Mahakama ya Hakimu Makazi Morogoro imewaachia kwa dhamana wabunge wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) leo Disemba 7.

Wabunge hao walioachiliwa ni Peter Ambrose Lijualikali ambaye ni Mbunge wa Kilombero na Susan Limbweni Kiwanga ambaye ni Mbunge wa Mlimba.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 296, wabunge hao pamoja na wanachama wengine wa CHADEMA zaidi ya 30 wanakabiliwa na mashtaka mbalimbali likiwamo la kuchoma moto Ofisi ya Kata ya Sofi iliyopo wilayani Malinyi.
Wakili Bantulaki wa upande wa mashtaka amedai kuwa washtakiwa hao kwa pamoja walitenda makosa hayo Novemba 26 mwaka huu katika Kata ya Sofi wilayani Malinyi.

Alidai kuwa bila uhalali huku wakijua kufanya hivyo ni kosa washtakiwa hao walikula njama na kuchoma moto ofisi ya kata hiyo sambamba na kufanya uharibifu wa mali mbalimbali za ofisi hiyo.

By Jamhuri