Na OWM KVAU
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Bi. Mary Maganga amewataka Watumishi wa Ofisi hiyo kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi ili kuongeza tija katika utoaji huduma kwa wananchi.
Bi. Mary amebainisha hayo leo Oktoba Mosi, 2025 mkoani Morogoro wakati alipofungua Kikao Kazi cha watumishi wa Idara ya Kazi na Kitengo cha Huduma za Ajira kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Idara hizo.

Ninataka mfanye kazi kwa ushirikiano, ubunifu na uwajibikaji ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika usimamizi wa masuala ya kazi na huduma za ajira nchini alisisitiza Katibu Mkuu huyo.
Awali, Kamishna wa Kazi Ofisi hiyo, Bi. Suzan Mkangwa, amesema kuwa kikao hicho kimehusisha watumishi kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara, ambapo watajadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta kazi na ajira.
Naye Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira Bi. Josephine Matiro amesema kikao hicho ni fursa muhimu ya kujadili changamoto na mafanikio yaliyopo pamoja na kubadilishana uzoefu wa kitaaluma ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kujadili kwa kina utekelezaji wa majukumu ya idara hizo pamoja na kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu namna bora ya kuboresha utendaji kazi.

