi zikatelekezwa kiwandani hapo.

“Ni juzi tu nimewaomba TRA tuzifukie hizo ngozi maana hali yake si nzuri, na hata maturubai yangu tuliyoyatumia kuzifunika nayo yanaharibika tu. Ila kama ni masuala ya magendo kampuni hii ya Chinyange imekuwa ikijihusisha kwa muda mrefu kwa kufoji nyaraka kuwa mzigo unakuja kiwandani kwangu. Nimeshawafahamisha TRA na wanachama wenzangu katika umoja wetu kwani nimekuwa nikipata taarifa kuwa kuna mzigo unakuja kwangu, lakini siuoni na sina taarifa nao,” anasema Sabas.

Kuhusu umiliki wa kiwanda hicho kuwa mali ya Basil Mramba, anasema si mara ya kwanza kwa Mwita kuyasema hayo ila anahitaji ampatie ushahidi kuhusu madai hayo kwani ni mali yake na ametumia nguvu kubwa kufika hapo alipo.

By Jamhuri