Na Rahma Khamis – Maelezo Zanzibar     

Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Nassor Ahmed Mazrui amewataka Mawakala wa Maabara ya Serikali kuendelea kuwa waaminifu na waadilifu katika kazi zao za kiuchunguzi wa matatizo ili wananchi waamini majibu yanayotolewa na taasisi hiyo. 

Wito huo ameutoa katika Ukumbi wa Shekh Idriss Abdul-wakil Kikwajuni katika uzinduzi wa maadhimisho ya siku ya Vinasaba Duniani.

Amesema kuwa uaminifu na uadilifu katika kazi za kiuchunguzi ni njia moja wapo inayowafanya wananchi kutokuwa na wasiwasi kwa kupata majibu sahihi na  kuamini kile wanachoambiwai.

Amesema kuwa vinasaba ni huduma muhumu sana katika kuchunguza jambo ama  kwa binadamu au hata katika kilimo ambapo vinasaidia kubainisha tatizo na oweza kutengeneza dawa.

Aidha amefahamisha kuwa watoto wengi wanaozaliwa Zanzibar wanaugua maradhi ya .mifupa  kutokana na ukosefu wa upimaji wa vinasaba kabla ndoa  jambo ambalo ni kikwazo. 

Ameeleza kuwa maadhimisho ya siku ya vinasaba duniani yametangazwa rasmi na Baraza la Seneta la Marekani ambapo baraza hilo limeitaka dunia kuadhimisha siku hiyo kila mwaka.

Aidha ameipongeza Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika kuanzisha siku hiyo ambayo inatoa ufafanuzi wa vinasaba vya afya za wananchi katika mambo mbalimbali.

Katika hatua nyingine Waziri Mazrui amewasisitiza wanafunzi kusoma sana masomo ya Sayansi ili kusaidia Serikali katika kufanya utafiti na kujua vinasaba kupitia makundi mbalimbali ikiwemo kilimo, afya na wanyama.

“Hatuwezi kujenga hospitali na Maabara za kisasa bila ya kuwa na wafanyakazi wenye uwezo wa hali ya juu na wasomi ambao watatusaidia kutatua changamoto zilizopo” alisema Waziri waAfya.

Ameongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inafanya kila jitihada kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora hivyo wataendelea kujenga maabara mbaimbali za kisasa zaidi zitakazosaidia kufanya tafiti za aina zote.

Akitoa salamu za Wakala wa Maabara ya Serikali Mkemia Mkuu wa Serikali Faridi Mzee Mpatani amesema kuwa teknolojia ya vinasaba inasaidia kutatua matatizo mengi yanayotokea katika jamii na kutafutiwa ufumbuzi kwa mujibu wa sheria.

Mkemia Mkuu huyo amefahamisha kuwa Serikali imejitahidi kununua vifaa tiba vya kubaini vinasaba ili kutatua changamoto zinazojitokeza hivyo ameiomba jamii kuendelea kuitumia maabara hiyo ili kufanikisha lengo la kuanzishwa kwa teknolojia hiyo.

Hata hivyo amebainisha kuwa jumla ya kesi 155 za udhalilishaji zimegundulika na kupatiwa majibu sahihi kupitia maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali

Akitoa maelezo kuhusu DNA Mkurugenzi Kinga Wizara ya Afya   Dkt

Wakitoa michango kuhusu DNA wadau wa vinasaba Zanzibar wamewataka wananchi kutunza ushahidi  pamoja na kuwataka madaktari kuendelea kutumia vinasaba kwa wahalifu ili kupata ushahidi kamili na kuweza kuwakamata.

 Aidha wamesema kuwa changamoto inayowakumba akina mama ni kuharibika kwa mimba kutokana na kutokukubaliana na vinasaba baina ya mume na mke pamoja na kuwepo na vinasaba ambavyo vinasababisha damu kushuka na kupelekea kutopata ujauzito hivyo ni vyema kufahamu elimu ya vinasaba kabla ya ndoa.

Wadau hao wameongeza kuwa teknolojia ya vinasaba pia imetoa mchango mkubwa hasa katika Sekta ya kilimo na kupelekea upatikanaji wa chakula bora nchini.

Pamoja na hayo wamefafanua kuwa  kuwa  maradhi mengi yasiyoambukiza yanatokana na urithi hasa  saratani ya matiti na shingo ya kizazi ni vyema jamii ikapata ulelewa kwa familia kutokana na urithi wa maradhi hayo.

Maadhimisho ya siku ya vinasaba hufanyika kila ifikapo Aprili 25 duniani ambapo kwa Zanzibar ni mara ya kwanza kuadhimisha siku hiyo na ujumbe wa mwaka huu “Teknolojia ya matumizi ya vinasaba ni nguzo kuu ya kutatua changamoto karika jamii juu ya uhalifu, udhalilishaji ,magonjwa na maafa”.

By Jamhuri