Muhammad Ali (74), bingwa wa zamani wa dunia wa ngumi za uzani wa juu na mmoja kati ya wanamasumbwi bora zaidi duniani, aliyefariki katika Hospitali ya Phoenix Area, Arizona, nchini Marekani mwishoni mwa wiki iliyopita.

Bondia huyo aliyetamba katika miaka ya 1960 mpaka 1980 alipoamua kujiuzuru, atakumbukwa daima kwa mchango wake mkubwa katika mchezo huo. Mwanamichezo huyo wa masumbwi, alijulikana zaidi kwa jina la “The Greatest” Alilazwa katika hospitali hiyo akisumbuliwa na tatizo la upumuaji uliosababishwa na ugonjwa Parkison Disease.

Alizaliwa katika kitongoji cha Cassius Marcellus Clay,Louisville, Kentucky, Januari 17, mwaka 1942. Alikuwa ni kijana wa mtoto wa mchoraji. Akiwa na umri wa miaka 12, aliibiwa baiskeli na aliwaambia maafisa wa polisi atahakikisha kwamba anawapata wezi wake.

 Enzi za uhai wake alikuwa amevunja rekodi ya kutwaa ubingwa wa dunia mara tatu wa ngumi za Uzani wa Juu. Mwaka 1981 aliamua kustaafu mchezo wa ndondi. Baadaye alianza kusumbuliwa na ugonjwa wa Parkinson hadi alipofikwa na mauti wiki iliyopita.

Pamoja na kusumbuliwa na ugonjwa huo, alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi na maambukizi katika njia ya mkojo. Msemaji wa familia ya bondia huyo, Bob Gunnell alisema kabla ya kufariki kwake alikuwa chini ya uangalizi wa Jopo la Madaktari na kwamba alikuwa anatarajia kutembelea jiji la London lakini alijikuta akisumbuliwa na maradhi hayo.

 

Kilichosababisha kujiunga na mchezo huo

Muhammad Ali hakuwa na nia ya kujiunga na mchezo wa ndondi, bali aliingia huko kwa bahati tu. Akiwa na umri wa miaka 12 akiwa na rafiki zake ndipo baiskeli yake ikaibwa.

Baada ya kugundua kwamba baiskeli yake imeibwa alishauriwa kwenye nyumba ya taasisi ya mafunzo ya Columbia ambako alimkuta Ofisa wa Polisi aliyefahamika kwa jina la Joe Martin aliyekuwa akisimamia mafunzo ya ndondi.

Alipomweleza Ofisa huyo wa Polisi kuhusu tukio la kuibwa kwa baiskeli yake na mtu ambaye hakufahamika alishauriwa kuanza kunoa ngumi zake kwa kujifunza mchezo huo wa ngumi kabla ya kuanza kumsaka mwizi huyo.

Alifanya bidii katika mafunzo hayo ya ndondi na alipofikisha umri wa miaka 18 alikuwa ameshinda medali ya dhahabu, katika mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika jijini Rome, Italia.

Ali alikuwa akiishi Louisville katika jimbo la Kentucky akijulikana kwa jina Mercellus Cassius Clay Jr kabla ya kubadili dini mwaka 1975 na kuitwa Muhammad Ali akiwa amefikisha umri wa miaka 33.

 

Rekodi yake ulingoni

Alicheza jumla ya mapambano 61, kati ya hayo alishinda 56, huku akishinda mapambano 37 kwa “knock out” na alipigwa katika  mapambano mitano tu.  

Akiwa kijana mdogo mwenye umri wa miaka 22 alivunja rekodi ya kutwaa ubingwa wa ngumi za uzani wa juu, ambayo baadaye ilikuja kuvunjwa na Mike Tyson mwaka 1986 akiwa na umri wa miaka 20.

Hata hivyo baada ya kutwaa taji la dunia la uzito wa juu mwaka 1967,  alikamatwa na kutupwa jela kwa kosa la usaliti, kwa kukataa kujiunga na Jeshi la Marekani ili kushiriki katika vita vya Vietnam. Ali alivunja rekodi ya kutwaa mataji matatu ya uzito wa juu wa dunia mwaka 1964, 1974 na 1978.

 

Mazishi yake

Mazishi ya Muhammad Ali yatkuwa ni ya wazi katika eneo la makaburi, matayarisho ya mazishi pamoja na zoezi zima la vitafanyika siku ya Ijumaa, nyumbani kwake, Louisville.

Rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton anatarajiwa kushiriki. Bingwa huyo wa ndondi za uzito wa juu mara tatu wa mmoja wa wanamichezo wa aina yake katika karne ya 20. 

 

Nukuu zake 

“Pepea kama kipepeo, ng’ata kama nyuki. Mikono haiwezi kupiga kitu ambacho macho hayaoni,” Maneno hayo yalikuwa yakirudiwa mara kwa mara kuelezea stairi yake ya kupigana anapokuwa kwenye ringi.

“Nilipigana na mamba, nikapambana na nyangumi, nilikumbatia moto, niliipeleka jela radi, mimi ni mtu mbaya ….Wiki iliyopita niliua mwamba, nikajeruhi jiwe, nilisababisha jiwe likalazwa hospitali. Mimi ni hatari, ninaweza kusababisha dawa zikaugua,” maneno hayo aliyasema huku akicheka alipokuwa anaingia kwenye pambano lake la mwaka 1974, lililochezwa katika ardhi ya Afrika, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, na kumshinda mpinzani wake George Foreman, katika pambano lililoitwa ‘Rumble in the Jungle’ 

By Jamhuri