MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Tanzania Bara, Stephen Wasira, amewaonya wanachama walioanza harakati za kusaka urais mwaka 2030 kwa kuwa muda wa kufanya hivyo bado haujawadia, hivyo wanaofanya hivyo wanakiuka kanuni, miongozo na utaratibu.
Amesema kuanza mapema harakati za kusaka uongozi kabla ya wakati inaweza kukigawa Chama badala ya kukijenga hivyo inapaswa kukemewa.
Wasira ameeleza hayo leo Mjini Bunda Mkoa wa Mara alipokuwa akiweka jiwe la msingi ujenzi wa jengo la ofisi za CCM Wilaya ya Bunda ambazo zilichomwa moto katika na vurugu za Oktoba 29, 2025.
Alisema ndani ya Chama kuna kundi la wanachama ambao hawana kazi za msingi ndani ya CCM zaidi ya kujihusisha na makundi ya kisiasa.

Kwa mujibu wa Makamu Mwenyekiti Wasira, kundi hilo limeanza kujipanga kwa kuunda safu kuanzia ngazi za kata, hali ambayo inaweza kusababisha mgawanyiko ndani ya CCM kwa kuwa kila mmoja anataka kuwa na wafuasi wake badala ya kuimarisha umoja.
Wasira alihoji uhalali wa baadhi ya watu kuanza kujitangaza mapema kuwania urais wa 2030, akisema hakuna anayeweza kujihakikishia uwepo wake hadi wakati huo.
“Unazungumziaje urais wa 2030 leo, wakati hata hujui kama utakuwepo? Hiyo ni kama kumjaribu Mungu. Wakati huu tunapaswa kujikita kwenye kazi za kujenga Chama na nchi,” alisisitiza.
Aidha, alionya tabia ya baadhi ya watu kutumia fedha kushawishi wanachama maskini kuungwa mkono, akieleza kuwa hali hiyo ni hatari na inaweza kuharibu maadili ya Chama.




