Burundi inafanya kura ya maamuzi hapo inayopania kuongeza muhula wa rais kutoka miaka tano hadi saba.

Marekebisho hayo ya katiba yakiidhinishwa na wananchi huenda rais Pierre Nkurunziza akaongoza taifa hilo hadi mwaka wa 2034.

Lakini kampeni hizo zimechafuliwa na tishio za upinzani kususia kura hiyo ya maamuzi huo na pia madai kwamba serikali imekuwa ikiwatisha wafuasi wa upinzani.

Umoja wa mataifa unahofia huenda ghasia zikazuka baada ya mauaji ya watu 26 hivi majuzi.

Wiki jana, washambuliaji ambao serikali imewataja kuwa magaidi, walivamia jiji la Chibitoke, wakafanya mauaji ya kiholela na kuaminika kutorokea taifa jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Serikali inaamini kuwa walikuwa wanajaribu kukomesha kura ya maoni kwa kutia watu woga na kuvuruga amani.

Hali hii ikiendelea huenda warundi wengine wasipige kura.

Ni kura tata yenye matokeo makubwa.

Rais Pierre Nkurunziza amekuwa akipiga kampeni nchini humo, akiwarai wananchi kuwa katiba hii mpya ni ya manufaa kwao.

Lakini wanaopinga wanamwona rais kama aliye na tamaa ya kukwamilia uongozi.

Warundi wanaulizwa kuchagua pendekezo la kuongeza muda wa kuwa rais kutoka awamu ya miaka tano hadi saba, ambayo itamwezesha Nkurunziza, ambaye amekuwa uongozini tangu mwaka wa 2005, kuendelea usukani kwa miaka mingine kumi na nne muda wake utakapokamilika mnamo mwaka wa 2020.

Serikali hata hivyo imekanusha madai kwamba hilo ndilo lengo kuu, ikisema mabadiliko yanayopendekezwa ni ya kulainisha katiba.

Burundi imebadilisha katiba yake mara kadhaa miaka ya hivi punde- Miaka mitatu iliyopita rais Nkurunziza alifanikiwa kujiongezea muda zaidi ya miaka kumi iliyotarajiwa, hali ambayo ilileta maandamano yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 700 huku wengine wapatao 400,000 wakitoroka makwao baada ya msako wa serikali.

Wapinzani wa rais Nkurunziza wanamshutumu kwa kupuuza makubaliano yaliyoafikiwa Arusha Tanzania, ambayo iliweka muda wa kuwa rais usipite miaka kumi.

Mashirika ya kutetea haki za kibinadamu pia yameelezea wasiwasi wao na kusema wapinzani wamekuwa wakishambuliwa na kuhangaishwa.

Serikali imekanusha vikali madai haya, ikieleza kuwa wapinzani wa kura hii wamepewa fursa ya kufanya kampeni zao kwa njia iliyo huru.

Lakini hali ya taharuki imetanda nchini, na baadhi ya viongozi wa upinzani wametorokea nchi nyingine.

Burundi ina historia ya machafuko tangu miaka ya 60, mabaya zaidi yakiwa ya miaka ya 90 ambapo vita vya wenyewe kwa wenyewe vilisababisha vifo vya zaidi ya watu 300,000.

Mkataba wa Amani uliotiwa sahihi Arusha ndio ulimaliza vita hivyo na kumwezesha Pierre Nkurunziza kuwa rais.

Ni mkataba huo huo ulio hatarini sasa baada ya kura ya Alhamisi.

 

 

 

By Jamhuri