Waziri akanusha ripoti kuwa Kenya haina fedha

Waziri wa Fedha Henry (kushoto)
Waziri wa Fedha Henry (kushoto)

Waziri wa Fedha Kenya Henry Rotich amesema Alhamisi kuwa ripoti zinazodai kuwa serikali ya nchi hiyo haina fedha ni “habari feki” na kuwa serikali kawaida haziwezi kukosa fedha.

Ameongeza kuwa shilingi bilioni 200 zilizotolewa hivi karibuni na Eurobond zitaweza kukidhi mahitaji ya taifa hilo.

Amesema ripoti hizo zinamakosa kwa kusema serikali haina fedha, limeripoti gazeti la The Daily Nation nchini Kenya.

Vipi mkurugenzi mtendaji mkuu wa kampuni isiyokuwa na fedha anaweza kuendelea kufadhili miradi mbalimbali? Amesema imemshangaza.

Waziri amesema kuwa mifumo mingine inatayarishwa kupunguza kiwango cha muda ambao huchukua kuwalipa wagavi (suppliers).

Hivi sasa wizara inafanya kila iwezalo kuhakikisha wazabuni wote wanalipwa katika kipindi cha siku 90.

Rotich alisema Jumatano kuwa serikali inakabiliwa na matatizo kadhaa katika kufadhili baadhi ya miradi yake ya maendeleo.

Rotich aliweka wazi pendekezo la kupunguza matumizi ya mabilioni ya fedha zilizokuwa zimetengwa kwa kaunti kadhaa ambazo ni kati ya shilingi bilioni 15 na shilingi bilioni 17.

Wakati akiongea mbele ya kamati ya fedha na bajeti ya Baraza la Seneti Jumatano, Rotich amesema hali hiyo inatokana na mamlaka ya mapato Kenya kushindwa kukusanya kodi kwa kufikia malengo waliopewa katika makadirio ya ukusanyaji wa kodi yaliyopitishwa.

“Tumezungumza na KRA juu ya njia bora ya kufikia udhibiti wa ukusanyaji kodi kamili kwa pato la ndani ya nchi na pato la bidhaa zinazoingia nchini,” Rotich ameiambia kamati hiyo inayoongozwa na Seneta wa Mandera Mohamed Maalim Mahamud.

Waziri ameongeza kuwa; “tunahitaji kulizungumzia suala hili pamoja (maseneta) na magavana kwamba kiwango cha mapato tunachojadili siyo rahisi kukusanya kutokana na changamoto nilizozielezea.”

Katika mwaka wa fedha 2018, shilingi bilioni 302 zilikuwa zimetengwa kwa kaunti za serikali 47 katika uwiano uliosawa wa mapato yaliyokusanywa, ikimaanisha kuwa katika hali mbaya kabisa ya kiuchumi, mgawanyo huo ungeweza kupungua kufikia shilingi bilioni 285.