Uongozi wa klabu ya Simba kupitia Ofisa Habari wake, Haji Manara, umesema kukosekana kwa Nahodha wake, John Bocco, hakutoweza kuleta athari yoyote katika mchezo dhidi ya Yanga leo.

Simba itakuwa mwenyeji kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam kucheza na watani zao wa jadi Yanga kuanzia majira ya saa 11 za jioni.

Kuelekea mechi hiyo, Manara ameeleza pengo la Bocco haliwezi kuiathiri timu kwakuwa ina wachezaji wengi ambao watachukua nafasi yake.

Manara anaamini bado mchezo huo utaleta ushindani licha ya kukosekana kwa Bocco ambaye alipewa kadi nyekundu ya moja kwa moja katika mechi iliyopita dhidi ya Mwadui FC.

Katika mechi hiyo ya ligi, Bocco alipatia kadi hiyo kutokana na kosa la kumpiga ngumi mchezaji wa Mwadui FC na leo ataishuhudia timu yake ikicheza akiwa jukwaani.

By Jamhuri