Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia,Pwani

WAKALA wa huduma za misitu Tanzania (TFS) imemkabidhi Mkuu wa mkoa wa Pwani kiasi cha sh.milioni 20 kwa ajili ya waathirika wa mafuriko Wilayani Rufiji na Kibiti.

Aidha imetoa eneo Chumbi Rufiji lenye viwanja 600 ili kuhamisha wale wanaoishi mabondeni wawe eneo salama.

Akipokea Mfano wa hundi ya msaada huo ,Mkuu wa mkoa wa Pwani alhaj Abubakar Kunenge aliishukuru TFS kwa msaada huo.

“Muhoro bado kuna changamoto ambayo bado sio salama lakini tunashukuru eneo mlilotupatia ili wananchi waweze kuhamia”

Kunenge alifafanua, msaada huo ni kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan ambae ndie mwana mazingira namba moja Duniani kwani amefanya jitihada kubwa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

“Pia tunashukuru katika jitihada za mazingira mmetupatia miche inayoendana na hali halisi ya mazingira yetu na kutoa elimu kuhakikisha tunatunza mazingira na kuondokana na nishati chafu ili kutumia nishati mbadala na safi” alieleza Kunenge.

Akikabidhi hundi hiyo ,Johari Kachwamba, Meneja Uhusiano kutoka TFS alitoa pole kwa waathirika wa mafuriko Rufiji na Kibiti.

“Rufiji na sisi tuna misitu kumi yenye zaidi ya hekta 32,000 ,ni wanamisitu wenzetu ,tunatoa pole, Kamishna wa Hifadhi wa TFS ametoa milioni 20 ” amesema.

By Jamhuri