Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh.Joachim Wangabo ameiagiza Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Sumbawanga (SUWASA) kuwakatia maji wateja wenye madeni sugu ili waweze kulipa madeni yao wanayodaiwa na taasisi mbalimbali za serikali nchini.

 

Amesema kuwa uendeshaji wa Mamlaka hiyo utaendelea kuwa mgumu endapo wataendelea kuwafumbia macho wateja wanaowadai na kushauri kuanza kuangalia namna ya kutumia kadi za “pre- paid” (malipo ya kabla) katika huduma hiyo ya maji ili kuzuia madeni yatokanayo na malipo baada ya matumizi.

 

“lazima muwabane walipe madeni, ni kama umeme kama mtu halipi Kata, na huku kata maji, kama umewekwa utaratibu basi uheshiumiwe huo utaratibu, nimesikia kwenye taafifa hapo kwamba kuna upungufu wa fedha makudsanyo madogo na matumizi makubwa na wakati huo huo mna madeni makubwa na watu hawalipi, kata,” Mh. Wangabo alisisitiza.

 

Ametoa kauli hiyo alipofanya ziara yake ya kwanza kwa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Sumbawanga (SUWASA) ili kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na mamlaka hiyo pamoja na kuufahamu kwa kina mradi wa Maji safi na usafi wa mazingira katika miji saba nchini Sumbawanga ikiwemo, chini ya MDG – Initiative unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya pamoja na Serikali ya Ujerumani wenye thamani ya Bilioni 31.

 

Aidha ameendelea kuwasisitiza Mamlaka hiyo kwa kushirikiana na Manispaa pamoja na vyombo vya usalama kuhakikisha vyanzo vya maji vinahifadhiwa na kupiga marufuku wale wote wanaofanya shughuli za kibinaadamu katika vyanzo vya maji na kuwachukulia hatua wale wanaokiuka sheria hiyo ya mazingira.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa SUWASA Hamis Makala amesema Mamlaka hiyo inadai taasisi za kiserikali Shilingi Milion 69 na pia inadai watu binafsi shilingi milioni 250 huku Mamlaka hiyo ikiwa inadaiwa shilingi milioni 100.6, na kuongeza kuwa miongoni mwa changamoto wanazozipata ni kukauka kwa vyanzo vya maji.

 

“Hadi Novemba mwaka 2017, SUWASA inadaiwa Milioni 100.6 kutoka kwa wadaiwa wake, mgawanyo wa madeni ni; Madawa ya Maji Shilingi Milioni 14.5, TRA Shilingi Milioni 13, EWURA Shilingi Milioni 6.8, Fidia Shilingi Milioni 32, TANESCO Shilingi Milioni 17, Mita za Maji Shilingi milioni 6, Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga Shilingi Milioni 11 kwaajili ya hati miliki,” Makala alifafanua.

 

Halikadhalika Makala alisema kuwa deni hilo limekuwa kubwa zaidi baada ya mkandarasi Herkin Builders kudai Shilingi Milioni 247.6 kama riba ya kucheleweshewa malipo ya kujenga mradi wa dharura wa maji safi Sumbawanga kati ya mwaka 2009 hadi March 2016.

By Jamhuri