Mawimbi ya sauti yanaingia kwenye sikio la nje kupitia mfereji wa sikio; hivyo kusababisha ngoma ya sikio na ile mifupa midogo midogo milaini sana ndani ya sikio inayojulikana kama ngoma ya sikio iliyopo katika sikio la kati kutetemeka.

Kutetemeka kwa ngoma ya sikio kunaruhusu mitetemo hii ya sauti isafiri hadi kwenye sehemu inayoitwa ‘koklia’. Koklia inapokea mawimbi ya sauti  na kusaidiana na  vinyweleo vidogo vidogo sana ( visivyoweza kuonwa kwa macho ya kawaida isipokuwa kwa kutumia kifaa maalumu cha hadubini) ambavyo vipo kwenye koklia, na vinyweleo hivi vinapeleka ishara ya sauti kwenye ubongo ndipo sauti inaweza kutafsiriwa.

Iwapo ikitokea sehemu yoyote kati ya hizi ikaharibika au njia ya sauti ikaziba, inaweza kusababisha matatizo ya usikivu. Inakadiriwa zaidi ya asilimia 20 ya Watanzania wana matatizo ya kutosikia vizuri na wengine kuwa viziwi kabisa.

Zipo zababu nyingi sana zinazosababisha matatizo haya. Tafiti zimethibitisha kuwa watoto wanaozaliwa na matatizo haya, yanachangiwa na aina fulani ya maisha ya mama zao wakati wanapokuwa wajawazito.

Tabia kama unywaji wa pombe na ulevi kwa ujumla, uvutaji wa sigara na baadhi ya vipodozi vikali kutumiwa wakati wa ujauzito vinamuathiri moja kwa moja mtoto akiwa tumboni, hasa ujauzito wa kuanzia miezi minne, ambapo mtoto anaanza kutengeneza neva za fahamu.

Kuna baadhi ya magonjwa yanayodumu kwa muda mrefu mwilini japo hayahusiani na homa za masikio, lakini yanaweza kusababisha matatizo katika kusikia. Magonjwa haya yanaweza kuleta hatari kwa kukorofisha mzunguko wa damu kwenye mfumo wa sikio (hasa sikio la ndani) kuelekea kwenye ubongo.

Magonjwa haya ni kama vile magonjwa ya moyo, kisukari hata saratani ya damu. Baadhi ya dawa zinaweza kusababisha kupoteza uwezo wa kusikia.

Asilimia kubwa ya dawa tuazozitumia kila siku katika tiba ya magonjwa mbalimbali, pamoja na ufanyaji wake wa kazi lakini pia zinaweza kusababisha hali nyingine tofauti kwenye miili yetu kama vile maumivu ya kichwa, uchovu, kichefu chefu, kutapika pia kupoteza uwezo wa kusikia.

Dawa hizi hasa ni zile tunazozitumia kutuliza maumivu kama vile Acetominophen, Asprin na zile zinazotumika kwenye tiba za saratani. Hata hivyo matatizo yanayotokana na matumizi haya ya dawa huwa ni ya muda tu, na baadaye mwili unakuwa sawa.

Magonjwa ya utotoni nayo yanasababisha kupoteza uwezo wa kusikia. Maambukizi ya sikio yanaweza kusababisha kujaa kwa utando mzito kwenye sikio la ndani na kusababisha matatizo ya usikiaji ambayo yanakwisha baada ya utando huu kuondolewa.

Maambukizi mengine yanaweza kusababisha uharibifu wa sikio la kati na hata sikio la ndani na kumfanya mtoto kuwa kiziwi kabisa. Magonjwa yanayoshambulia sana mfumo wa usikiaji kwa watoto ni kama vile tetekuwanga (chickenpox), surua, degedege na malaria sugu kwa watoto.

Wazazi wanashauriwa pia kuwapikia watoto vyakula vyenye lishe kwa wingi ili kuwakinga na magonjwa nyemelezi yatakayoathiri mifumo ya fahamu katika ukuaji wao.

By Jamhuri