Baada ya kuambulia kichapo cha bao 1-0 dhidi ya Mbao FC katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa CCM Kirumba, jijini Mwanza, uongozi wa klabu ya Simba umewaomba radhi mashabiki wake.

Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara, ameibuka na kuomba radhi wa wapenzi, mashabiki na wanachama wa timu hiyo kwa namna walivyoyapokea matokeo hayo ya kusitikisha kwao yaliyosababisha kupoteza alama tatu.

Manara amesema kuwa klabu imejipanga kufanya maamuzi sahihi bila ya presha kwani anajua wanasimba wote wameumizwa kufungwa na Mbao ugenini huku akiwataka wawe watulivu kipindi hiki.

“Bodi ya Wakurugenzi, Sekretarieti na Benchi la Ufundi na wachezaji wa klabu ya Simba wanawaomba radhi Wanachama na Washabiki wetu kwa matokeo ya leo (jana).

“Tumeumia sote na tunawaomba mjue hii ni mechi ya nne tu, tutafanya maamuzi sahihi bila pressure kwa maslahi MAKUBWA ya Timu na klabu, nawaomba mtulie katika kipindi hiki” aliandika Manara kupitia ukurasa wake wa Instagram.

By Jamhuri