Mkurugenzi wa Mikakati na Maendeleo wa Shirika la REEEP, lenye makao makuu Vienna, Austria, Bw. James Smith amesema Shirika lake limepokea msaada wa Euro milioni 5 sawa na Shilingi bilioni 15 kuzisadia kampuni za Kitanzania kuongeza uzalishaji wa bidhaa za chakula hususan kilimo kwa kutumia nishati mdabadala.
Amesema hayo alipofanya mazungumzo na Mhe. Naimi S.H. Aziz, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Vienna tarehe 18 Februari, 2026 kwenye ofisi za Ubalozi Vienna.
Bw. Smith alieleza kuwa, Shirika hilo limepokea msaada wa Euro milioni 5 sawa na Tzs Bil. 15 kutoka Serikali ya Austria kwa ajili ya kuwezesha Kampuni na Mashirika nchini Tanzania kuongea uzalishaji wa bidhaa za chakula hususan kilimo kwa kutumia nishati mbadala. Alieleza kuwa, Kampuni na Mashirika mbalimbali nchini yameomba kutekeleza miradi kupitia fedha hizo, na kwamba Shirika hilo liko katika hatua za mwisho wa uhakiki wa Kampuni na Mashirika yaliyoomba ili kupatiwa fedha hizo. Timu ya wataalam kutoka Shirika hilo unatarajia kuwasili nchini Tanzania mwezi Machi, 2026 kwa ajili ya kukamilisha taratibu za uhakiki.
Upatikanaji wa fedha hizo ni matokeo ya sera nzuri za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na utekelezaji wa diplomasia ya uchumi.
REEEP ni shirika la kimataifa linalofanya kazi ya kupeleka na kuharakisha (accelerate) matumizi ya nishati katika nchi zinazoendelea. Shirika lilianzishwa mwaka 2002 ikiwa ni matokeo ya Mkutano wa Kilele wa Dunia wa Maendeleo Endelevu uliofanyika Johannesburg, Afrika Kusini mwaka 2002.



