Jambazi ni jambazi, fisadi ni fisadi, tapeli ni tapeli tu. Madhara ya

vitendo vya watu hawa kwa jamii ni yale yale bila kujali kuwa wanatoka

chama tawala au upinzani. Madhara ya vitendo hivi hayaangalii kuwa mtu

huyu anajifanya mchungaji, askofu au sheikh. Hayaangalii kwamba mtu

huyu anapenda kuuza sura kwenye runinga kiasi gani. Na wala hayazingatii kuwa mtu huyu anapiga kelele bungeni kiasi gani au anajua

matusi kiasi gani.

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ndicho chama kikuu cha upinzani nchini. Matarajio yao ni kushika dola, na ndiyo maana siku zote wako mbele kuanika udhaifu na upungufu uliomo ndani ya chama tawala. Ndiyo maana karata dume inayochezwa na Chadema na vyama vingine vya upinzani sasa hivi ni UFISADI wa ESCROW unaonasibishwa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi

(CCM). Sina mgogoro na hilo. Ni wajibu wao na kama kweli wana nia ya

dhati kututoa hapa tulipo na kutupeleka katika nchi ya asali na

maziwa, basi wajitahidi kuhakikisha hili la Escrow na ufisadi mwingine

yanafikia mwisho.

Inatosha sana kwa uongozi wa juu wa Chadema kutafakari juu ya hatua

waliyochukua wana-Chadema wa Iringa kwa kumuengua Msigwa kwenye

kinyang’anyiro cha kugombea uenyekiti wa wilaya. Sababu zilizotolewa

kwa kuenguliwa Msigwa ni kujifanya msomi na mjuaji wa kila kitu; mtu

aliyejaa dharau na mchache wa kukubali kushauriwa, miongoni mwa sababu

nyingine.

Msigwa hajataka kujifunza chochote na bado anajihesabu kuwa na mvuto

kwa wananchi wa Iringa! Nitahadharishe kuwa kama Chadema wamelichoka

Jimbo la Iringa Mjini, basi wampe Msigwa kijiti.

Kupitia mikutano iliyo rasmi na ile ya vijiweni, upinzani unaonekana

kuwa na ajenda nzuri na nia ya dhati kutukwamua kutoka hapa tulipo.

Hata hivyo, upinzani utafanya makosa makubwa kama wataamini kuwa

wananchi tunawapima kwa maneno yao matamu tu. Wananchi wanaona vitendo

vyao au vya baadhi ya viongozi wa upinzani.

Peter Msigwa (nasita kumwita mchungaji au mheshimiwa), ni Waziri

Kivuli wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Ni mmoja wa viongozi wa

Chadema, chama kinachoonekana mbadala wa CCM.

Komredi Freeman Mbowe amempa Msigwa kazi kuhakikisha kuwa anachunga rasilimali zetu zisifujwe na kuharibiwa hovyo. Naamini kwamba Komredi Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya

Upinzani Bungeni, hakumtuma Msigwa kwenda kuunda genge la ulaji na

mafisadi; kwenda kutetea uhuni unaofanywa na baadhi ya watu na wala

kwenda kutafuta utajiri kwa kutumia kofia ya uwaziri kivuli. Hiyo ni

dhamana na lazima aitunze na aipe heshima yake.

Naomba nisitafune maneno kwamba kama Chadema kweli inataka kuendelea

kuaminika mbele ya Watanzania, basi ingeonesha mfano kwa

kuwawajibisha watu ambao wanaonekana kukitia najisi chama kama

mchungaji huyu.

Katika kipindi cha runinga ya ITV kinachojulikana kama ‘Dakika 45’ Desemba 8,

mwaka huu, Msigwa ndiye aliyekuwa mgeni wa kipindi. Katika maswali

aliyoulizwa ni pamoja na baadhi ya kashfa  zinazomhusu Lazaro Nyalandu

na James Lembeli. Kwanza, mtangazaji alitaka kujua kulikoni, kwani

siku za nyuma Msigwa alikuwa akipigia sana kelele Wizara ya Maliasili

na Utalii, lakini siku hizi amekuwa bubu.

Jibu la Msigwa likawa eti Waziri Nyalandu ametumia ‘approach’ nzuri

tofauti na wenzake ambako anamwalika katika shughuli na hafla

mbalimbali na hivyo hana sababu ya kuongea!

Hivi mtu mwenye akili anaweza kutoa jibu la kipuuzi kama hili? Ukweli

ni kwamba hii haina tafsiri nyingine zaidi ya ukweli kwamba Msigwa

anakiri kuingizwa kwenye ulaji, kwa hiyo hawezi tena kupiga kelele!

Vinginevyo, atuambie kwamba unapofadhiliwa unapata wapi ‘moral

authority’ ya kumkemea mfadhili wako.

Jibu jingine lililotia kichefuchefu ni utetezi wake juu ya matumizi

mabaya ya Leseni ya Rais iliyoruhusu kuuawa wanyamapori zaidi ya 700.

Msigwa anadai kuwa si kweli kwamba eti marafiki hawa wa Nyalandu

wameua wanyama 700, bali waliua nyati watano tu na pundamilia wawili.

Akadai kuwa picha za watoto wadogo waliokuwa wanawinda zilizotoka

katika gazeti la JAMHURI hazikuwa zao! Huyu mbunge ni wa ajabu kabisa!

Mchungaji gani mwongo namna hii? Ambacho hakusema kuwa hakikuwa cha

kweli ni juu ya nakala za vibali na nyaraka zilizokuwa gazetini.

Halafu akawafagilia Wamarekani hawa kuwa ingawa hawakutakiwa kulipa,

waliamua kulipa pesa nyingi sana serikalini! Kwa mara nyingine,

nashangaa ni vipi mtu anayejiita mchungaji anaweza kuwa mwongo kiasi

hiki!

Kwanza, Msigwa ameupotosha umma kwa makusudi kuwa eti JAMHURI

iliripoti kuuawa wanyama 700. Hamna aliyeripoti kuwa wanyama 700

wameuawa. Tulichoandika ni juu ya Leseni ya Rais iliyoruhusu kuuawa

wanyama 700. Na ni baada ya JAMHURI kuripoti uhuni huu ndipo

Wamarekani hawa walipoamua kutimka na kurudi kwao huku wakiwa wameua

nyati watano. Jibu alilotakiwa kujibu kibaraka huyu wa Nyalandu na

Wamarekani ni endapo kulikuwa na uhalali wa kutoa Leseni ya Rais kwa

familia ya Friedkin (je, wana sifa hizo?) Leseni nane zilizotolewa

ziliruhusu wanafamilia wanane kuwinda wanyama 49 kila mmoja. Kwa hesabu

za msomi Msigwa jumla ya wanyama wote itakuwa saba!

Kwa kuwa Msigwa ameamua kuwa kuwadi wa Nyalandu na Wamarekani, basi

angetusaidia zaidi kujibu maswali mengine tuliyouliza yakiwamo yale ya

uhalali wa Nyalandu kugawa vitalu kinyume cha sheria kwa marafiki zake

hawa. Itakumbukwa kuwa mara tu baada ya kuibuka kashfa hii ya matumizi

mabaya ya Leseni ya Rais, tulitabiri kuwa si Msigwa wala Lembeli

ambaye angenyanyua mdomo kukemea ufisadi huu. Tuliweka wazi kuwa hili

lisingewezekana kutokana na kujengeka kwa mtandao wa ulaji kati ya

wawili hawa na Nyalandu.

Uswahiba wa kampuni za Friedkin na Nyalandu na Lembeli

unaeleweka. Tuna taarifa juu ya ufadhili wa ndege alizokuwa anapanda

Nyalandu kwa shughuli zake binafsi. Kwa upande wa Lembeli, mfano mmoja

ni ile hadidu ya rejea aliyojitengenezea kwenye ripoti ya Operesheni

Tokomeza akitaka Mkurugenzi wa Wanyamapori awajibishwe kwa kuwa eti

rafiki zake hawa wamekosa kitalu walichokuwa wanakitaka huko Makao

WMA!

Ingawa suala hili halikuwa na uhusiano kabisa na ujangili, Lembeli

hakuona soni kuliweka kwenye ripoti ili kuwafurahisha Nyalandu na

mawakala zake Wamarekani.

Huhitaji akili nyingi kugundua kuwa Msigwa naye ameingizwa kwenye

ulaji wa kampuni hizi; na kuingia kwake humo kumekuja kutokana na haja

ya kumtumia kufanikisha unyang’anyi wa kitalu cha Green Miles ambacho

Nyalandu kawakabidhi Wamarekani bila kufuata sheria za nchi.

Katika hali kama hiyo ambako Msigwa tayari kageuka bidhaa, tunatarajia

angethubutu vipi kusema lolote kuhusu uharamia wa Wamarekani hawa

kuruhusiwa kuua wanyama wetu 700? Ujasiri huo atautoa wapi? Ni kwa

sababu hiyo hiyo Msigwa aliamua kuufyata ghafla juu ya ile kashfa ya

Nyalandu kuamua kurefusha msimu wa uwindaji ili kuwafurahisha

Wamarekani hawa waliotaka waruhusiwe kuwinda mwaka mzima.

Awali, Msigwa alitoa taarifa kwenye vyombo vya habari kulaani kitendo

kile akikiita ufisadi. Lakini huhitaji akili nyingi sana kugundua kuwa

baada ya kuingizwa kwenye ulaji, hakuwa na ujasiri wa kusema chochote

na ndiyo maana hata kwenye hotuba yake ya bajeti aliipotezea.

Atasemaje wakati kusema ina maana kugusa maslahi ya waajiri wake?

Swali juu ya mpango wa Nyalandu na Lembeli kuuza mbuga na hifadhi za

Taifa, Msigwa anawatetea maswahiba wake hawa akidai kuwa ni upuuzi

mtupu na kwamba eti tulitaka kuuza gazeti tu!

Afadhali basi Msigwa angeamua kukaa kimya kuliko kuropoka upuuzi huo.

Lakini kwa kuwa ameamua kuwa kuwadi na msemaji mkuu wa mabwana hawa,

basi angejibu maswali ya msingi yaliyojitokeza kwenye makala zetu

kadhaa kuhusu kashfa hii.

Atuambie rafiki zake hawa walifuata nini Afrika Kusini hata baada ya

kupata ushauri wa kitaalamu juu ya hatari ya African Parks Network

(APN)? Atuambie ilikuwaje Lembeli ambaye ni mmoja wa Wakurugenzi wa

Bodi ya APN (asasi inayotaka kukabidhiwa mbuga zetu) aiwakilishe

Serikali kwenye mapatano na asasi hiyo. Kama akili ya Msigwa haiwezi

kuyaona hayo, basi hatuna budi kurejea kuhoji ule utata wa kupata

division zero form four’ na hatimaye kutunukiwa digrii ya uchungaji!

Lakini wakati tunashangaa majibu ya kipuuzi ya Msigwa kwa maswali ya

Emmanuel Buhohela wa ITV, kuna haja ya kurejea historia yake kwa

ufupi ili tujue kuwa huyu ni mtu wa namna gani. Peter Msigwa amekuwa

akijipambanua kama kiongozi wa dini msomi mwenye digrii (graduate),

ingawa wapo wanaohoji uchungaji wake na kutaka kujua kuwa ni chuo

kikuu kipi ambacho hupokea wanafunzi waliofeli. ‘Mtumishi huyu wa

Mungu na msomi’ ndiye Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii.

Alhamisi, Februari 13, mwaka huu, Nyalandu alipomjibu Martin Fletcher

kutokana na makala yake kuhusu ujangili kwenye gazeti la Daily Mail,

Msigwa alimjia juu huku akimtuhumu kuwa anawabembeleza majangili ambao

wanafahamika kwa majina na wapo mitaani wakiendelea na ujangili.

Msigwa alibainisha kuwa mara nyingi Nyalandu amekuwa akinukuliwa na

vyombo vya habari akidai kuwa mtandao wa ujangili unafahamika na ni

mpana unaohusisha watu wenye nguvu za pesa na huku akiwaomba

wanaojihusisha na biashara hiyo waachane nayo mara moja.

Akasema kuwa kauli hizo za Nyalandu zinaonesha dhahiri kuwa kuna watu

hawaguswi na sheria na wapo juu ya sheria. Msigwa akasema: “Majibu

haya ya Waziri (Nyalandu) yanadhihirisha kuwa mtandao huu

unaolalamikiwa na kuogopwa ndiyo unaohusisha Ikulu, wanasiasa,

watumishi wa Serikali, maafisa wanyamapori, maafisa usalama, polisi,

wanajeshi, pamoja na wafanyabiashara wakubwa, ambao wamekuwa

wakijihusisha na Serikali ya CCM.”

Akaendelea kumponda Nyalandu kuwa anatumia hisia badala ya vielelezo

kujibu hoja. Akatuhumu kuwa Serikali haichukui hatua kwa wahusika

ambao wanajulikana kwa majina na wako mitaani wakiendelea na biashara

hiyo haramu kwa kuwa wanatafuta fedha kwa ajili ya uchaguzi ujao.

Machi 23, mwaka huu, Msigwa alitoa taarifa kwa umma iliyokuwa na kichwa

cha habari kilichosema: “Taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu

mazingira ya rushwa na ufisadi katika sekta ya uwindaji nchini.”

Katika taarifa hiyo, Msigwa alisema: “Ndugu wanahabari, kati ya mambo

yanayoashiria mazingira ya rushwa katika sekta ya uwindaji hapa nchini

ni kitendo cha Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu,

kurefusha, kinyume cha sheria, muda wa msimu wa uwindaji kuanzia

tarehe 1 Julai hadi 31 Machi kila mwaka tofauti na muda wa kisheria

ambao ni kuanzia tarehe 1 Julai hadi 31 Desemba kila mwaka. Waziri

Nyalandu ametoa agizo la kurefusha msimu wa uwindaji tarehe 19 Machi,

2014 akiwa na wamiliki wa vitalu na makampuni ya uwindaji.”

Aidha katika taarifa hiyo Msigwa akasema: “Ndugu wanahabari, jambo

linaloashiria mazingira ya rushwa zaidi ni kwamba wenye makampuni ya

uwindaji wamemmwagia sifa waziri na kusema kuwa ni mtu makini na

msikivu. Jambo hili la wenye makampuni kufurahia uamuzi wa waziri

linaonesha japo kwa mazingira kwamba wenye makampuni hao walikuwa

wakitafuta kubatilisha sheria iliyoweka ukomo wa msimu wa uwindaji

kuwa miezi sita na badala yake wanataka wawinde bila ukomo kwa ajili

ya kujinufaisha wao wenyewe.”

Mwisho akamuonya Nyalandu na kumtaka abatilishe uamuzi wake mara moja

huku akisema: “Wafanyabiashara ni wadau muhimu sana, ila ni hatari

kuwaruhusu waiburuze wizara kiasi cha kuhatarisha maslahi ya uhifadhi

wa wanyamapori.

Mei 13, mwaka huu, wakati anawasilisha hotuba ya Kambi Rasmi ya

Upinzani Bungeni kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015, Msigwa alianika

udhaifu wa Nyalandu huku akimlaumu kwa kukiuka kwa makusudi sheria na

taratibu za utumishi wa umma, kutumia vibaya pesa za umma kumwalika

Martin Fletcher wa Daily Mail nchini kama njia ya kumhonga n.k.

Msigwa akasema: “Si mara ya kwanza kwa Kambi Rasmi ya Upinzani kuhoji juu ya usafi wa Lazaro Nyalandu, Waziri wa Maliasili na Utalii, na mara

kadhaa tumeonesha kwa kiasi kikubwa udhaifu wake na kutoa vielelezo

mbalimbali vinavyotilia shaka utendaji wake kabla na hata baada ya

kukabidhiwa wizara hii nyeti!”

Ndugu msomaji, taarifa hizo za Msigwa kwa umma na hotuba yake bungeni,

achilia mbali kauli nyingine ambazo si rasmi, zinaonesha mtazamo wa

Msigwa kwa Nyalandu katika kipindi cha miezi michache tu iliyopita.

Hapa kuna vimelea vya rushwa.

 

Itaendelea

By Jamhuri