Tuache kufyatua maneno – 2

 

Katika Kamusi hiyo, neno, ‘ari’ linaainishwa kuwa ni “hamu ya kutaka kukamilisha jambo na kutokubali kushindwa; ghaidhi, hima, nia, kusudio’. Hii ina maana kwamba matumizi ya neno ‘changamoto’ yameachanishwa na ufafanuzi wa Kiswahili.

Lifuate neno ‘uhaini’ ambalo lilitumiwa sana Januari mwaka huu katika kauli za kibabe, kejeli na matusi ya viongozi dhidi ya wananchi wa Mtwara waliohoji kuhusu rasilimali yao ya gesi asilia. Wanamtwara waliitwa wajinga, wahuni na hata wahaini na wachochezi.

 

Kifupi, neno ‘uhaini’ limetafsiriwa na Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyotajwa hapo juu kwamba ni njama za kupindua Serikali ya nchi. Adhabu ya uhaini katika Tanzania ni kifo kwa kunyongwa.

 

Kwa hiyo, mtu anayemshitaki mtu mwingine kwa uhaini bila kusoma na kuelewa maelezo ya kifungu 39 cha Kanuni za Adhabu, Sura 16 ya Sheria za Tanzania Bara, Toleo la 2002, ambacho kinaeleza kwa ukamilifu kosa la jinai la uhaini ni mpuuzi anayecheza na moto. Nani anaweza kusimama na kutoa ushahidi kwamba ni Wanamtwara wangapi walistahili kunyongwa hadi wafe? Kama wapo, kwanini hadi leo hawashitakiwi ili wanyongwe?

 

Vichaka vingine vinahusu matumizi ya maneno: mchakato, nyeti, na muda si mrefu. Mchakato maana yake ni mfululizo wa shughuli unaosababisha kitu fulani kufanikiwa. Muulize mhusika kama huo mchakato umeanza lini, wanaohusika ni nani na nani, na wangapi, jinsi zinazotumika, na kama utakwisha lini. ‘Nyeti’ ufafanuzi wake ni ‘l. -enye umuhimu wa hali ya juu kwa maslahi ya jamii au taifa 2. -enye kugusa hisia za watu au siri za serikali’. Uliza kama idadi ya jamii ni watu wapi na wangapi; kama watu hao ni jinsia gani, kama unyeti unalindwa na sheria gani. Kuhusu “muda si mrefu”, uliza muda unaanza lini na utaisha lini, na wanaoshughulika ni nani.

 

Labda tuombe Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) watusaidie. Maana Baraza hilo limedumu kwa miaka 46 tangu lilipoanzishwa na Sheria Na. 27 ya mwaka 1967, sura ya 52 ya Sheria za Tanzania, Toleo la 2002. Miongoni mwa madhumuni ya sheria hiyo, ni kwamba Bakita isimamie upatikanaji wa kiwango cha juu katika matumizi ya Kiswahili na kukatisha tamaa matumizi mabaya ya lugha hiyo. Sijui kama Bakita imeishasikia maneno haya yote ambayo nimeyazungumzia.

 

Kwa vyovyote vile, sijui kama Bakita, katika miaka 46, iliwahi kuchapisha Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Kwa kuanzia, inaweza kutueleza neno ‘changamoto’ lilitoholewa kutokana na ‘changa’ na ‘moto’.

 

Kwa kifupi, Watanzania tuwe na tabia ya kudadisi. Kuna wanaoshikilia kwamba Watanganyika ni Wadanganyika. Haya, shime, Wadanganyika wote tuendeleze udadisi kwa mdundo mmoja!

Novatus Rweyemamu

Wakili Mwandamizi

Simu: 0784 312623