Moja ya mambo yaliyomfurahisha Mkata Mitaa (MM) ni hatua iliyochukuliwa na Serikali kupiga marufuku pikipiki maarufu kwa jina la ‘bodaboda’, mikokoteni (makuta), baiskeli na bajaj kuingia katikati ya jiji la Dar es Salaam.

MM amefurahishwa na mpango huo kutokana na boda boda kuwa kero kwa waendesha magari na waenda kwa mguu wanaotumia barabara za katikati ya jiji.

Mara kwa mara MM amekuwa akishuhudia ajali mbalimbali zinazosababishwa na bodaboba.

Kabla ya mpango huo ilikuwa jambo la kawaida kuona sheria ikivunjwa, mfano, katika Barabara ya Samora ambayo inaruhusu magari kutoka mnara wa saa kwenda mnara wa askari, lakini kwa waendesha bodaboda wao kwao ilikuwa sawa kutoka mnara wa askari kupanda hadi mnara wa saa.

Msemaji wa Mamlaka  ya Udhibiti Usafiri wa Nchi kavu na Majini,  David  Mziray, amenukuliwa akisema, “Madereva wa bajaj na Bodaboda wamekuwa wakifanya kazi pasipo kuzingatia sheria za nchi jambo ambalo limesababisha ajali nyingi kutokea.”

Mziray amesema  kuwa leseni ya bodaboda inamtaka mwendeshaji bodaboda kuwa na kikundi, namba ya chombo chake iwe nyeupe na anatakiwa kuingia kituo cha kufanyia kazi nje ya jiji.

Pia MM amemsikia Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohammed Mpinga, akisema kikosi kipo katika msako mkali wa kudhibiti bajaj na bodaboda zinazokiuka sheria ya kuingia mjini.

Mkuu wa huyo amesema madereva wote wa bodaboda na bajaj wanatakiwa kufanya kazi pembeni ya mji kama ambavyo sheria zao za kufanya biashara zinavowataka.

Mbali ya viongozi hao, wapo wengine kama Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki na Kamshna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleimani Kova, wametoa maagizo  mbalimbali, tena makali, lakini bado boda hizo zinaingia mjini.

Uchunguzi uliofanywa na MM katika Jiji la Dar es Salam, hususan katika maeneo ya katikati ya jiji katika kituo cha daladala cha Posta Mpya, Jengo la Peugeot House na  maeneo kadhaa ya Kariakoo, umebaini kuwa vituo vya pikipipiki na vinaeandelea kubeba watu.

MM anajiuliza pikipiki hizo ni mali ya nani na kwa nini hazikaatwi kama alivyosema Kamanda Mpinga.

By Jamhuri