Nashawishika kuamini kuwa kama Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage

Nyerere, angekuwa hai, jambo moja kubwa ambalo angelipinga kwenye

Rasimu ya Katiba ya Tume ya Jaji Warioba ni la muundo wa Muungano.

Sidhani kama angekubali muundo wa Serikali Tatu.

Sina hakika kama Mwalimu angepinga mambo mengi mazuri ambayo Tume ya

Jaji Warioba iliyaweka kwenye Rasimu, lakini yamefyekwa kana kwamba

hayana maana kwa Tanzania ya leo na ijayo.

Alipoingia Ikulu mwaka 1995, Rais Benjamin Mkapa kazi yake kubwa ya

kwanza ilikuwa kuteketeza maelfu ya ngano ya tajiri mmoja. Kazi hiyo

ilifanywa na makamanda wa JWTZ. Naamini Rais ajaye mwakani, kazi ya

kwanza itakuwa kutupa mbali kabisa hii ‘Rasimu ya Sitta’.

Ibara 28 kwenye Rasimu ya Warioba zimefutwa kwa sababu pengine

kutokana na kupanguliwa kwa suala la kuwa na muundo wa Serikali Tatu.

Kwa maneno mengine, kukwazwa kwa mfumo au aina hiyo ya muundo wa

Muungano kumezifanya ibara nyingine zife kifo cha kawaida.

Hata hivyo, kuna ibara zilizofutwa na wabunge hawa katika mazingira

yanayotia shaka. Na hapa ndipo inapokuja hoja ya kwamba Katiba yetu

haikupaswa kutungwa na watu wenye maslahi nayo. Kwa mfano, tumeona

wabunge wakipigia upatu kuendelea kwa sifa ya ‘kujua kusoma na

kuandika’ kama sifa mama ya kuchaguliwa kuwa mbunge. Hapa hakuna shaka

kwamba mbunge ambaye ana aina hiyo ya elimu, hawezi kukubali kuona

sifa ya kuwa mbunge ikibadilishwa. Kuikubali maana yake ni kumwambia

akose ubunge.

Jaji Warioba na timu yake wamemaliza kazi yao. Najua wajumbe wengi

kwenye Tume hiyo wanasikitika. Wanasikitika kwa sababu wanaona kazi

waliyofanya imetupwa. Imeonekana haina maana. Kwa maneno mengine,

wajumbe hao wanaona wamefanya kazi iliyoshusha au kupoteza heshima

yao. Hili linawauma hasa miongoni mwao wanapoona namna jamii na

jumuiya ya kimataifa inavyowaheshimu.

Nawaomba Jaji Warioba na timu yake watulie kwa sababu sisi tulio huku

mitaani tunasikia maneno ya wananchi — maneno ya hasira. Wananchi

wanajiandaa kuiadhibu Rasimu ya Sitta. Kinachofanywa na waheshimiwa

hawa ni kuendeleza hila za kushika madaraka, basi. Wiki mbili zilizopita nilihoji weledi wa baadhi ya wabunge wetu katika kufikia mwafaka wa kupitisha rasimu hii ambayo sioni soni kuitambua kama rasimu mbovu kabisa.

Nitajaribu kueleza kwa uchache. Baadhi ya ibara zilizofutwa kwenye

Rasimu ya Warioba ni ya 15 iliyohusu zawadi wanazopewa viongozi wakuu

wakati wa utekelezaji dhima zao. Rasimu ilitaka zawadi anazopewa

kiongozi ziwe mali ya umma. Wabunge wamelikataa jambo hilo. Wanataka

mali ziwe za huyo aliyepewa. Rais akienda mgodini akapewa rushwa ya

kilo 10 za dhahabu, hiyo iwe mali yake kwa sababu ni ‘zawadi’ halali

aliyopewa! Hatari ya uamuzi huu ni kwamba rushwa sasa itatolewa kwa

mgongo wa ‘zawadi’. Haina tofauti na ile rushwa iliyoletwa kwa

msamiati wa ‘takrima’.

Ibara ya 17 ilitaka kiongozi wa umma pamoja na mke/mume na watoto wake,

aorodheshe mali na madeni yake kwa muda utakaopangwa kisheria, kwa

maana wakati wa kuingia na wakati wa kutoka tujue kavuna au kapoteza

nini. Hilo limepingwa. Kwa maneno mengine wanataka tuwe na waziri

anayeingia madarakani akiwa lofa wa mali, lakini baada ya kutoka

madarakani awe na ukwasi ambao hauhojiwi! Hawa ni wabunge walio karne

ya 21!

Ibara ya 20(1) ilipendekeza mali za kiongozi ambazo kazipata kwa

kukiuka sheria zitwaliwe ili ziwe za umma. Hilo wabunge hawa

wamelikataa. Hawataki kuliona katika Katiba. Kwa maneno mengine,

kiongozi anayekuwa madarakani aibe kadri anavyoweza kwa sababu hakuna

breki ya kumzuia iliyowekwa kikatiba.

Katika Ibara ya 103 kulikuwa na hoja njema ya kuona mawaziri na naibu

wao hawahudhurii vikao vya Bunge. Kwa maneno mengine mawaziri wasiwe

wabunge ili uwajibikaji wao uwe mkubwa na wenye tija kwa nchi. Hilo

waheshimiwa hawa wamelikataa. Wanataka mawaziri waendelee kutoka

miongoni mwa wabunge. Hili wamelikomalia kwa sababu ubunge wanautaka

na  uwaziri wanautaka. Kwa hiyo, kusema wawe wabunge tu ilhali na

uwaziri wanautaka, hawawezi. Na uwaziri wanapoutaka, na kama

ilivyokuwa kwenye Rasimu ya Warioba, ilibidi wabaki nje ya Bunge ili

pengine kwa dua na ndumba, waweze kuteuliwa kuwa mawaziri.

Lakini hapo hapo hakuna mwenye hakika asipogombea ubunge atateuliwa

kuwa waziri. Kwa hiyo, njia rahisi waliofanya ni kuona waziri anatoka

miongoni mwa wabunge; na kwa njia hiyo akikosa uwaziri, basi walau awe

mbunge. Wametega kote kote. Huu ni ubinafsi. Kama kweli tulidhamiria kupata Katiba nzuri, ilikuwa hawa wanaotunga hii Katiba wazuiwe kisheria kuwa kwa miaka walau mitano ijayo wasigombee ubunge. Bila shaka wangekuja na Rasimu ya maana.

Ibara ya 107 ilihusu Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu chini ya Katibu

Mkuu Kiongozi ambayo ingekuwa na dhima ya kuchambua na kulishauri

Baraza la Mawaziri juu ya masuala mbalimbali kabla ya kuwasilishwa na

kutolewa uamuzi na Baraza hilo. Hili nalo wamelikataa. Ibara hii

ilikuwa muhimu kwa sababu makatibu wakuu ni wataalamu; tofauti na

mawaziri ambao ni wanasiasa tu.

Kituko kingine kilichofanywa na Bunge hili ni kuifuta Ibara ya 129

iliyokuwa ikipendekeza kuwapo nguvu za kikatiba kwa wananchi kumwondoa

mbunge madarakani. Mambo ambayo yangeweza kuwafanya wananchi wachukue

hatua hiyo ni kama mbunge angeunga mkono sera zinazoenda kinyume cha

maslahi ya wapigakura, au maslahi ya Taifa; kushindwa kuwasilisha kero

za wapigakura, kuacha kuishi au kuhamisha makazi yake kutoka eneo la

Jimbo la Uchaguzi kwa miezi zaidi ya sita bila sababu za msingi; na

kadhalika.

Ibara hii ingesaidia kuondoa vilio vya wapigakura kwa sasa ambao

hulalamika kuwa hawaoni wabunge wao uchaguzi unapomalizika. Wabunge wengi wamekuwa wakiishi mijini kwa kisingizio kwamba huko ndiko wanakosaka misaada kwa ajili ya wapigakura wao. Hili wabunge wamelikataa kwa sababu wanajua ni hao hao watakaokuwa wabunge mwakani, kwa hiyo kutunga sheria ya kuwaondoa ni kuwaondolea uhondo wanaoufaidi bungeni. Haihitaji akili nyingi kubaini kuwa huwezi kumpa mlamba asali ajipangie muda anaotaka kuacha kulamba asali!

Ibara ya 253 ilikuwa na orodha ndefu ya watumishi ambao wasingekuwa na

haki ya kugombea, kuchaguliwa au kuteuliwa kushika nafasi za kisiasa

hadi unapopita muda wa miaka mitatu tangu kuacha au kustaafu madaraka

au nafasi aliyokuwa akishikilia. Humo wamo majaji, wakuu wa vyombo vya

ulinzi na usalama, makatibu wakuu, Msajili wa Vyama vya Siasa, na

kadhalika. Ibara hii, na nyingine, zimefafanuliwa vizuri sana kwenye

Bango Kitita. Hawa wakubwa wameliweka kando na sasa linaletwa kwa

staili tofauti kabisa. Wanataka hawa wanaosimamia wananchi kupigwa chini,

waking’atuka tu kwenye upolisi, waingie katika siasa. Ndiyo maana kuna

matendo mengi ya wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama kujipendekeza

kwa wanasiasa kwa sababu wana malengo mapana ya kuingia kwenye siasa

au bodi za mashirika ya umma, au kuteuliwa kuwa mabalozi!

Wabunge hawa hawa walipinga muundo wa Serikali Tatu kwa nguvu kubwa

sana kwa kigezo kwamba zingeongeza gharama za uendeshaji, lakini ni

wabunge hawa hawa ambao sasa wanapendekeza Bunge la Jamhuri ya

Muungano wa Tanzania liwe na wabunge 360 na wasiozidi 420! Wanapendekeza kuwapo kwa marais wanne — kwa maana ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Rais watatu.

Wameondoa Mamlaka ya Tume ya Utumishi wa Umma ambayo ingefanya kazi

kubwa ya kumpendekeza kwa rais majina ya watumishi wa nafasi mbalimbali. Badala ya kupunguza madaraka ya rais, wao wameongeza. Katiba ya majirani zetu Kenya imejitahidi sana kupunguza madaraka ya rais. Leo hii Rais Uhuru Kenyatta hawezi kuamka na kumtangaza Jaji Mkuu, Mkuu wa Jeshi la Polisi, na kadhalika.

Wenzetu wamefikia hatua ambayo kazi hizo zinaombwa na watu wenye sifa. Wanafanyiwa usaili hadharani huku vyombo vya habari vikirusha mahojiano hayo moja kwa moja. Sisi hapa hata uteuzi wa makatibu wakuu bado tunaiacha kazi hiyo ifanywe na rais mwenyewe. Bado tunataka hata mkuu wa Shirika la Masoko

Kariakoo ateuliwe na rais. Huyu rais atafanya kazi ngapi?

Lakini jingine linalotia hasira ni hili la kuwapo wagombea binafsi. Suala hili wameliruhusu, lakini kuna kila dalili kuwa fursa ya kuwapata wagombea binafsi itakuwa ngumu mno kutokana na masharti yanayoandaliwa. Moja ya mambo hayo ni kama lile la kuwapo muda maalum kwa anayetaka kugombea, wa kuwa amejitoa katika chama cha siasa.

Ndani ya mpango huu kuna hila za Chama Cha Mapinduzi (CCM) za

kuhakikisha wanachama wake wengi hawakihami chama hicho na kwenda

kugombea endapo majina yao yatakatwa kwa mizengwe kwenye vikao vya

vyama. Kwanini mgombea binafsi isiwe fursa huru kwa kila mwenye sifa.

Ndiyo, sheria na vigezo vinapaswa kuwapo, lakini havipaswi kuwakwaza

watu.

Kwa haya na mengine, ndiyo maana namsihi Jaji Warioba akae kimya. Sauti

zinazotolewa na wapinzani wake hawezi kuzikabili maana zimejaa kiburi na jazba. Kitu pekee kitakachopigana vita hii kwa niaba yake, ni historia. Na hiyo historia imo mwenye mioyo na bongo za Watanzania. Mijadala inayoendelea mitaani na katika mitandao ya kijamii inadhihirisha pasi na shaka kuwa wananchi, kwa idadi ya kutosha; wapo nyuma ya Jaji Warioba.

Tulidhani kupinga mfumo wa Serikali Tatu, kama kweli kulikuwa na hoja

ya kufanya hivyo, ndiko kungekuwa jambo kuu la wanaompinga Jaji Warioba, na si kufuta hata mambo kama ya uadilifu yaliyokuwa kwenye Rasimu yake. Rasimu ya Sitta imeandaliwa na wabunge kwa misingi ya ndoto za Chama Cha Mapinduzi kuendelea kuitawala nchi hii. Huo ni ubinafsi unaoweza kuliangamiza Taifa.

Kama wengine wamejipachika jukumu la kutaka Watanzania Rasimu hii kura ya ‘ndiyo’; kwanini iwe nongwa kwa wanaosema ipigiwe kura ya ‘hapana’? Sina kigugumizi kuwasihi Watanzania kwa kuwaambia; “Ikataeni Rasimu ya

Sitta”. Bado naamini rais ajaye baada ya Uchaguzi Mkuu mwakani, kama

kweli kwake Tanzania ni zaidi ya CCM au Chadema au CUF, ataitupilia

mbali rasimu hii iliyojaa ubinafsi.

By Jamhuri