Zanzibari kuna waislamu wengi na wakristo wachache sana, lakini katika uteuzi mbalimbali imewahi au imepata kusikika jina la mkristo likiteuliwa? Wakristo wa kule si wanahaki zile zile za ubinadamu na za uraia? Mfumo upi hapo kandamizi -ule Mfumo Kristo unaoogopwa upande wa Bara kama kandamizi kwa dini ya kiislamu au Mfumo Islam unaokandamiza kila dini isipokuwa uislamu kule Zanzibar?

Hebu tazama ile orodha ya walioteuliwa kwenye ile Tume ya Katiba ya Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba, utaona upande wa Bara wapo wakristo na waislamu, lakini kwa wajumbe wa kutoka Zanzibar, wajumbe wote 15 ni Waislamu tupu, hata mkristo mmoja hakuteuliwa! Hapa elimu ya uraia inataka tutafakari na kujifikiri kuwa Watanzania wote kwanza tu wazawa wazalendo ndipo tukaingia hizo dini za imani tulizonazo.


Aidha, napenda tukumbushane zaidi kuwa kule Marekani Rais wa Kwanza wa Taifa lile aliyeitwa George Washington wakati anawaaga Wamarekani mwaka 1789 aliwakumbusha raia wenzake kuwa dini pamoja na Serikali ni sehemu ya mfumo wa maisha.


Alisema hivi namnukuu, “Dini na uadilifu ni mambo ya lazima, itakuwa haina maana yoyote kwa mtu anayedai heshima ya uzalendo kama atafanya bidii kuhujumu mihimili hii muhimu ya furaha ya binadamu, ambayo ni nguzo imara za wajibu wa binadamu na raia”.


Hivyo tunaona hapo kuwa pamoja na utawala bora, lazima katika taifa kuwe na haki ya watu kutekeleza imani wanayoona kuwa ni lazima kwa ajili ya mihimili mikuu ya furaha ya binadamu (taz. Uhuru wa kidini kama Haki ya Binadamu juzuu ya 6 namba 2 uk. 2). Kila raia ana haki ile ile ya kufuata imani ya dini yake- iwe ukristo au uislamu- na Serikali iwatendee sawa raia wake wote bila kubagua imani zao.


Rais John F. Kennedy wa Marekani mwaka 1960 kabla ya kuapishwa Januari 20, 1961 aliwahi kuulizwa na waandishi wa habari, “Mr. President, you are a Roman Catholic, won’t you be taking orders from Rome to America?” Alijibu kwa tabasabu hivi; Ladies and gentlemen. Iam PRIMARILY an AMERICAN born an American – then I became a Roman Catholic”.


Je, wananchi wa Tanzania tunao uzalendo kama huo wa kusema mimi nimezaliwa Mtanzania kisha nikauvaa ukristo au uislamu? Kwa nini tunatanguliza imani ya kidini kuliko utaifa wetu? Hebu tulifikirie hilo. Tubakie na utamaduni wetu kama Waafrika, na hasa Watanzania -Mzaramo, Mngoni, Mhehe, mnyaturu, Mha, Msukuma, Mkurya, Mtumbatu, Mmakunduchi – wote ni Watanzania tu. Mwislamu au mkristu mwenye mbari ya Kiafrika aslani hawezi kufikiria imani ya dini yake kwa Mungu muumba wake itazidi akijifanya mzungu mweusi au mwarabu mweusi, la hasha! Kila muumini abakie kama alivyoumbwa na Mwenyezi Mungu.


Waislamu na wakristu huko mitaani tunaishi pamoja katika makazi yetu. Wakati wa ibara kila mmoja anakwenda kwenye jengo lake la ibada na kuabudu humo. Maisha ya mitaani kwetu kati ya watu wenye itikadi tofauti na wenye imani tofauti ningediriki kusema yanategemeana sana hata ingelinganishwa kisayansi kwa kutumia neno “SYMBIOSIS”, hivyo kuyalinganisha maisha yetu na kuita symbiotic life.


Wakristu na waislamu tunategemeana sana na hata Mtume (S.A.W) aliwahi kusema “…Na utawakuta waliokaribu kwa urafiki na waislamu ni wale wanaosema sisi ni wakristo” sura 5 aya ile ya 82 mstari ule wa pili -vipi leo waislamu kuwa na mihadhara, makongamano kuuchambua ukristo? Mbona ni kinyume cha matakwa na maagizo ya Mtume?


Ipo mifano kadhaa hapa nchini kuthibitisha ukarimu wa wakristo kwa ndugu waislamu. Kule Mtwara alikuwapo Padre mmisionari mmoja (Pd. Ildefons OSB) alijitahidi sana kuwa karibu na ndugu zetu waislamu. Waislamu kadhaa wamesaidiwa, mathalani kupaua na kuezeka misikiti yao, pengine kumalizia ujenzi wa misikiti iliyoonekana kukaa muda mrefu bila kukamilika, pengine hata kujenga nyumba mpya hizo za ibada ilimradi waumini wale waweze kuswali na kumtukuza Mungu. Misikiti kama Chikongola, ule wa Soko Kuu, ule wa kule Maurunga na ule wa Kitaya.


Kule Kanisa la Ndanda limemaliziwa kupaua na kuezeka Msikiti wa Wilaya hapo Ndanda. Huko Handeni Padre Odilo Hupper OSB amewanunuliwa vipaza sauti kwa ule Msikiti Mkuu wa Chanika Handeni na huko Butiama mkoani Mara Baba wa Taifa alitafuta fedha na akawajengea waislamu msikiti hapo Butiama. Ujenzi ule usilimamiwa na injinia aliyemalizia ujenzi wa nyumba ya Baba wa Taifa hapo Butiama mwaka 1999 (Brigedia Jenerali Mstaafu Urassa).


Songea Vijijini sehemu ya Morogoro Peramiho, Pd. Gerald OSB alijenga msikiti kwa waislamu. Matendo haya yanaonesha wakristo walivyo karibu na kuwa marafiki wa ndugu zetu waislamu.


Hadi leo sijawahi kusikia ndugu masheikh waislamu wanasaidia wakristu kwa ujenzi wa aina yoyote ile au kwa tendo lolote la kijamii. Ninafikiri katika utamaduni wetu huu wa kitanzania inawezekana sana tukasaidiana na wenzetu wakajaribu kuulea uhuasino namna hii (should reciprocate) kwa kuchangia nao.


Kinachoonekana wazi wazi ni kukashifu dini nyingine, kukejeli kubeza hata kuchoma moto nyumba za ibada kwa chuki walizojijengea kwa kurithi utamaduni wa kigeni. Pengine wanalipuka na kutamka TAKBIR! Basi vurugu mechi zinaanza. Baadhi ya waislamu wakiombwa misaada ya kifedha hujibu bila hata aibu, “Dini yetu hairuhusu kutoa fedha kwa shughuli za makanisa”.


Je, inaruhusu kuezekewa misikiti na watu wa dini nyingine kama wakristu? Hii ni ufinyu wa fikra (mayopic reasoning power) tu siyo imani ya kidini. Inafaa sasa kubadilika, tujisahihishe na tuishi kama Watanzania huru tuliokomboka hasa kifikra (mentally liberated).


Siku ya Maulidi nilifurahishwa sana na masheikh waliotoa mahubiri kwa waamini wao katika kusherehekea siku hiyo ya kuzaliwa Mtume (S.A.W).


Mkoani Dar es Salaam Sheikh Mkuu alitamka pale Mnazi Mmoja, “Waislamu watende matendo mema, waishi kwa upendo na amani na wenzao kama alivyofanya Mtume Mohammed (S.A.W)”.


Kule Kigoma Sheikh wa Mkoa alihimiza waislamu kutenda matendo mema na kuwa na uhusiano mzuri na wengine kama Mtume (S.A.W) alivyodumisha uhusiano mwema na majirani zake.


Katika kipindi cha dini katika TBC asubuhi ile, masheikh watatu jijini Dar es Salaam walijadiliana na kufafanua sifa za Mtume kuwa alikuwa NURU na MWANGA wa AMANI. Hii inadhihirisha kuwa waislamu wasomi huwa daima wanatafakari Qur’an na hadithi za Mtume (S.A.W) kisha huwaomba waislamu wote kufuata vile Mtume (S.A.W) alivyoagiza.


Tudumishe AMANI. Ikijatoweka tutasambaratika. Hatutakuwa na mahali pa kukimbilia. Leo nchi yetu inawarudisha wakimbizi wote wa mifarakano Congo DRC, Rwanda na Burundi. Sisi tukichafuana mnafikiri tutapokewa huko? Hapo patakuwa patashika nguo kuchanika. Mungu apishilie mbali balaa namna hilo. Waislamu na Wakristo tuishi pamoja kama watoto wa Mungu.

 

Tusiishi kama paka na panya. Vitimbwi, visingizio ni mawazo ya utamaduni wa kigeni, kamwe siyo IMANI YA kiislamu wala ya KIKRISTU! Udini Tanzania usiwe nongwa. Tusije tukakatana majambia bila sababu. Uislamu usiwe na tabia ile ya mbwa mwitu na kutafuta kila sababu za kuusukama ukristo. Sisi sote tuwe na tabia za kimungu – na tuige pia zile tabia za Mtume (S.A.W) za upendo, uvumilivu masikilizano na umoja katika ulimwengu huu.

 

Mkristu ni kiumbe cha Mwenyezi Mungu na mwislamu ni vivyo hivyo. Sote ni wamoja kiasilia (we have a common denominator), basi tusifuate tofauti za kigeni na tusikubali zitutenganishe. Mila na desturi za asili za Watanzania ziko tofauti sana na mila na desturi za wageni wote waliotuletea dini hizi mbili ukristu (uzungu – Magharibi) na uislamu (uarabu – Mashariki ya Kati).


Jamani udini kamwe usiwe nongwa hapa nchini. Tusiwe manokoa wa wageni wowote wale kwa suala hili la imani za kidini.


Kule Geita Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Assemblies of God – Mathayo Kachila aliuawa, Uchunguzi wa Polisi bado unatafuta ukweli wa tukio hilo. Al’Jazeera katika taarifa zake za habari Jumamosi ya Februari 16, mwaka huu usiku ilionesha kule Sri Lanka wananchi wanalizungumzia suala namna hii la uhalali wa kuchinja na walikuwa wanajadili kwa jazba kubwa.


Jumapili ya Februari 17, 2013 majira ya asubuhi kule Zanzibar lilitokea jambo la kutisha na kustaajabisha sana. Vyombo vyote vya habari, radio, runinga na magazeti hata SMS katika simu zetu za mikono, habari hii ya kutisha ilitangazwa Padre Evarist Mushi, Paroko wa Kanisa la Minara miwili, mjini Zanzibari, Kathedrali la Askofu, amepigwa risasi tatu kichwani na kufariki dunia papo hapo. Huyu Padre alikuwa anajiandaa kwenda kutoa sadaka ya misa katika Kigango cha Mt. Theresia Mtoni, Jumapili ya kwanza ya KWARESIMA.


By Jamhuri