Uongozi wa Klabu ya Azam FC yenye makazi yake huko Chamazi jijini Dar es salaam, umethibitisha kuwa umeingia makubaliano ya usajili na mshambuliaji Donald Ngoma, kwa ajili ya msimu ujao 2018/2019.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na klabu hiyo mapema leo, imeeleza kwamba muda wowote kuanzia sasa Azam FC inatarajia kumpeleka mchezaji huyo katika Hospitali ya Vincent Pallotti jijini Cape Town, Afrika Kusini kwa ajili ya kumfanyia vipimo vya afya ili kuona ni kwa kiasi gani majeraha yaliyokuwa yakimsumbua yamepona.

Azam FC inaamini ya kuwa ujio wa nyota huyo kutoka nchini Zimbabwe aliyewahi kuchezea FC Platinum ya huko kabla ya kuhamia Yanga, ni sehemu tu ya mikakati ya benchi la ufundi na uongozi katika kuboresha kikosi kwenye eneo la ushambuliaji kuelekea msimu ujao.

Pia uongozi wa Azam FC unaamini kuwa Ngoma atakuwa ni miongoni mwa nyota wapya wa timu hiyo watakaoonekana kwenye Kombe la Kagame (CECAFA Kagame Cup) linalotarajia kuanza hivi karibuni tukiwa kama mabingwa watetezi wa michuano hiyo.

Tayari mchezaji huyo ameandaliwa jezi namba 11 iliyokuwa ikitumiwa na mshambuliaji Yahaya Mohammed, aliyerejea Aduana Stars ya nchini kwao Ghana.

By Jamhuri