Tunapozungumzia huduma za jamii huwa tunazungumzia masuala ya elimu, afya ,maji, umeme, huduma kwa wazee, huduma kwa walemavu na kadhalika.

Kwa ujumla huduma za jamii ni huduma zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya watu wote. Watu wote maana yake ni wananchi.

Hapana shaka kuna malalamiko ya vyama vya upinzani dhidi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuhusu masuala mbalimbali yanayoweza kuchangia katika kuing’oa CCM.

Lakini ukitaka kusema kweli malalamiko ya wananchi dhidi ya CCM ndiyo yatakayo angusha CCM. Hao ndio walio wengi.

Chukua, kwa mfano, kama wapinzani watategemea kushinda kura za maoni kwa kupigania Serikali tatu wasahau.Hawatashinda.

Tunaendelea kukumbushana tena na tena  kwamba wananchi wa kawaida (ambao ndio walio wengi ) hawaipendi Serikali. Kwao kila Serikali ni chombo cha ukandamizaji.

Kwa hiyo mwananchi wa kawaida hataki Serikali tatu. Serikali mbili alizoendelea kuwa nazo zinamtosha. Ni vyama vya upinzani  vyenye maslahi na Serikali tatu katika mategemeo kwamba moja itakuwa yao.

Serikali inaweza ikajenga mijini barabara za kisasa kama nini. Mwananchi wa kijijini  haoni kama kuna kitu kimefanywa  na Serikali kama barabara za vijijini haziwezi kusafirisha  mazao yake.

Ni huduma za jamii zinazotolewa  kwa wananchi mijini na vijijini zitazokazoamua kushinda au kushindwa kwa CCM katika uchaguzi.

Tuanze na elimu. Hakuna asiyekubali kuwa hali ya elimu Tanzania ni mbaya sana. Na sababu yake ni moja. Wizara ya Elimu  na Mafunzo ya Ufundi imeshindwa kusimamia elimu Tanzania. Ni katika mazingira hayo Waziri wa Elimu nchini Tanzania ameendelea kuitwa ‘mzigo’ hata na chama tawala.

Kusema ukweli juu ya  mambo  ya nchi yako si kukosa uzalendo. Waliokosa uzalendo ni wale wasiosimamia elimu kwa ufanisi.

Tatizo kubwa Tanzania si kukosekana kwa watu wanaoona mambo yalivyo mabaya na kushauri kifanyike nini. Tatizo  moja kubwa la Tanzania ni wale walio serikalini kufanya mambo  kwa kiburi na ukaidi  kana kwamba elimu ni chombo chao cha mfukoni kumbe elimu  ni mali ya umma wote wa Tanzania.

Wananchi wameendelea kupiga kelele kwamba vitabu vinavyotumika mashuleni havifai. Walioko wizarani wanaendelea kuruhusu vitabu hivyo vibovu kuingia mashuleni kwa sababu tu wanapewa rushwa na wachapishaji wa vitabu.

Sasa wametosheka na utajiri walioupata kutokana na kuruhusu vitabu vibovu kuingia mashuleni. Kwa hiyo suala la uteuzi wa vitabu  vya kuingia mashuleni wamehamishia Taasisi ya Elimu.

Kusema kweli miaka yote hii watoto wa maskini wa Tanzania wameendelea kupewa elimu mbovu  kwa kukusudiwa kabisa. Vitabu vinavyotumika mashuleni vinashindana kwa ubovu  badala ya kushindana kwa ubora.

Tunasema kwamba kama upinzani utafanikiwa kushika madaraka ya kuongoza nchi  wahakikishe wanawakamata watendaji wakuu wote wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi  na mawaziri wao kwa kuendelea kuhujumu elimu  ya watoto wa maskini ambao ndio walio wengi. Wamekuwa wasaliti wakubwa. Watu na akili zao timamu  wanaruhusu vitabu vibovu viingie mashuleni eti kwa sababu wanalipwa na wachapishaji wa vitabu  kwa kuvuruga elimu Tanzania.

Fedha ya vitabu vya rada imetumika  vibaya. Kadhalika na fedha ya madawati ya rada. Tuna wizara inayosimamiwa  wa watu waliokosa uzalendo na uadilifu.

Haihitaji kueleza wazazi wa Tanzania walivyochoka  na fedha ya tuisheni wanayotakiwa  kutoa kila siku. Inatisha kukutana hata na watoto wa chekechea  wanao rudishwa nyumbani na walimu huku wakidai kuwa wamepigwa kwa sababu tu wazazi wao wamekosa fedha ya tuisheni.

Ni vyema Serikali ikaona ubaya wa tuisheni kwa wazazi na ikachukua hatua ya kurekebisha mambo.

Halafu kuna suala la lugha ya kufundisha Shule za Sekondari. Wadau wa elimu nchini kote wamepiga kelele kudai lugha ya kufundishia shule za sekondari iwe lugha ya Kiswahili

Lakini wakaidi tulio nao hawasikii kitu. Wameshikilia lugha ya kufundishia iendelee  kuwa Kiingereza. Watu hawa wanashindwa kujua kuwa Kiingereza ni lugha au chombo cha kupashania habari. Kiingereza siyo elimu.

Ni ujinga ulioje mtu anayeshugulika na elimu  kuamini kwamba Kiingereza ni elimu Kiswahili si elimu!

Nchi zilizoendelea (si sisi) zinafahamu kwamba mtu yeyote duniani anaeelewa vizuri na kumiliki maarifa akifundishwa kwa lugha anayoijua sana.

Kwa hiyo nchi hizo zilizoendelea zinafundisha watoto wao kwa lugha zao. Lugha za kigeni  zinafundishwa kama somo tu. Waingereza hawafundishi watoto wao kwa kutu mia lugha ya Kigiriki au hata Kirumi kama ilivyofanya huko nyuma.

Leo Waingereza wanafundisha watoto wao kwa kutumia lugha ya Kiingereza  Wafaransa kwa kutumia lugha ya Kifaransa,  Wanyarwanda kwa kutumia Kinyarwanda, na Watanzania kwa kutumia Lugha ya Kiingereza!

Hebu turudi kwenye Tume ya Makwetta ya mwaka 1980. Hii ni tume iliyoteuliwa na Rais Julius Nyerere kuchunguza mwenendo wa elimu Tanzania. Iliongozwa na Jackson Makwetta, Waziri wa Elimu.

Kwa muda mrefu  Serikali ya Mwalimu Nyerere ilikuwa imesikia manung’uniko ya wadau wa elimu kwamba elimu ilikuwa  imeshuka kiasi cha kutisha.

Serikali ilikuwa sikivu. Haikuwa ya ukaidi. Ikaunda tume. Tume ikathibitisha kwamba  elimu ilikuwa imeshuka. Ikapendekeza hatua za kuchukuliwa kurekebisha hali ya mambo.

Tume ya Makwetta, pamoja na mambo mengine, ilibaini ukweli kwamba mwanafunzi anaelewa vizuri zaidi akifundishwa kwa lugha anayoijua vizuri. Tena huchangia mawazo kirahisi.

Matokeo ya dosari ya kufundisha wanafunzi kwa lugha ya kigeni ambayo hawaielewi yako wazi kabisa .Watoto hawapati maarifa wanayoyahitaji kwa ukamilifu wake. Kwa kawaida watoto huyapata maarifa kwa kukariri tu kwa ajili ya mitihani. Wakitoka shule wanasahau mambo yote. Kikubwa zaidi vipaji vya watoto wetu wa  Tanzania hupotea bila kutimika kwa sababu mwanafunzi anashindwa kujieleza.

Ukiuliza sababu kwa nini watu wachache wameshikilia wanafunzi wa shule za sekondari waendelee  kufundishwa kwa lugha ya Kiingereza utaambiwa lengo ni kuhakikisha kwamba nchi jirani hazituachi nyuma. Hivi nani hajui kuwa Kenya na Uganda zimetuacha mbali sana kielimu? Wao wana Wizara za Elimu zinazoongozwa na wazalendo na waadilifu.

Lakini unaweza kuambiwa pia kwamba  Kiingereza  kinaendelea kutumika kama  lugha ya kufundishia shule ya sekondari ili vijana wetu wapate ajira. Tuseme  kweli.

Hivi mpaka leo ni vijana wangapi wa Tanzania wamepata ajira baada ya kumaliza masomo yao  kwa sababu wamefundishwa  katika lugha ya Kiingereza?

Wengi hawana kazi  kwa sababu  hata wakipewa usaili kwa lugha ya Kiingereza hufanya vibaya.

Mbona kuna Watanzania wamepata ajira China  ingawa  hawajui Kichina? Mbona tuna Wachina wengi Tanzania  walipata ajira  pamoja na ukweli kwamba  hawajui lugha ya Kiswahili?

Cha kushangaza taifa la Tanzania lina lugha  yake  ya taifa, Kiswahili, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alifanya juhudi  kubwa katika kuhakikisha  kwamba lugha ya Kiswahili  inakuwa lugha ya taifa.

Ilikuwa Januari  1960 Mwalimu Nyerere  alipoongoza Chama cha TANU  katika kupitisha azimio  kwamba Kiswahili kingekuwa lugha ya taifa  baada ya Tanganyika kupata uhuru.

Ikawa hivyo. Februari 13,1963  lugha ya Kiswahili  ilianza kutumika kama lugha rasmi Bungeni pamoja na Kiingereza.

Kuna mataifa mengi ya Afrika ambayo lugha rasmi ni Kiingereza au Kifaransa  Tanzania ina lugha yake rasmi, Kiswahili. Lakini leo watu wachache wanabeza lugha ya Kiswahili. Hawapendi Kiswahili kichukue nafasi yake.

Pengine unaweza kusamehe lugha ya Kiswahili kutotumika kama lugha ya kufundishia. Lakini huwezi kusamehe kuona kwamba hata somo la Civics (Uraia) linafundishwa kwa Kiingereza.

Ukweli ni kwamba somo la Uraia  linahusu maisha ya kila siku ya Mtanzania. Na Mtanzania ana lugha yake ya taifa. Ni kweli Kiswahili hakifai hata kufundishia somo la Uraia? Kwa kweli tunashangaza. Tunafundisha uzalendo  na maadili  ya taifa kwa kutumia lugha ya kigeni ambayo  hata mwalimu mwenyewe hajui vizuri?

Hii ni sababu ya kutosha maadili na uzalendo  kuendelea kumomonyoka nchini Vijana wetu hawaelewi lugha inayotumika kuwafundishia uzalendo na maadili ya Tanzania. Wakati wa somo la Elimu  ya Siasa ambalo lilifundishwa kwa lugha ya Kiswahili wanafunzi  walilielewa vizuri na wakajengeka kizalendo.

Sasa tuangalie huduma za afya. Nazo pia zina matatizo makubwa kuanzia kwa daktari Katika nchi ambayo watu wake walio wengi ni maskini kama Tanzania kumdai mgonjwa ada ya shilingi elfu tano  ili aweze kumwona daktari ni mzigo mkubwa sana  kwake.

Ajabu ni kwamba ataandikiwa dawa ambazo hatazipata hospitali. Atatakiwa akatafute mahali pengine. Huko akizikuta atalazimika kuzinunua  na hana fedha za kununulia dawa.

Kwa hiyo mgonjwa ataendelea kujiuguza bila kupata dawa. Atapona? Na hata kama atauguzwa hospitalini atalazwa sakafuni. Hatalala kitandani.

Kwa hiyo katika hali hiyo unakuta mtu wa kawaida anaichukia CCM na Serikali yake. Huduma za maji nazo pia haziridhishi. Wanawake vijijini wanatumia wakati wao  mwingi kutafuta maji badala ya kuendelea  na shughuli zao za kuzalisha mali. Nako mijini mambo ni hayo hayo. Wanawake wanatumia saa za kazi kwa  kusaka maji  mitoni na kando ya bahari.

Hakuna asiyeona kwamba Serikali inafanya kazi nyingi tena nzuri. Katikati ya kazi zote hizo inazofanya Serikali ni vyema  ikaweka mstari wa mbele  huduma za jamii mijini na vijijini.

Hata wakati wa Azimio la Arusha Serikali ya Mwalimu Nyerere ilitoa bure huduma za elimu, afya, na maji kutokana na umuhimu wake kwa wananchi.

Kwa hiyo  hali ya kulegalega huduma za jamii mijini na vijijini inaweza kusababisha anguko la CCM na Serikali yake.

By Jamhuri