Taifa Stars yawanyong’onyesha mashabiki

Mashabiki na wapenzi wa soka nchini wameiponda timu ya Taifa (Taifa Stars) kutokana na kichapo ilichopata kutoka timu ya Taifa ya Uganda (The Cranes).

The Cranes iliitandika Taifa Stars bao 1-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam wa kuwania kucheza fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani wanaocheza ligi za ndani.

 

Mashabiki na wadau wa mchezo huo kwa kutumia mitandao mbalimbali ya kijamii wameiponda Taifa Stars. Yupo aliyeandika maneno aliyopata kusemwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hasani Mwinyi kuwa Tanzania ni sawa na kichwa cha mwendawazimu ambacho kila mtu anajifunzia kunyoa.

 

Amendelea kusema kuwa maneno hayo yataendelea kuishi hadi Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) litakapoamua kuwekeza katikan soka la vijana na watoto.

 

Mwingine ameandika kuwa kama tumeshindwa soka sasa tutafute kuwekeza katika michezo mwingine.

 

Wachambuzi mbalimbali wa michezo nchini wanasema kufanya vibaya kwa timu hiyo kunatokana na TFF kushindwa kuwekeza katika mpira wa miguu.

 

Mmoja wa wachambuzi hao ni kocha mahiri wa soka nchini, Kenedy Mwaisabula ‘Mzazi’, ambaye alipata kulimbia JAMHURI kuwa Tanzania bado ina safari ndefu ya kufikia mafaniko katika soka kwa kulinganisha na mataifa ya Ulaya.

 

Mwaisabula ambaye amefundisha soka katika timu mbambali nchini jijini, amesema ili Tanzania ipige hatua katika soka, inatakiwa kuwekeza kwa  vijana, jambo ambalo halifanywi katika nchi nyingi za Afrika.

 

“Huwezi kusema unataka kuendeleza soka wakati hujawekeza katika soka la vijana, huo utakuwa ni utani au ndoto za mchana,” amesema.

 

Mwaisabula ambaye hivi karibuni alikuwa katika mafunzo ya muda mfupi ya ukocha nchini Ujerumani, amesema kuwa nchi hiyo imepiga hatua katika soka kutokana na kuwekeza kwa vijana.

 

“Nilipokuwa Ujerumani nimekuwa nikizungumza na wadau wa michezo hususan soka, waliniambia kuwa mafanikio yao yanatokana na kuwekeza kwa kuanzia kwa watoto wadogo.

 

“Nimekaa katika Timu ya Buyern Munich, kuna viwanja 19 vyote vimejaa vijana kutoka sehemu mbalimbali ya nchi yao.

 

“Kuna makocha wazoefu waliowahi kuchezea timu hiyo kama Rummenigge (Karl-Heinz Rummenigge Kalle) na wengineo, wanatumika vizuri ili kuwapa ujuzi wa soka vijana wadogo na baadaye kuja kuwa hazina ya timu hiyo na taifa la Ujerumani tofauti na hapa kwetu.

 

Amsema kuwa katika mafunzo yake amebaini kuwa timu hizo hazitegemei miradi ya mlangoni tu balia imekuwa zikibuni miradi mbalimbali katika kukuza uchumi wa timu.

 

Amesema  tofauti na hapa kwetu, jezi za timu zimekuwa zikiuzwa holela mitaani, lakini katika timu ya Buyern Munich imekuwa ikidhibiti uuzwaji wa bidhaa zake na fedha yote imekuwa ikiingia katika mfuko wa timu.

 

Amsema kuwa timu hiyo imebuni miradi mingi ikiwamo vifungashio vya funguo (key holders) mifuko ya Rambo na hata kiberiti kilicho na nembo ya timu hiyo ni mali ya timu na vimeandikishwa katika msajili wa makampuni ya nchi hiyo.

 

Hata hivyo, Mwaisabula anaisifu Timu ya Azam FC kuwa ndiyo timu ya mfano wa kuigwa hapa nchini, kutokana na mfumo na utaratibu wake wa kuwekeza katika soka.

 

Amesema Azam pamoja na kuendeshwa na mtu ambaye hakuwahi kucheza soka katika maisha yake, lakini anaendesha timu hiyo kitaalamu, hali ambayo  kama ataendelea nayo ataifikisha mbali timu hiyo, na soka la Tanzania katika kilele cha mafaniko.

 

“Azam ni timu iliyoanza juzi juzi tu, lakini hadi sasa imekuwa na uwanja mzuri wa mazoezi na ukumbi wa mazoezi ya viungo, tofauti na Simba na Yanga ambazo ni timu kongwe kisoka hapa nchi, lakini ni tofauti.

 

“Timu hizi ambazo tunatarajia kuwa ndizo zitakazofanya kazi kubwa ya kuinua soka kwa kuwa ni kongwe, na zina nafasi kubwa katika kuendeleza soka, badala ya kufanya hivyo zimeingia katika malumbano madogo madogo  yasiyo na tija kila mara, kwa mfano, sasa wameingia katika malumbano ya kukataa kuchukua fedha ya udhamini wa Azam.

 

Mzazi ameusifu mpango Chama Cha Makocha Mkoa wa Dar es Salaam, kuanzisha kozi ya makocha kwa kuwa inaweza kuinua soka nchini na kuitaka mikoa mingine kuiga mpango huo.

 

Amsema kuwa makocha hao watakapohitimu na kurudi mitaani, wataibua vipaji vingi katika maeneo yao na kuzifanya timu kubwa kutopata shida kuchukua wachezaji watakaowaona.

 

Kuhusu wachezaji wa kigeni, Mwaisabula amesema kuwa kwa sasa Tanzania inatakiwa kuwa makini katika kusajili wachezaji wa nje, kwa kuweka sheria itakazozitaka timu husika kusajili wachezaji wanaocheza soka katika timu za taifa kuliko hali ilivyo sasa.

 

Amesema hatua hiyo imesababisha timu nyingi kusajili wachezaji wa nje bila kufanya utafiti, na matokeo yake hujikuta wanachukua wachezaji wa mitaani wenye viwango vya chini kisoka.

 

“Naungana na kaka yangu, King Kibadeni kuwa kama ni kusajili wachezaji kutoka nje, basi awe ni yule anayechezea timu ya taifa na si kuwaokota mitaani, kama ni hao hapa wako wengi mno mfano kuna Haruna Niyonzima, huyu anacheza timu ya taifa ndiyo wanaotakiwa,” amesema.

 

Karl-Heinz ‘Kalle’ Rummenigg ametoka katika familia ya soka. Alizaliwa Septemba 25, 1955 katika mji wa Lippstadt.

 

Alijiunga na Bayern Munich mwaka 1974 alikitokea Westphalian Amateur Side, Borussia Lippstadt kwa ada uhamaisho ya euro 10,000.