Mamia ya wahamiaji wa Kiafrika waishio nchini Israel wameandamana huku wakiendelea na
mgomo wa kutokula wakipinga sera mpya ya Israel yenye utata ya kutaka ama kuwafunga na
kisha kuwarejesha makwao.
Wahamiaji hao walitembea umbali mfupi kutoka kituo cha wazi cha Holot hadi gereza la
Saharonim, wakipaza sauti na kutoa ishara za kutaka kuachiwa kwa wafungwa wenzao ambao
wapo magerezani nchini humo.
Mhamiaji mmoja kutoka Afrika nchini Eritrea, Muluebrhan Ghebrihimet mwenye miaka 27,
aliyewasili nchini Isreal miaka sita iliyopita, amezishutumu mamlaka za nchi hiyo kwa kukataa
kumpa uraia licha kuomba miaka mingi iliyopita.
“Tuko hapa kuomba hifadhi na siyo kufanya kazi au kusaka utajiri.” amesema kijana huyo
ambaye alikuwa ni miongoni mwa maelfu ya waandamanaji wanaopinga ukandamizaji dhidi ya
wahamiaji nchini humo.
Wimbi la wahamiaji kutoa Afrika liliwasili Israel mwaka 2007, wakivuka mpaka kwa kupitia rasi
ya Sinai nchini Misri. Hata hivyo, njia hiyo isiyo salama ilikuja kudhibitiwa kwa kiasi kikubwa na
kukomesha wahamiaji kuingia nchini humo.
Wahamiaji hao wengi wao wanaishi katika vitongoji maskini kusini mwa Tel Aviv, mji mkuu wa
kibiashara wa Israel, lakini uwepo wao umesababisha msuguano na wenyeji kiasi cha
kusababisha hali ya kutokuelewana.
Serikali ya Israel yenye mlengo wa kulia imeshutumiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa
la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), wasomi na makundi ya haki za binadamu kuhusu mpango
wake kuhusu wahamiaji walioko nchini humo.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Mambo ya Ndani, Israel ina wahamiaji karibu 42,000 wa
Kiafrika, nusu yao ni watoto, wanawake na wanaume wanaoishi nchini humo wanaotarajiwa
kurejeshwa makwao.
Nchi hiyo inajiandaa kuwarejesha maelfu ya wahamiaji wa Eritrea na Sudan walioingia nchini
humo kinyume cha sharia, na ambao maombi yao ya kuomba hifadhi hayako chini ya uchunguzi
wa kama wanastahili kuishi nchini humo.
Hata hivyo, serikali imewapatia chaguo, kuondoka nchini humo hadi kufikia mapema mwezi
Aprili, au kukabiliwa na kifungo jela na kisha kurejeshwa makwao baada ya kutumikia kifungo,
hali inayoendelea kusababisha mvutano.

By Jamhuri