Magufuli Awanyooshea Kidole Wanaotaka Kuandamana

Rais Dkt John Magufuli amewaonya vikali watu wanaopanga kufanya maandamano nchini humo akisema kwamba hawataruhusiwa.

“Wapo watu wangependa nchi hii kila siku tuwe na migogoro,” amesema Dkt Magufuli.

“Wapo watu ambao wameshindwa kufanya siasa za kweli, wangependa kila siku tuko barabarani tunaandamana. Watu wao wanahamia huku, wao wanataka wabaki wanaandamana kule.

Nitasema ngoja waandamane wataniona. Kama kuna baba zao wanawatuma, watakwenda kuwasimulia vizuri.”

“Niliapa kwa katiba kwamba nchi hii lazima iwe ya amani.”

“Maneno huwa ni mabaya, na maneno saa nyingine huwa yanaumba,” amesema, na kuwahimiza Watanzania wawe “wazalendo”.

Dkt Magufulia amekuwa akishutumiwa na vyama vya upinzani na makundi ya kutetea haki za kibinadamu nchini humo kwa kukandamiza demokrasia, tuhuma ambazo amezipinga.

Dkt Magufuli leo amekuwa eneo lake la nyumbani la Chato, mkoani Geita kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo ambapo pia ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BOT) kuendelea kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kuzifungia benki ambazo zinaendeshwa kwa kusuasua ili kulinda sekta ya benki na uchumi wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki.

“Benki itakayoshindwa kujisimamia ifungeni, ni afadhali tuwe na benki chache zinazofanya vizuri kuliko kuwa na utitiri wa benki ambazo hazifanyi vizuri,” amesema.

“Kulikuwa na mchezo benki ikishindwa kujisimamia Serikali inatoa fedha za wananchi na kwenda kuipatia mtaji, matokeo yake huko ndiko wajanja walikuwa wanakula fedha za wananchi kwa kukopa na kutorudisha mikopo, naomba niwaeleze mimi sitatoa fedha kuipatia benki inayoshindwa kujisimamia” ameeleza.