Zikiwa zimebaki siku 6 kabla ya uchaguzi mdogo wa ubunge Siha na Kinondoni na kata nane kufanyika, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema maandalizi yanaendelea vizuri.

NEC imesema maandalizi hayo ni pamoja na ufumbuzi wa changamoto ndogondogo zinazojitokeza.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhani Kailima amesema hayo baada ya mkutano wa watendaji wa Tume na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kinondoni, Aron Kagurumujuri.

Kailima amesema Tume inafuatilia kwa karibu maandalizi ya uchaguzi huo utakaofanyika Jumamosi Februari 17,2018.

Katika taarifa ya NEC iliyotolewa leo Februari 11,2018 Kailima amepongeza jitihada zinazofanywa na msimamizi wa uchaguzi  na wasaidizi wake katika kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka.

Amewashauri wasimamizi wa uchaguzi kuendelea kukutana na wawakilishi wa vyama vya siasa kwa ajili ya kutoa taarifa katika kila hatua.

Kailima amesema Tume imejipanga kuanza kutoa vipindi vya elimu ya mpiga kura mfululizo hadi siku ya uchaguzi.

Amesema elimu itahusu mada kadhaa zikiwemo haki na wajibu wa mpiga kura, wakala wa vyama vya siasa na msimamizi wa uchaguzi pamoja na taratibu zote za upigaji kura.

By Jamhuri