Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, REX TILLERSON

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Rex Tillerson, anatarajiwa kufanya ziara ya siku nane barani Afrika kuanzia Jumanne wiki ijayo. Hii itakuwa ziara yake ya kwanza kwenye bara hilo kama waziri.

Taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya nje ya Marekani Alhamisi ilisema kuwa Tillerson atazuru Kenya, Ethiopia, Djibouti, Chad na Nigeria, kwenye safari ambayo itakamilika tarehe 13 mwezi huu.

Tangu rais Donald Trump kuingia madarakani, wachambuzi wa masuala ya kisiasa wamekuwa wakieleza kwamba hajaonyesha shauku kubwa juu ya masuala ya bara hilo.

Mwishoni mwa mwezi wa Januari mwaka huu, Trump aliibua utata na hisia mseto aliporipotiwa kutumia lugha chafu kwa nchi za Afrika pamoja na Haiti.

Lakini katika barua aliyowatumia viongozi wa Kiafrika, Trump alisema ana heshima kubwa kwa watu wa Afrika na kwamba waziri wa mambo ya nje Rex Tillerson atafanya ziara ndefu barani humo mwezi Machi.

Alhamisi, msemaji wa wizara ya mambo ya nje wa Marekani Heather Nauert alisema ziara ya Tillerson kwa ujumla itaangazia masuala yafuatayo:

-Kutafuta ushirikiano katika kupambana na ugaidi

-uongozi bora

-Uimarishaji wa amani na usalama

-Kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji.

 

By Jamhuri